Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Chato Kaskazini
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
1
Ministries
nil
MHE. CORNEL L. MAGEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kukushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii njema jioni ya leo ili niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu katika kujadili bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu, kama ilivyowasilishwa katika Bunge lako Tukufu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, niungane na Watanzania wote kuendelea kumshukuru sana Mwenyezi Mungu, kwa namna ambavyo ameendelea kutujalia afya Watanzania wote wakiwemo viongozi wetu na kiongozi wetu mkuu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizo, niendelee kumwombea sana Mheshimiwa Rais aendelee kuongoza Taifa letu kwa busara hiyo aliyonayo, lakini akisaidiwa na Makamu wake wa Rais, akisaidiwa na Waziri wake Mkuu, lakini pia na Mawaziri wote pamoja na watendaji wote wa Serikali; kuanzia ngazi ya Taifa mpaka kwenye vijiji vyetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii pia, kuendelea kuwashukuru sana wananchi wa Chato Kaskazini. Wananchi hawa wa Chato Kaskazini ni watu wema sana, walinipigia kura kwa mahaba makubwa kwamba nije niwe mwakilishi wao katika Bunge lako Tukufu hili la Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wamekuwa na mimi siku zote, toka uchaguzi umekwisha, tumekuja Bungeni tumeapishwa, wamekuwa na mimi katika changamoto zote ambazo Mbunge wao nimekuwa nikizipitia na mazuri yote na mema yote tumekuwa bega kwa bega nao. Ninawashukuru sana wananchi wa Chato Kaskazini kwa kuendelea kuniunga mkono na ahadi yangu kwao ni kwamba sitawaangusha katika uwakilishi wangu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tupo kwenye kuchangia hotuba ya Waziri. Katika hotuba ile ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, yapo mambo mengi na mazuri ambayo Serikali imeyaweka mbele yetu kuonesha ina mpango mzuri wa kwenda kutekeleza kwa ajili ya Watanzania. Pamoja na mipango ambayo imewekwa yapo mambo mazuri na makubwa ambayo yametengwa kwenye maeneo yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi wananchi wa Chato Kaskazini, ninatumia nafasi hii kumshukuru sana Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Serikali yake, lakini ikiwemo chama change, Chama cha Mapinduzi kwa makubwa na mazuri na mengi yaliyoletwa kwa wananchi wa Chato katika kipindi cha miaka minne ya utangulizi wa utawala wake. Tunamshukuru sana sisi watu wa Chato. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wilaya yetu ya Chato, ipo miradi mingi ya kimkakati ambayo ililetwa, ambayo nikianza kuitaja hapa nadhani, muda hautatosha lakini itoshe kusema tu kwamba mabilioni ya fedha kwa ajili ya miradi, kwa ajili ya Watanzania waliopo Chato, kwa kweli sisi tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na fedha zile ambazo zimeletwa kwa wingi, nilitamani niseme mambo haya. Zipo fedha ambazo zimeletwa kwenye miradi mingi kwenye maeneo yetu, lakini inapokwenda kukamilika miradi ile haisimamiwi sawasawa kwa ajili ya kuleta tija ambayo ilikusudiwa na Serikali yetu. Kwa mfano, leo tukitembea kwenye miji mingi ikiwemo Mji wa Dodoma, Dar es Salaam, Mwanza na miji mingine, wako Wabunge wenzetu hapa wanaomba kujengewa stendi katika maeneo yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Chato ni moja ya mji ambao tulipata bahati ya kupata mradi mkubwa wa kujengewa stendi ya kisasa, kama zilivyo stendi nyingine kama Dodoma na kwingineko. Serikali ikifanya intervention ya kwenda kuona yale ambayo yanaendelea kwenye stendi zile utagundua kwamba fedha nyingi zimekwenda kule lakini tija iliyokusudiwa haiendi sawasawa kama ambavyo ilitarajiwa na Serikali yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ile stendi ukienda kuna maeneo mengine ambayo hayafanyi kazi kama ambavyo ilitarajiwa kwenda kutumika. Vilevile hata ukienda kwenye stendi yetu ya Chato ambayo imetengewa mabilioni ya fedha mpaka leo, haijakamilika katika ubora ambao unatakiwa na haifanyi kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, fedha zile zilizokwenda pale zinaishia huko bila kuleta matokeo yaliyokusudiwa. Kumbe, pengine tusingejenga ule mradi mkubwa unaoonekana sasa upo, ilhali umetumia fedha nyingi, lakini haufanyi kazi ipasavyo; badala yake, tungelielekeza fedha hizo katika kujenga vyoo kwenye shule zetu ili watoto wetu wapate kusoma katika mazingira bora zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kwenye hii miradi: nimemwona Mheshimiwa Waziri Mkuu amepita huko kwenye mikoa yetu, anapofika kwenye mikoa yetu na maeneo yetu, nimwombe sana aende akashughulike na miradi mikubwa ya kimkakati aone kama tija yake iliyokusudiwa inakwenda kufanya kazi, hilo ndilo lililokuwa ombi langu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na miradi hiyo kwetu pale Chato kuna uwanja mkubwa wa ndege, ulitumia mabilioni ya fedha na uwanja ule ukaanza kutumika na wananchi wa kule Chato na maeneo mengine ya jirani mpaka na nchi za jirani, uwanja ule ulikuwa unatumika kwa ajili ya kusafirisha watu, lakini mpaka leo ninavyozungumza, mabilioni ya fedha yamepotea katika uwanja ule. Sasa umebaki kwenda kwa Wasukuma kwenda kuanika pale mihogo ili wapate udaga waende wakale chakula badala ya kuweka ndege pale. Sasa shida iko wapi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamwomba sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, ninamwomba sana Waziri anayeshughulika na mambo ya usafirishaji na uchukuzi, wahakikishe kwamba Chato bado tunahitaji tupate ndege kwa sababu fedha ya Serikali ilikufa pale kwa kujenga kiwanja cha ndege katika eneo letu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika miaka minne ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ziko bandari mbili ambazo zilijengwa kwa fedha kubwa zaidi ya shilingi 6,000,000,000, iko Bandari ya Nyamirembe, iko na bandari ya Bwina. Bandari hizo zilitarajiwa kwamba baada ya kukamilika, meli zingeanza kutia nanga katika maeneo hayo, wananchi wapate huduma ya usafiri na pia kuwezesha upatikanaji wa mizigo kutoka maeneo mbalimbali kwa ajili ya biashara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tunavyozungumza miaka minne iliyopita ya bandari zile kuchukuliwa shilingi bilioni sita mpaka sasa hazitumiki na meli zipo kutoka Mwanza kwenda huko kwetu, lakini haziwezi kufika pale zinakwenda kwenye maeneo mengine. Kwa hiyo, ninamwomba sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba mahali ambapo Serikali imeamua kuwekeza fedha zake, basi fedha zile zikatutumike kama ambavyo zimekusudiwa kutumika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ninaomba niishauri Serikali hasa wakati inapokuwa inatoa miradi kwa wakandarasi, ninaona wakandarasi ambao ni private wanaweza wakafanya vizuri kuliko wakandarasi ambao ni taasisi za Serikali. Nina mfano pale kwangu pale Chato, kuna mkandarasi ambaye alikuwa National Housing alikuwa amepewa kujenga shule... (Makofi)
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Mheshimiwa muda wako umekwisha.
MHE. CORNEL L. MAGEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nimalizie tu hili, kwamba wako wakandarasi ambao wamepewa kujenga shule zetu, iko Shule ya Mbuye ya watoto wenye mahitaji maalum. Shule imejengwa kwa fedha nyingi lakini mpaka sasa haijakamilika na mkandarasi ameacha mradi amekwenda na ile shule inahitajika watu wasome pale na fedha zilipelekwa nyingi.
MWENYEKITI: Ahsante.
MHE. CORNEL L. MAGEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa sababu ya muda, ninaomba niseme ninaunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)