Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. Nyamizi Simon Mhoja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. NYAMIZI S. MHOJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa. Kwa kuokoa muda ninaomba nijielekeze mchango wangu katika mambo mawili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza nitagusia Tume ya Utumishi wa Umma na Watu Wenye Ulemavu; mwaka wa fedha 2025/2026, Tume ilipangiwa fedha takribani milioni 500 na fedha hizi mpaka kufikia Februari mwaka huu 2026, Tume hii haikupokea hizi pesa. Hizi pesa ziliwekwa kwa ajili ya ujenzi wa mfumo wa kielektroniki wa kushughulikia rufaa za watumishi wa umma na malalamiko yanayotolewa na watumishi wa umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yameongelewa mengi kwa watangulizi waliotangulia, watumishi wa umma wako kila sehemu na endapo mfumo huu utaanzishwa na kufungwa utawezesha watumishi kufikia rufaa na malalamiko yao moja kwa moja kwenye Tume na siyo kupitia kwa mwajiri ambavyo ilivyo sasa hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukumbuke kwamba hizi ofisi ziko kikanda na hazipatikani moja kwa moja kwenye kila halmashauri. Kwa hiyo, huyu mtumishi anapotaka kukata rufaa kwa malalamiko yake kupitia huu mfumo endapo ungefungwa, basi huyu mtumishi kwanza tutampa uhakika wa suala lake la malalamiko la kiutumishi, kwamba limefika sehemu sahihi kwa sababu atajaza kwenye mfumo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtumishi ambaye yuko kijijini kule au yuko mbali, kumfikishia mwajiri lalamiko lake kwa kweli wakati huo tukumbuke kwamba hawaelewani, kuna sintofahamu kati yao, kwa hiyo kila mtu anajiona kwake ni bora kuliko mwenzake. Kwa hiyo, ukiwepo huu mfumo ninashauri Serikali hii pesa itolewe ili huu mfumo uweze kuwekwa kwa ajili ya manufaa ya watumishi wa umma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijielekeze pia kwa watu wenye ulemavu. Kwa mujibu wa sheria ya watu wenye ulemavu Na.9 ya 2010, Kifungu cha 27, kinamtaka mwajiri aliyeajiri watu kuanzia 20 ahakikishe kuwa asilimia tatu ya wafanyakazi wake ni watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili kiukweli, kwanza tunaipongeza Wizara kwa kuendelea kupambania watu wenye ulemavu kuingia katika ajira, lakini tunaomba iweze kuboresha kidogo. Kwa sababu ukiangalia hii sheria na idadi ya watu wenye ulemavu ambao wanamaliza chuo ni wachache sana, ilitakiwa hata mtaani kusiwepo na watu wenye ulemavu ambao wanahangaikia ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukimwona mtu mwenye ulemavu amemaliza degree yake anatafuta kazi, kwanza tu kufikia ile elimu ni kwamba amepambana vya kutosha mpaka kufikia pale, tukumbuke kwamba Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa watu wenye ulemavu kwa kweli anapenda kutupa kipaumbele. Si tu hivyo tu ni kwa sababu ya mazingira mbalimbali ambayo tunayapitia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni kuwa Sekretarieti na Wizara husika, tunaamini Waziri Ridhiwani na Naibu Waziri wake wanafanya kazi nzuri sana na hicho kitu hakikwepeki, wanamsaidia vizuri Rais, lakini katika hili tunaomba mwendelee kutupa kipaumbele, watu wenye ulemavu wako mtaani, kwa hiyo watafaidika nao angalau wapate elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaishukuru pia hii Wizara kwa sisi watu wenye ulemavu kwenye mfumo wa HCMS pale kwenye dashboard kwa kweli Wizara hii imetutambua. Kwamba Afisa Utumishi anaposhughulikia file labda la mtumishi Nyamizi anajua kabisa Nyamizi pale imeonyesha ni mwenye ulemavu. Kwa hiyo, tunashukuru kwa kututambua hivyo, pia ninaomba mambo yetu, masuala yetu, utawala bora uende pia kwa ajili ya kurahisisha na mambo yetu, kurahisisha angalau kupunguza makali ya maisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende haraka haraka pia kwenye suala la Pay as You Earn kwa watu wenye ulemavu nilikuwa ninaomba Wizara kwa huko nyuma, ninakumbuka kuna Rais ninadhani alipunguza Pay as You Earn, ninaomba kwa nini tunataka tupunguziwe Pay as You Earn au saa nyingine kuweka zero kabisa, kwa sababu kuna gharama ambazo ukiwa tu mwenye ulemavu unaingia utake usitake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumbuka tunatumia vifaa saidizi vinahitaji ukarabati wa mara kwa mara, umetumia mguu bandia mara nyayo imegeuka unarudi hospitali, kwa hiyo kuna zile hela ambazo zinaingia tu kwa sababu tu ya ulemavu, hii inazungumzia kwa mtumishi mwenye ulemavu. Kwa hiyo, Serikali tufikirie kwamba hawa watu tuwapunguzie hii Pay as You Earn au kuiondoa kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili litakuwa si la kwanza kwa Tanzania hata kwenye nchi za jirani ambazo sisi ni wanachama pia kwenye SADC na East African Community, mfano mzuri Kenya. Kenya katika hili suala la watumishi kwenye kodi hii Pay as You Earn wameondoa wameweka zero kabisa hawalipi. Kwa hiyo, nina imani Serikali yetu ni sikivu na itasikia, Waziri yuko pale na Naibu Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina imani hili suala litaenda vizuri kwa sababu tu kuna gharama ndugu zangu, kwa sababu tu ya muda ninashindwa kueleza zaidi, ukiwa mwenye ulemavu kuna gharama kubwa unaingia, hata kufika pale kazini, yule mwenye ulemavu anatumia gharama kubwa kufika ofisini, tofauti na mfanyakazi ambaye hana ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo Wizara pia inaweza ikatufikiria watu wenye ulemavu kwenye kuongeza muda wa kustaafu. Kuna mamlaka ambayo ninajua wameongezewa kwa sababu zao wanazifahamu. Kwa upande wetu sisi ninarudia pale pale kwamba ukiwa mwenye ulemavu, nimeanza kusoma darasa la kwanza. Mfano, mwenye ulemavu ambaye anazaliwa nao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo mbalimbali mfano mtu asiyeona, analazimika aeleweshe nukta nundu kabla ya kuendelea na masomo mengine. Kwa hiyo, inamaanisha anatumia muda mwingine, ataelewa ile herufi, lakini bado masuala ya nukta nundu hataelewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile viziwi na wenyewe pia lugha ya alama, watoto wale wanafundishwa kujua ile lugha ya alama. Kwa hiyo najikuta nakuja kumaliza chuo nina miaka 30 mpaka 35, lakini asiye na ule mlemavu amemaliza chuo na miaka labda 20 mpaka 25 kwa hiyo, naona hapo utofauti, tunachoangalia hapo ni uwiano tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tukiongezewa muda wa kustaafu watu wenye ulemavu tutashukuru sana kwa ajili ya ku-cover ule muda ambao tumepoteza kwa ajili ya ulemavu, tumehangaika kwa ajili tu ya kuhangaikia masuala ya watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kusema hayo, ninaunga mkono hoja na ninashukuru sana kwa kunisikiliza. Ahsante. (Makofi)