Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Mbeya Vijijini
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
1
Ministries
nil
MHE. PATALI S. PATALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuchukua nafasi hii kukushukuru wewe binafsi kwa kunipa nafasi hii ya kwanza katika kuchangia hotuba ya bajeti ya Wizara ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote ninaomba nichukue fursa hii kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzani, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutekeleza ahadi yake kwa vitendo, ahadi ya siku 100 kuhakikisha anaajiri watumishi 7,000 nchini kote. Nasi Mbeya Vijijini, kwenye ajira hizi 7,000 tumenufaika kwa kupata watumishi 115 wa kada mbalimbali zikiwemo afya, elimu pamoja na ugani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii pia kuupongeza uongozi mzima wa Wizara hii nyeti ya Utumishi wa Umma, ikiongozwa na Waziri, kaka yangu Ridhiwani Jakaya Kikwete, Manaibu Waziri, Makatibu Wakuu wote wanaohudumu kwenye hii wizara. Sambamba na hili, kwa kutambua kwamba hii ndiyo wizara inayosimamia utumishi wa umma nchini, leo hii tunapojadili na kupitisha bajeti hii maana yake inawagusa watumishi wa umma wote nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nichukue fursa hii kuwashukuru na kuwapongeza kwanza, watumishi wote wa Jimbo la Mbeya Vijijini; watumishi wanaohudumu kwenye afya, watumishi wanaohudumu kwenye kilimo, watumishi wanaohudumu kwenye elimu (walimu), watumishi ambao wanaohudumu kwenye ugani na sehemu zote, wote waliopo Jimbo la Mbeya Vijijini. Pia niwapongeze watumishi wote ambao ni watumishi wa umma Tanzania nzima; tunatambua kazi kubwa wanayoifanya ya kuhakikisha kwamba nchi inakuwa yetu yenye ustawi kamili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba niende haraka sasa kutoa mchango wangu kwenye baadhi ya maeneo. Kwa sababu ya muda niaomba uridhie kwamba, nitakuwa ninaongea kifupi na kutoa ushauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kufikia kiwango cha juu cha utekelezaji wa Dira ya Taifa ya 2050 tunahitaji sana mchango madhubuti wa utumishi wa umma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa ninataka kusema jambo moja hapa; ninaomba niwakumbushe Wabunge wote na viongozi wote ambao wapo katika Bunge hili, lakini pia na wale viongozi wa utumishi wa umma, wakiwemo Ma-CEO katika maana ya Wakurugenzi wote, na maafisa usimamizi wa taasisi mbalimbali, kwamba ni lazima tuweke jitihada za makusudi za kuulinda utumishi wa umma. Tusikubali hata kidogo utumishi wa umma ukabagazwa ama ukatwezwa kwa namna yoyote ile, kwa sababu, ukirejea kwenye Mpango wa Maendeleo 2026/2027 utekelezaji wake gharama tunahitaji takribani shilingi trilioni 86.3.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji na namna tutakavyogharamia huo mpango, 69% ni sekta binafsi, ambayo ni sawa na shilingi trilioni 60, na 30.4% sawa na shilingi trilioni 26 ni sekta ya umma; katika maana ya kwamba ni watumishi wa umma watakao-play part kuhakikisha kwamba mpango huu unatekelezeka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu; pamoja na hizi ajira ambazo zinaendelea kutolewa na Serikali yetu, ninaishauri Serikali kuongeza wigo wa ajira nchini. Hapa nishauri mambo machache. Ni lazima tukubaliane nchi yetu inapambana sana kuhakikisha kwamba inaziba lile gap la ajira nchini; lakini bado tuna vijana wengi wasiokuwa na ajira nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, kwa kuwa kuna utaratibu unaoendelea wa kuandaa andiko la mpango wa zile ajira za part time; niiombe wizara hii iharakishe iulete haraka ili tupitishe ili hizi ajira za muda ziweze kutambulika na ziingie sokoni ili kupunguza gap la watumishi la vijana wetu ambao hawapo kwenye utumishi wa umma, wapo mtaani tu bila ajira. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nichangie kwa hawa watumishi wanaojitolea. Mimi nimekuwa mtumishi, watumishi wa umma hawatoshi nchini. Mara nyingi tumekuwa tukitatua majukumu mbalimbali kupitia watumishi wanaojitolea. Hapa nishauri jambo dogo, ninaomba, ninafahamu hofu iliyo na dhamira njema ya Wizara hii na viongozi hawa juu ya watumishi wanaojitolea. Watumishi hawa wanaojitolea wakati ajira zinatoka wapewe kipaumbele.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mfano wa watumishi ambao wanahudumu mwaka mmoja, hadi miaka miwili, akitoa huduma ya kujitolea kwa uzalendo ajira zinapotoka hapati zile ajira, lakini ametumikia miaka miwili. Hili jambo si sawa, liangaliwe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri sehemu nyingine, eneo la vetting (upekuzi). Kwa mujibu wa kanuni za utumishi wa umma hasa kwenye nafasi za madaraka, ili mtumishi a-qualify pamoja na qualification zingine, kuhudumu nafasi ya madaraka kwenye utumishi wa umma ni lazima apitie process za upekuzi (vetting).
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hapa kupitia wizara hii ninaomba nishauri machache. Kwanza, ninaomba sana, ikiwezekana, kwa sababu zile veting, hivi sasa hivi kwenye taasisi nyingi sana, hasa mashirika binafsi, ukienda unakuta watumishi wengi wa umma wenye nafasi za uongozi hawana hizo nafasi katika utimilifu wao bali wanakaimu. Hii inatokana na sababu kwamba mchakato wa kufanya upekuzi kwenye nchi yetu unachukua muda mrefu. Unachukua kuanzia miezi sita, miezi nane na wakati mwingine hata mwaka mzima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ningependa kushauri jambo moja, kuona uwezekano wa upekuzi kufanyika katika local level, katika maana ya mikoani na wilaya. Ninafahamu, kwamba Ofisi ya Katibu Mkuu Utumishi kupitia Ofisi ya GSO (Government Security Office) inashirikiana na RSO inashirikiana na ma-GSO kufanya upekuzi. Wawaache hawa ma-RSO, ma-GSO wafanye upekuzi ili wawaletee taarifa kuharakisha huu utaratibu wa upekuzi kwa watumishi wa umma. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni uhamisho na hapa ninaomba nisisitize jambo moja…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Muda wako umekwisha Mheshimiwa.
MHE. PATALI S. PATALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nimalizie. Baadaye nitaleta taarifa; moja ya jambo ambalo ni janga la Taifa ni hili suala la uhamisho. Ndoa nyingi zinavunjika kwa sababu ya watumishi wa umma kukataliwa uhamisho. Sisi kama Bunge, tuielekeze Wizara ya Utumishi. Kwa mujibu wa kanuni mtumishi anapokuwa amekaa ile miaka stahili miaka mitatu kwenye kituo chake aruhusiwe kuhama…
MWENYEKITI: Mheshimiwa, muda wako umeisha.
MHE. PATALI S. PATALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, ninaomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana kwa kunisikiliza. (Makofi)