Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Chato Kaskazini
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
1
Ministries
nil
MHE. CORNEL L. MAGEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ninaanza kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi, ili niweze kutoa mchango wangu katika Wizara hii ya elimu, ambayo tunajadili kupitisha bajeti yake. Kwanza ninaomba nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambaye kwa kweli, kwa kiwango kikubwa ameifanya Tanzania sasa imekuwa ni miongoni mwa nchi ambazo Kimataifa zinaonekana zinakwenda kasi katika hii sekta ya elimu. Tunamshukuru na kumpongeza sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, ninaomba nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Profesa Adolf Mkenda Pamoja, Naibu Waziri wake, pamoja na watendaji wote wakiongozwa na Katibu Mkuu. Kwa kweli, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Elimu, Waziri pamoja na wasaidizi wake wamekuwa wakitoa ushirikiano mkubwa sana kwetu sisi Kamati, lakini kwa niaba ya Bunge zima ambalo sisi ni wawakilishi wenu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kazi yao wanayoifanya, ukienda kupitia mambo ambayo wameyaleta leo hapa Mezani kwa kweli, hata hizi fedha shilingi trilioni 2.3 ambazo wanaomba tuziidhinishe zikawe matumizi katika Wizara hii, mimi binafsi naona bado ni kidogo sana. Kama inawezekana, basi ninaomba Bunge lako hili Tukufu liangalie namna nyingine na kuishauri Serikali itafute fedha nyingine ya kuiongezea Wizara hii kwa sababu, ina mambo makubwa inayokwenda kutekeleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Awamu ya Sita ilipoingia madarakani toka mwaka 2021 ukienda kule vijijini mabadiliko ambayo utakutana nayo kwenye vijiji vyetu na kwenye Kata zetu ni mambo ya kupigiwa mfano ambayo hayajawahi kutokea toka tumepata uhuru katika nchi yetu hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kuangalia shule za msingi ambazo zimeanzishwa mpya bila involvement ya mwananchi mwenyewe kuchangia fedha yake ni shule nyingi sana huko tunakotoka. Ukienda pia kwenye shule za sekondari kwa maana ya sekondari mpya pamoja na madarasa ambayo yamejengwa na miundombinu mingine kwa kweli Serikali ya Awamu ya Sita imefanya kazi ya kutukuka na ya kupigiwa mfano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kikubwa zaidi ambacho kimefanyika ni kuja na mpango huu wa kuhakikisha kwamba kila wilaya tunakwenda kupata VETA na ambayo leo hapa tulikuwa tunaambiwa zaidi ya vyuo 64 ambavyo vinajengwa na vinaelekea kwenda kukamilika viko karibu 67%, viko kwenye hatua nzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka nikuhakikishie na kulidhbitishia Bunge lako Tukufu kama Mjumbe wa Kamati ile, tumekwenda tumeona kwa macho kazi nzuri ambayo inafanyika ika katika miradi hiyo na insha Allah inakwenda kukamilika, ninadhani baada ya kupata kazi hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Chato ni moja ya Wilaya ambazo zimenufaika na mipango mingi ya Serikali ya Awamu ya Sita. Chato imepata shule nyingi za sekondari, imepata shule nyingi za msingi, lakini tumekwenda mbali zaidi sisi tumepata VETA kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika shule hizi za sekondari zilizojengwa nitoe ushauri kwa Wizara, ni kwamba tumejenga sekondari nyingi, wananchi maeneo mengine wamehamasika wameanzisha shule za sekondari, lakini katika sekondari hizo ambazo zimejengwa na wananchi pamoja na zilizojengwa na Serikali, sekondari hizi hazina maabara katika shule zenyewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niishauri Serikali na Wizara yenyewe kwamba tukitaka kufanya vizuri na kupata vijana ambao watakuwa ni wazuri watakaokwenda kwenye vyuo vyetu vile vya VETA ambavyo vimeanzishwa kwa wingi, tunaomba Wizara ijikite kwenda kukamilisha maabara zinazokosekana katika sekondari zile.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, katika Jimbo langu la Chato Kaskazini, kwenye Kata 14 ninazo shule zaidi ya shule 19 za sekondari, katika shule 19 zile shule 12 hazina maabara kabisa. Shule zile zimekuwa zikifanya vizuri zimekuwa zimeanza kufanya kazi, leo ni miaka mingine takribani miaka mitano, miaka minne na kadhalika. Sasa ninaiomba Wizara sana kwamba wakati inakwenda kupeleka pesa zile za matumizi kwenye shule hizi, kwenye sehemu ya sekondari. Ninaomba katika shule hizi zifuatazo katika Jimbo langu la Chato wazingatie kuziletea maabara ili watoto wale waweze kupata elimu vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, shule ya kwanza ambayo ina tatizo kubwa la maabara ni Shule ya Sekondari Mwelani, Shule ya Sekondari Mkungo, Shule ya Sekondari Bukamila, Shule ya Sekondari Nyambiti, Shule ya Sekondari Itale, Shule ya Sekondari Rubambangwe, Shule ya Sekondari Katende, Shule ya Sekondari Ilyamchele, Shule ya Sekondari Buhingo, Shule ya Sekondari Kasenga, Shule ya Sekondari Nyambogo na Shule ya Sekondari Nyamirembe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana Mheshimiwa Waziri wakati unakwenda kugawa fedha hizi na ninaomba kwenye shule zile tuweze kupata angalau tujenge maabara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu mwingine kwa Wizara ni kukamilisha ile miradi ambayo imeanzishwa na Wizara. Iko miradi mingi ambayo imeanzishwa imepeleka fedha nyingi. Kwa mfano, pale Chato kulianzishwa shule ya watoto wenye mahitaji maalum, ile shule imepeleka zaidi ya bilioni nne ambazo zimetumika, leo hii ni miaka mitatu shule ile imeshindwa kufunguliwa kwa sababu tu imekosa shilingi 900,000,000 lakini shilingi 400,000,000,000 imekwishatumika, shilingi 900,000,000 ndiyo imekosekana ya kwenda kukamilisha shule ile.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana Waziri kwamba wakati unakwenda ku-wind up utueleze watu wa Chato, shule ile ni ya watoto wenye mahitaji maalum kwa Tanzania kwa sababu ziko shule tatu tu ambazo zilianzishwa katika nchi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wale watoto wanahitaji kusoma, lakini leo ukienda kwenye shule ile majengo yameanza kuchakaa. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anakwenda ku-wind up ahakikishe kwamba anatueleza hiyo shule ya Chato inakwenda kuanza kufanya kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili kwenye miundombinu na kwenye maeneo ambayo ujenzi ulikuwa umeshaanza, Mkoa wa Geita hatuna tawi la chuo kikuu, lakini kulikuwa kumeanzishwa na Wizara kwenda kujenga Tawi la Chuo Kikuu cha Dar es Salaam pale Chato kwenye eneo la Kasagara, lakini mpaka sasa hivi nikwambie yule mkandarasi aliyekuwa amepewa kazi hiyo ya kwenda kuanzisha ujenzi wa chuo kikuu kile alishabeba mitambo, alishabeba kila kitu akaondoka, ameacha eneo lile. Eneo lile lilichukuliwa kwa wananchi na wananchi wakapata fidia yao, lile eneo sasa wanataka wananchi kuanza kuvamia na kwenda kuendeleza shughuli zao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri kwamba, tawi la Chuo Kikuu cha Dar es Salaam linapaswa lijengwe pale Chato, ninaomba sana Mheshimiwa Waziri atakapokuja basi atusaidie.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba yake pia Mheshimiwa Waziri amezungumza kwamba wanakwenda kuanzisha maktaba, Chato kulianzishwa ujenzi mkubwa wa Maktaba ya Taifa…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Muda wako umekwisha Mheshimiwa.
MHE. CORNEL L. MAGEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, dakika moja. Maktaba kubwa ya Taifa ilianzishwa pale, ambapo maktaba ile itakapokwisha itasaidia watu wengi na wanafunzi wengi kutoka kwenye shule nyingi ambazo zinazunguka Mji wa Chato na vyuo vikuu ambavyo tunatarajia kuvianzisha pale, kipo Chuo cha IFM, kipo Chuo cha Utumishi wa Umma.
MWENYEKITI: Mheshimiwa Ahsante kwa mchango wako.
MHE. CORNEL L. MAGEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana na ninaunga mkono hoja. (Makofi)