Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Female
Party
CCM
Constituent
Special Seats
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
1
Ministries
nil
MHE. NYAMIZI S. MHOJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ya kuchangia Wizara hii ya Katiba na Sheria. Kwanza kabisa ninamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha sisi sote hapa kwa uzima na afya njema. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ninapenda kuipongeza Wizara, kiukweli inafanya kazi nzuri sana. Tumesikiliza taarifa yake hata taarifa ya Kamati pia inafanya kazi nzuri sana. Mfano mzuri ninampongeza Waziri kwa kuanzisha siku maalum ya sema na Mheshimiwa Waziri; kwa hiyo, ile ni nafasi ya pekee ambayo wananchi wanaitumia kwa ajili ya kueleza kero zao zinazohusiana na sheria. Kwa hiyo, ninawapongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuweka huduma ya uwakili kwa makundi maalum ikiwemo watu wenye ulemavu. Kwa kweli watu hawa, watu maalum, mfano wenye ulemavu unakuta hawana pesa ya kumlipa wakili au unakuta mwananchi wa kawaida hana uwezo wa kumlipa wakili, lakini Wizara imetoa hiyo huduma bure kwa haya makundi. Kwa hiyo, ninaipongeza sana Wizara sana, sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine pamoja na pongezi hizo kuna ambao wamesema kwamba Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria, Fungu la 101 kwamba taarifa inaonyesha walitafsiri sheria mbalimbali kutoka lugha ya Kiingereza kuja ya Kiswahili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, sijasikia kwamba walitafsiri lugha ya watu wenye ulemavu, mfano, nukta nundu kwa wasioona kwa sababu wako wanasheria wengi sana wasioona, nadhani tunashuhudia kwamba wako mawakili pia wasioona. Sasa tusipotafsiri lugha hii kwenye nukta nundu kwa kujali haya makundi inaweza ikawa siyo ujumuishi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nina imani kwa kupitia hii ninadhani wanaweza wakaboresha zaidi katika hilo kama hizo nukta nundu hazipo. Pia katika hili nina imani niko sehemu sahihi kulizungumzia, Tanzania iliridhia Mkataba wa Umoja wa Mataifa kuhusu haki za watu wenye ulemavu iliridhia mwaka 2009 na ilipaswa ku-submit ripoti ile initial report kwa sababu na sisi Tanzania ni wanachama. Kwa hiyo, ile initial report ilitakiwa ikabidhiwe baada ya miaka miwili na baada ya hapo inatakiwa ku-submit progress report kila baada ya miaka minne.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa hivi naona process haifiki mwisho. Kwa lugha nyingine hata ukiangalia kwenye ile link hakuna ripoti ya Tanzania kuhusiana na masuala ya watu wenye ulemavu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hilo pia yako mambo mengi mno ambayo nchi kama nchi imefanya kwa watu wenye ulemavu. Sifikirii kwamba hakuna kabisa, hapana! Maendeleo ni hatua, huwezi ukafananisha watu wenye ulemavu wa sasa hivi na wa miaka ile 2000 au miaka ya nyuma, kuna maendeleo hasa ukizingatia kwa Mheshimiwa Rais huyu Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan, amefanya mambo mengi sana; ukiangalia kwenye sekta ya elimu, ukiangalia kwenye afya, lakini bado kwenye uwekezaji kwenye dira tumejumuishwa mambo mengi sana matamu mazuri ya kuripoti kama nchi kwa masuala ya watu wenye ulemavu. Mpaka sasa tunaonekana hii Nchi ya Tanzania haifanyi chochote kuhusiana na mambo ya watu wenye ulemavu, lakini si kweli. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninaomba sana tuangalie namna ya kuripoti, kwa sababu tunavyozungumza sasa hivi hiyo USRPD ilitakiwa turipoti taarifa nne ukijumisha na ile initial report na tunakoelekea sasa hivi USRPD hiyo imeshaboreshwa tuko kwenye ADP ambayo na yenyewe tunatarajia Serikali iweze kuridhia kwa ajili ya kutekeleza mambo ya watu wenye ulemavu kwa muktadha wa Afrika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maana ile USRPD ilikuwa kwa Kimataifa haiendani na mazingira ya Tanzania au ya Afrika. Kwa hiyo, wamekaa wameona hapana tutengeneze hii mkataba mwingine ambao ni itifaki ADP kwa ajili ya watu wenye ulemavu kwa muktadha wa mazingira yetu kama Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaomba Serikali pale inapokwama sijui inakwamia wapi kwa nini isiripoti mambo mazuri mazuri, matamu ya watu wenye ulemavu na sisi tunajivunia na siyo tu sisi Serikali hata wadau wanazitumia hizi ripoti, wadau NGOs, CBOs na wadau wengi wanaojishughulisha na masuala ya watu wenye ulemavu, wanatamani nchi kama nchi itoe ripoti ambayo na wao itawasaidia katika mambo yao na activity zao za kuwaendeleza watu wenye ulemavu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hilo pia kuna Tume ya Kurekebisha Sheria, Marekebisho ya Sheria ya Watu Wenye Ulemavu Na.9 ya 2010 iko haiendani na mazingira ya sasa hivi: mazingira ya sasa hivi mfano kama sasa hivi yako ujasiriamali, wako TEHAMA yaani mambo mengi ambayo yameendelea kwenye ile sheria na ile sheria tunahitaji iboreshwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wamesema kwamba wamerekebisha sheria mbalimbali; tulikuwa tunaomba pia kama haipo Sheria ya Watu Wenye Ulemavu na ni kweli haipo ninaomba pia iweze kurekebishwa. Tunaomba Wizara watusaidie tuweze kurekebisha ili mambo yetu na sisi yaende vizuri yaendane na kasi ambayo ipo ya sasa hivi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hilo pia tunaishukuru Tume, ukisoma Ibara ya 12, 13 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; inasema hakuna aliye juu ya sheria. Kwa hiyo, hata hili suala linaenda moja kwa moja kwa Mahakama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi watu wenye ulemavu siyo kwamba hatutendi makosa, wapo wanaotenda makosa na wanaadhibiwa kwa sababu hakuna aliye juu ya sheria, yapo magereza je, yale magereza ni rafiki kwa watu wenye ulemavu? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba wawaangalie, lakini pia kuna sheria ambazo zipo zinafanyika kule magereza; ukiangalia mimi ninatumia vifaa saidizi: vifaa saidizi ni chuma na ukiangalia sheria za kule zinaweza zikanizuia nisiingie na gongo au kifasaidizi changu. Matokeo yake mwisho wa siku inakuwa inatweza utu wa watu wenye ulemavu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimeongea kwa mjumuisho katika hilo suala na nina imani Serikali yetu ni sikivu, nina imani Wizara wanafanya kazi vizuri sana, nina imani kabisa kwa sababu kama alikuwa hamjui basi wanajua kwa ajili ya kutekeleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaendelea kupongeza sana Wizara kwa mambo makubwa ambayo wanaendelea kuyafanya kama Wizara sisi watu wenye ulemavu tunawapongeza sana, tuna imani na wao, tuna imani na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye amewapa hii kazi wasaidie katika kazi hii ya sheria. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna imani mambo yetu ya watu wenye ulemavu hayatakwama badala yake yatasonga mbele hatua kwa hatua, maendeleo ni hatua. Tuna imani sasa hivi na tunakoelekea tulikotoka ni tofauti na kila kitu; sheria ndiyo msingi wa kila kitu. Kwa hiyo, tusipoangalia sheria tukaziweka vizuri na sisi watu wenye ulemavu tutakuwa hatujajumuishwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna imani kabisa sheria zikikaa vizuri, sheria zikieleza vizuri watushirikishe pale ambapo wanaona hapa tunahitaji mawazo mengine, sisi tupo ambao ni wataalam, tumebobea na masuala haya ya watu wenye ulemavu kama Waheshimiwa Wabunge tutasongesha mbele mambo ya watu wenye ulemavu hasa katika sheria. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunisikiliza. (Makofi)
MWENYEKITI: Mheshimiwa, ahsante kwa mchango wako.
MHE. NYAMIZI S. MHOJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaunga mkono hoja. (Makofi