Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Female
Party
CCM
Constituent
Special Seats
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
1
Ministries
nil
MHE. LUCY S. D. KOMBANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sana kwa kunipatia nafasi hii ili niweze kuchangia. Kwanza ninawapongeza sana Wizara kwa harakati wanazoendelea kufanya kuhakikisha kwamba elimu ya Tanzania inazidi kukua siku hadi siku. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ninapenda kumpongeza na kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kufadhili walimu 150 kwenda India ili wakajifunze mafunzo ya ufundi stadi. Hili ni jambo kubwa sana kwa sababu tunajua kama tunataka kuendelea kwenye mambo haya ya sayansi na teknolojia, lazima tujifunze kwa nchi ambazo zimeendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda Waziri atakapotoa majibu yake atwambie uwiano wa kimkoa. Hawa watu 150 mikoa mingine imeshirikishwaje, kama yote imeshirikishwa ni walimu wangapi walioenda hususan Mkoa wangu wa Morogoro? Kwamba, kati ya walimu 150, hawa ni wangapi wamekwenda kupata haya mafunzo India? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuongezea kwenye hili, tunaelewa kwamba sayansi, teknolojia tunajifunza kwa nchi ambazo zimeendelea, ninamwomba Waziri ashirikiane na Mabalozi wa Tanzania wa nchi mbalimbali kutafuta exchange programmes. Tunajua programu hizi zinawawezesha walimu na wanafunzi waende nje ya nchi kujifunza vitu mbalimbali na mara nyingi hizi programu wanagharamia zile shule husika za nje ya nchi. Kwa hiyo, ili kupeleka hili zoezi kwa uharaka na kuokoa gharama, basi wasaidie kufanya hivyo. Pia, hili zoezi la exchange programme mara nyingi huwa motisha kwa walimu na wanafunzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine nililokuwa ninataka kuchangia ni suala la msawazo wa walimu. Walimu wengi sasa hivi wako mijini wanakimbilia mjini. Hali za vijijini siyo nzuri kabisa, utakuta kuna mwalimu mmoja na mwalimu huyu labda kasomea Kiswahili na English, lakini kutokana na uhaba, huyu mwalimu analazimika afundishe hisabati au sayansi, hiki kitu siyo kizuri kwa ustawi wa mwanafunzi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kinaleta stress kwa mwanafunzi kinaleta stress kwa Mwalimu, Mwalimu ili afiche ile weakness yake sasa ana-develop ego defence mechanism. Utakuta likifika somo la hesabu anaingia na fimbo nyingi mno, kwa hiyo, yule mtoto akiona zile fimbo hata kuelewa kwenyewe inakuwa ngumu. Tuangalie huu msawazo wa walimu, walimu wapelekwe vijijini ili kila mwalimu afundishe somo alilolisomea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sula lingine ninalotaka kuongelea ni ustawi katika elimu kwa mtoto wa kijijini. Tunahimiza udahili wazazi wanaandikisha watoto, lakini kwa hali ilivyo kwa kijijini kwa kweli inakatisha tamaa. Utakuta mtoto kaanzishwa darasa la kwanza, inaanza kwanza mzazi hana hata uwezo wa kumnunulia viatu, lakini huyu mtoto utakuta anatembea umbali mrefu kwenda shuleni, akifika shuleni anakaa chini, hajamaliza kukaa chini anashinda na njaa siku nzima. Tujiulize je, huyu mtoto ndiyo mtu mzima ambaye atafikia vizuri hii dira tunayoiongelea ya 2050? Wizara iangalie namna ya kumrahisishia maisha huyu mtoto wa kijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ambalo ninataka kumaliza nalo na kushauri Wizara, Profesa ninatamani sana, katika mitaala yetu ifike mahali mitaala iendane na mazingira ya shughuli za kiuchumi za jamii husika. Ninatokea Ulanga, kule tunayo madini mbalimbali tunachimba, lakini leo hii ukichukua rubi ukanichanganyia na chupa ninashindwa kutofautisha na Ulanga ni kwetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninatamani sana, kwa mfano sisi Ulanga tunachimba madini, basi mtoto kuanzia elimu ya msingi afundishwe vile vitu vya pale. Ninatamani sana mkulima wa mpunga Malinyi, huyu mtoto aanze kufundishwa kuanzia umri mdogo. Mimi siyoni haja ya kuendelea kulisoma sikio na sehemu zake zote za ndani ambalo hadi leo hii halijawahi kunisaidia, hicho kitu basi tungejifunza kwenye kutambua labda mbegu ya mpunga imekaaje na inafanyaje. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye sehemu za wafugaji hivyo hivo, watoto wajifunze kuanzia wadogo, kwamba ufugaji unakuwaje, ng’ombe huyu anatoa vitu gani, anatoa nyama. Ng’ombe huyu hatakiwi kuchapwa sana ngozi itaharibika na hizi ngozi tunatumia kwenye kutengeneza mabegi. Huyu mtoto afundishwe kwamba ng’ombe huyu hatakiwi kwenda kumlisha kwenye shamba la mtu mtatafuta ugomvi. Hivi vitu vingetusaidia sana zaidi ya kusoma vitu ambavyo ni vya sehemu ambazo hazituhusu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ifikie mahali tusiwe na wananchi ambao vichwani tumelishwa vitu vya kigeni, halafu wale wageni wanatoka kule wanakuja kutumia rasilimali zetu ili kuendelea kimaisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kufikia hapo, ninaomba niunge mkono hoja. (Makofi)