Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Female
Party
CCM
Constituent
Special Seats
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
1
Ministries
nil
MHE. AISHA M. MDUYAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa nafasi hii. Ninaanza kwa kuwapongeza Wizara, Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Manaibu Katibu Wakuu, Menejimenti ya Wizara, pamoja na Watumishi wote wa Wizara na Taasisi zake. Kubwa zaidi ninapenda kumpongeza na kumshukuru Rais, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa mageuzi makubwa sana aliyofanya katika elimu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepata Sera ya Elimu ya Mwaka 2014, Toleo la 2023, Sera ambayo imeleta maono makubwa katika nchi yetu. Kwanza tumeona tuna Mtaala unaojumuisha masomo ya amali, lakini pia, tumeona tumeongezewa lugha; mbali ya Kiswahili na Kingereza, Lugha ya Alama pia, inatambulika kama lugha rasmi ya kujifundishia na kujifunzia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna lugha nyingine kama brail, pamoja na lugha ya mguso kwa wenzetu wenye uziwi na kutoona; hongera sana na shukrani sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. Mbali na hiyo tumeona pia, sera imekuja na miongozo minne, ikiwemo Mwongozo wa Shule ya Nyumbani. Ninapongeza kwa sababu, inawapa nafasi wanafunzi wenye mahitaji maalum ambao hawawezi kufika shule nao waweze kupata fursa sawia za kusoma, kama wenzao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninatoa pendekezo katika utekelezaji huu, bado jamii kubwa sana haijaweza kuufahamu huu mwongozo. Tunao wanafunzi wengi wenye mahitaji maalum ambao wako nyumbani, lakini hawapati fursa ya kujifunza. Hivyo basi, ninashauri Wizara iweze kuangalia ni kwa namna gani uelewa unazidi kuendelezwa kwa jamii ikiwemo walimu ambao ndiyo watekelezaji, lakini pia, wazazi na walezi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hiyo pia, Wizara ione ni kwa namna gani wataweza kuwawezesha walimu hawa usafiri na posho, kwani tunajua mwongozo huu unatekelezwa nje ya muda wa shule. Pia, kwa mapenzi mema ya Rais wetu ameweza kuruhusu wanafunzi kurudi shuleni, wakiwemo wale ambao walisitisha masomo kwa changamoto za ujauzito, tukapata re-entry guideline. Bado uelewa wa mwongozo huu haujafika kwa jamii kwa ukubwa wake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona kwamba, kuna urasimu mkubwa sana ambao mabinti hawa wanaupata pindi wanapotamani kurudi shule. Mbali na hapo kwa wale wanaorudi shule bado mazingira ya shuleni hayapo sawa, kuna ubaguzi kutoka kwa wanafunzi wenzao, lakini pia, sehemu salama ambayo wanaweza kuwahifadhi watoto wao kipindi wao wako shule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaendelea pia, kuipongeza Wizara kwa nafasi nyingine ambazo wanaendelea kufanya. Ninaomba nichangie pia katika suala la teknolojia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona kwamba, Wizara ya Mawasiliano inafanya kwa ukubwa wake kuendeleza huduma ya internet katika jamii, lakini ninaishauri Wizara ione ni kwa namna gani teknolojia inafika shuleni. Hii itapunguza gharama za uchapaji wa vitabu, wanafunzi watapa vitabu kwa njia ya E-books na pia, itaharakisha upatikanaji wa vitabu hivi, hasa kwa wale ambao wako pembezoni mwa miji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la elimu jumuishi, ninajivunia tumepiga hatua kubwa sana, hasa katika masuala ya miundombinu. Tumeona ni kwa namna gani Serikali inaboresha miundombinu, ninaomba bajeti iweze kuongezwa katika elimu jumuishi, hasa kwenye vifaa saidizi vya kujifunzia na kufundishia. Tuone ni kwa namna gani wanafunzi hawa wanapata vifaa hivi ambavyo vinaendana na uhitaji wao, vifaa ambavyo havitowaongezea wenyewe ulemavu, bali vitawasaidia katika kupata elimu yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiwa ninahitimisha ninaiomba Serikali, pamoja na kushukuru kwamba, Mheshimiwa Rais ametoa ajira mpya za walimu, lakini pia, ione ni kwa namna gani walimu hawa wanakwenda kuongezwa, hasa walimu wa masomo ya sayansi, masomo ya amali na masomo jumuishi. Hii inaenda sambamba na kuona ni kwa namna gani walimu hawa wanapatiwa mafunzo ya elimu jumuishi ili waweze kwenda kufundisha wanafunzi hawa ambao wengi wao hawana changamoto na wale ambao wana changamoto katika shule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia ninaomba kuunga mkono hoja. Ninawatakia Wizara kila la kheri katika utekelezaji wake. Ahsante. (Makofi)