Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. John John Nchimbi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. JOHN J. NCHIMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa nafasi hii uliyonipatia. Kwanza kabisa ninaungana na mwenzangu aliyepita kuipongeza na kuitakia kheri kwa mwaka mpya wa fedha unaokuja Wizara ya Utumishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizi pia ninapenda kuwapongeza katika maeneo machache. Moja, ni kuendelea kuimarisha kwa utoaji wa huduma kwa umma, hasa kupitia e-Government. e-Government imekuwa ikitatua matatizo mengi sana ya Watanzania na inawapunguzia adha mbalimbali. Pia ninapenda kuwapongeza katika eneo la uwajibikaji, hasa upokeaji wa malalamiko kwa kuanzisha mtandao wa kupokea malalamiko na wananchi wengi wanapeleka malalamiko yao kule na yanachukuliwa hatua zinazostahiki na wanajibiwa kwa wingi inavyowezekana; kwa hili pia nipongeze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho pia ninapenda kuwapongeza kwa kuendeleza na kuwezesha kukaribia kufikia hatua ya 50/50 kati ya akina mama na akina baba katika utumishi wa umma. Hili ni jambo kubwa sana na pengine tunaweza tukawa tunaongoza katika Afrika Mashariki katika kuwasogeza akina mama katika nafasi hizo na wamekuwa ni msingi wa utumishi bora katika Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na haya, nitakuwa sijatendea haki nafasi yangu kama sitatoa ushauri kidogo ili na wao waone wapi pa kwenda kurekebisha na wapi pa kupaangalia vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kwanza ninachopenda kukiongelea hapa, bado kuna changamoto sana ya upungufu wa walimu maeneo ya vijijini na wafanyakazi wengine kama wa afya na kadhalika. Maeneo ya vijijini yana upungufu mkubwa sana na maeneo ya mijini na wizarani wamejaa watumishi wengi sana. Ninaifahamu wizara moja ina watumishi kama 60 lakini maafisa utumishi wapo 14. Nilikuwa nawauliza mnafanyaje kazi? Wanasema kuna wiki unaweza ukawa hujagusa file hata siku moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hawa watu wanatakiwa watawanywe na kutengenezwa usawazishaji ili waweze kwenda vijijini. Sasa, hii ni kazi ya Utumishi kufahamu nani yupo wapi, anafanya kazi gani na anafanya kwa mazingira gani. Hii lazima Utumishi waifanye, ni kazi yao muhimu sana ili kuweza kufanya maeneo ya pembezoni yaweze kupata watumishi wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2010 tatizo hili lilionekana, kwamba maeneo ya vijijini watumishi hawapendi kukaa kwa sababu mazingira ni magumu, sehemu nyingine hamna nyumba, hamna chochote. Serikali ilianza mchakato wa kutoa mwongozo wa kuwapatia motisha wale walimu na watumishi wengine wa afya na kadhalika, wanaokaa mazingira magumu maeneo mbalimbali. Mwongozo ule ulipita na mpaka leo haujaanza kutekelezwa; lakini wenzetu wa Utumishi wameendelea kuwahamisha watumishi vijijini na kuwaleta mijini badala ya kuwatekelezea mwongozo huu ili wabaki kule kule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa huu mwongozo ninafikiri umefikia wakati sasa kwa Mawaziri hawa ninaowaona na kasi yao utekelezwe ili kuwapatia motisha watumishi walioko maeneo ya vijijini waweze kukaa, walioko maeneo yenye mazingira magumu waweze kukaa na kufanya kazi na kulitumikia Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulianzisha utaratibu wa kupima utendaji kazi kwa kutumia PEPMIS; ule utaratibu umeanza kutumika na sasa ninafikiri ni mwaka mmoja na kitu. Ninadhani ni wakati muafaka wa kwenda kuupitia upya. Utaratibu ule kwa sasa na nao umegeuka kuwa kazi, kwa sababu mtumishi anatumia masaa mengi kuujaza ule mfumo; na nchi yetu ina maeneo mengi hayana mtandao, inabidi wapande pikipiki na baiskeli kwenda sehemu za mbali kwenda kujaza ili wasikose vyeo kwenye upandishaji wa vyeo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Daktari mmoja wa Muhimbili ananiambia alikuwa anafanya surgery ya wagonjwa 14 kwa wiki, imebidi apunguze mpaka 13 ili ajaze mfumo wake wa PEPMIS asije akakosa cheo. Mfumo wa PEPMIS umegeuka kuwa kazi badala ya kitendea kazi cha kupima performance. Waende kwa watumishi watawaeleza haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninatoa rai kwa Utumishi wajipunguzie kazi. Wanafanya kazi nyingi sana ambazo wangeweza kuzifanya zikafanywa kwenye taasisi na kadhalika. Kwa mfano, mashirika ya umma tangu miaka ya 1961, mzee wangu Profesa hapa atatuambia, wamekuwa wana bodi zao, wanaajiri wenyewe, wanatengeneza succession plan, watumishi wanakua. Sasa hivi Utumishi imenyang’anya ile inaajiri kwa niaba yao. Wale waliwekwa ili wawe semi-government autonomies, waweze kushindana na private sector.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ukimchukua mwanasheria kutoka kwenye halmashauri yangu mimi, ambaye amezoea kukusanya kodi, unampeleka aende aka-vet mikataba kwa sababu yeye ni senior, hawezi kuwa mwanasheria sawa na yule aliyezoea kupitia mikataba. Hata kama ni mwanasheria, lakini professionally, mme-grow up tofauti, lazima mwende katika yale maeneo yenu. Sasa, Utumishi hawezi kuwa jack of all trades, anataka aende huku aajiri, aende huku aajiri, aende huku ahamishe, atoe huku apeleke huku. Hiyo inawafanya kule kunakuwa kuna weakness kubwa na Utumishi wenyewe wanashindwa kuangalia masuala ya msingi, wanakuwa wote wanagombania kupeleka watumishi maeneo yenye maisha bora zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barua za watumishi za malalamiko, barua za kupanda vyeo wakiwa wameonewa na kadhalika zikienda Utumishi zinakaa mpaka mwaka mmoja hazijajibiwa. Maafisa utumishi wanaogopa kuyasema haya kwa sababu wanaogopa ni mabosi wao. Sasa, leo tunaona tuwaambie, watengeneze utaratibu wa siri kuwafuata watumishi wakawaoneshe jinsi ambavyo barua zao zinaachwa kujibiwa zaidi ya mwaka ndani ya utumishi. Hili jambo ninadhani likiwa sasa kwa kasi mpya ya Mawaziri wapya ninaamini litakwenda kurekebishwa bila tatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahamisha watumishi bila kuangalia weledi wao. Mwaka jana au mwaka juzi, kuna nurse amekwenda India kusoma miezi sita, robotic surgery ambazo nchini kwetu ndiyo zinaingia. Amekaa miezi sita kwa gharama zetu sisi akisoma robotic surgery, amerudi amekaa mwezi mmoja kapata barua ya Utumishi, akahamishiwa damu salama kwenda kukusanya damu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa, kwa haya tutanyamaza vipi? Ni kwa sababu Utumishi wanakaa pale mezani wanaanza kuhamisha, peleka huyu, peleka huyu! Hawafanyi consultation na Wizara Mama, hawafanyi consultaion na mashirika, hawafanyi consultation na Wakurugenzi wa Halmashauri kujua yule wanayemuhamisha ana umuhimu gani kule wanakotaka kwenda kumtoa. Sasa hii haiwezi kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahitaji nchi hii kuwa na Salary Board itakayokuwa inasimamia mishahara ya watumishi wa umma. Sasa hivi Wabunge watakuwa ni mashahidi, kila ndugu yake anayemjua anakufuata anamwambia nihamishie shirika fulani, nihamishie shirika fulani kwa sababu lina mishahara bora na yale mashirika bora hata kusikia yanatangaza kazi ni ngumu sana. Mara zote utaona tu kule kuna watumishi wanaingia wapya, wanaingia lakini hata kutangazwa huwa hayatangazwi. Mara moja moja utaliona moja au mawili. Yale yenye mishahara bora sitaki kuyataja nitakuwa siko sawasawa na nitakuwa sijawatendea haki, lakini wanayajua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule hata mtumishi akiwa amestaafu, mwezi haupiti vetting imemalizika na mtu mpya kashaingia na ameajiriwa. Ukienda yale mashirika ya mwenzangu na mimi ya Posta, mwaka mmoja, miwili hakuna mtumishi kaenda pale kwa sababu hakuna anayetamani kwenda. Wanakwambia vetting bado, vetting bado, vetting bado, lakini hawa watumishi wanaogombania kwenda kule wana sababu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mtumishi ni mhasibu kama mhasibu mwingine yuko halmashauri, yupo wizarani, yupo wapi akitoka tu akienda e-Government anatoka na mshahara wa milioni mbili mpaka milioni kumi na tano. Nani ataacha kugombania kwenda huko? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini inawa-demoralize wengine ambao wanaona; hii Serikali ni yetu wote na nchi hii ni yetu wote. Watumishi wote lazima waende kwenye utaratibu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JOHN J. NCHIMBI: …waende kwenye utaratibu wa Salary Board itakayokuwa ina-regulate mishahara ya watumishi wote ili kupunguza tofauti iliyokuwepo hapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuunga mkono hoja na ninaamini haya yatafanyiwa kazi katika bajeti inayokuja. (Makofi)