Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mkutano wa Tatu - Kikao cha Thelathini na Sita - Tarehe 25 Mei, 2026

Hon. Lucy Simirya Kombani

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mkutano wa Tatu - Kikao cha Thelathini na Sita - Tarehe 25 Mei, 2026

MHE. LUCY D. S. KOMBANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ili niweze kuchangia bajeti ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora. Mchango wangu utajikita kwenye ustawi na mslahi ya watumishi, nikianza na watumishi wa ajira mpya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipongeza sana Wizara kwa kasi wanayoenda nayo kwenye kuajiri. Ni kasi nzuri na hata ukiangalia kwenye mitandao ya kijamii feedback ni nzuri, watu wameridhika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiendelea na mchango wangu ni kwamba, hili zoezi la kuajiri ni zoezi ambalo linaanza kwa hatua mbalimbali kwamba, tunaangalia sehemu ambayo ina uhitaji wa watumishi, tunatangaza hizi kazi, wanafanya interview na wanaenda kwenye vituo vyao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kumetokea sintofahamu moja kwamba, mtumishi anaenda kituo chake cha kazi, hela za kujikimu hana na kuna wengine wanalalamika mishahara inachelewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara iangalie tatizo ni nini? Kwa sababu, mchakato wa kuajiri ni mrefu na unachukua miezi mingi kwa nini linapofika suala la watu kupata hizo hela iwe tatizo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku zote hizi ajira, hasa za utumishi wa umma, kitu cha kwanza ni kutengeneza mindset yake. Sasa anafika eneo, kwa mfano kijijini kama kwetu Malinyi kule au Ulanga, hela ya kujikimu hana na majibu anayopewa atafute namna ya ku-survive. Jamani mtumishi huyu anakuja na nia nzuri ya kutenda kazi, kufanya kazi, kuhudumia jamii, lakini kwa kitendo tunachomtendea sisi waajiri mwisho wake anakuja kukengeuka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ninalotaka kuchangia ni kuhusu mashauri ya rufaa yanayoenda Wizarani. Ninapongeza Wizara, inafanya kazi nzuri, hasa pale inapochakata na kushughulikia mashauri ya rufaa hadi mtumishi ambaye anonekana ameonewa anapata haki yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu ndiyo utu ambao Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, anausema, lakini ikizungumzwa kwa upande mwingine, bado kuna malalamiko kwamba, kuna madai yanachukua muda mrefu sana. Tukumbuke, jamani Wizara, dai linapokuja huku mtumishi anakuwa tayari ameshapewa adhabu, aidha kapunguziwa mshahara au kashushwa cheo na wengine wanakuwa nje ya ofisi. Hii hali ina-frustrate sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunapozidi kuchelewesha haya madai, hizi rufaa, kwa kweli inakuwa si kitu kizuri. Ninaiomba Wizara sasa iangalie namna ya kukaa vikao ku-fast track hizi rufaa na haki zipatikane kwa watumishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikizungumzia upande mwingine ni, kumekuwa na observation hizi rufaa zikifika utumishi kuna issue nyingine inaonekana mtumishi ameonewa, kwamba, wakati anahukumiwa huku chini Sheria za Utumishi wa Umma hazikuzingatiwa. Likifika huko, linarudishwa mtumishi ameshinda ile rufaa arudishwe kazini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ninaomba Wizara iangalie, sometimes utumishi wa umma kuna watu tu na agenda zao binafsi wanawaumiza hawa watumishi. Tujiulize, je, ni watumishi wangapi hawajui utaratibu wa rufaa? Hawajaja kukata rufaa na wamefukuzwa kazi wapo nyumbani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Wizara iangalie na endapo kama ikithibitishwa, hizi rufaa, mtu amemhukumu mtu ndivyo sivyo, basi na huyo aliyehukumu achukuliwe hatua kutokana na miongozo ya utumishi wa umma. Uzuri utumishi wa umma tunaongozwa na miongozo, sheria pamoja na sera, siyo mtu tu ana maamuzi yake kichwani, anakuja anafanya vitu anavyojua mwenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la tatu ninalotaka kuzungumzia, nitalitoa kwenye Sera ya Menejimenti ya Ajira katika Utumishi wa Umma, Toleo Na. 2 la Mwaka 2008. Nitajikita kwenye aya ya 4.11 na nitanukuu tamko namba nne na tamko namba tano. Tamko Na.4 linasema: “Waajiri wataweka utaratibu utakaowarahisishia watumishi wao kuwahi kazini na kurudi kazini.” Tamko Na.5 linasema: “Waajiri wawawezeshe watumishi kupata unafuu wa kupata makazi.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikizungumzia Mkoa wangu wa Morogoro; ninashukuru Waziri ana-fast track hili suala la kujenga nyumba za watumishi, lakini niaomba watukumbuke Morogoro. Morogoro ni mkoa mkubwa sana na jiografia yake kwa kweli, kwa mgeni, inaweza ikamtia sonona.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna wilaya zetu za mbali, Ulanga, Malinyi, kuna Wilaya kama Mvomero; mtumishi unaajiriwa unaenda kule haujui pa kukaa. Kwa kweli, utumishi wa mtu huyu unaanza vibaya kwa hiyo, tunaomba katika nyumba hizo, Mheshimiwa Waziri, atukumbuke Mkoa wa Morogoro, hasa kwenye majimbo haya ya mbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia taasisi zetu zina mipango ya motisha na mikataba ya hali bora. Hii mikataba ya hali bora imeleta sintofahamu mbalimbali kwamba, tasisi moja inapatiwa kitu fulani, taasisi nyingine haipatiwi kitu fulani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ameongea hapa ndugu yangu, Mheshimiwa Nchimbi, amesema kuna tendency ya watu kukimbia taasisi moja kwenda nyingine kwa sababu ya maslahi, lakini chimbuko la hiki kitu linaanzia kwenye mikataba ya hali bora. Kwa hiyo, Wizara iangalie kwenye upitishaji wa mikataba ya hali bora kusiwe na double standard, kama taasisi inapatiwa kitu hiki na taasisi nyingine ipatiwe kitu hicho hicho, ili tupunguze hii ya watu kutaka kuhamia kwenye taasisi moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia ninapenda kuunga mkono hoja na ninashukuru sana. (Makofi)