Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. Nyamizi Simon Mhoja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. NYAMIZI S. MHOJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ya kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu. Awali ya yote ninapenda nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kutufikisha kuwa wazima mpaka dakika hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia shukrani za pekee zimwendee Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutujumuisha katika kila sekta watu wenye ulemavu Nchini Tanzania. Pia shukrani zingine zimwendee Waziri Mkuu ambaye kwa sisi wenye ulemavu kuwa chini yake na kuendelea kuratibu mambo yetu ya wenye ulemavu. Kwa kuthibitisha hili hata kwenye hotuba yake amezungumza kuwa yeye ni mdau mkubwa wa watu wenye ulemavu, tunashukuru sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kwa moja kwa kuokoa muda mchango wangu utajikita katika ukurasa wa 71 na 72 ambao ni uratibu wa masuala ya watu wenye ulemavu. Hotuba ya Waziri Mkuu ilieleza kwamba Serikali imewezesha bohari ya dawa kuzalisha na kusambaza vifaa saidizi na mafuta kinga kwa watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vifaa saidizi kwa watu wenye ulemavu ninaweza nikatolea mfano, ni sawasawa na samaki na maji huwezi kuvitenganisha. Ukimweka samaki nchi kavu atatapatapa mwisho wa siku mambo yataharibika, hivyo hivyo hata sisi watu wenye ulemavu. Nimefika hapa kwa sababu tu nina vifaa saidizi vimeniwezesha kuingia humu na kutekeleza majukumu yangu ya kiubunge kama Wabunge wenzangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba Serikali kuwa vifaa hivi vimekuwa ni gharama na wote tunafahamu watu wenye ulemavu hali zetu wanazifahamu, ni duni. Nitolee mfano, mguu bandia kwa aliyekatikia juu ya goti miwili nitolee mfano moja kwa moja kwenye hospitali yetu ya Muhimbili pale Moi, wanauza unapata invoice ya milioni saba miguu miwili. Sasa niambie mtu mwenye ulemavu wa kawaida hiyo gharama anaipata wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, vifaa saidizi tukimaanisha hata magongo na crutches kama hizi ninazotembelea mimi nazo ni gharama kwa mtu mwenye ulemavu. Ninamzungumzia mwenye ulemavu wa hali ya kawaida kule kijijini, kwenye kata na kwenye Wilaya kule ambapo anapatikana, hizi gharama anazipata wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashauri Waziri Mkuu, Serikali imewezesha KCMC kuzalisha mafuta kinga kwa watu wenye Ualbino, wako wadau mbalimbali ambao wanazalisha vifaa saidizi maana vimekuwa adimu ndiyo maana hata gharama zinakuwa kubwa, wawezeshe hizi hospitali kila Mkoa pawepo basi hata hospitali ambayo inatoa vifaa saidizi na ili kurahisisha maisha kwa watu wenye ulemavu, vinginevyo hali zetu zinakuwa ni mbaya sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo ninazungumzia suala la mikopo ya 10%, kwa wenye ulemavu tunapata asilimia mbili. Imezungumzwa sana na wenzangu wazungumzaji waliotangulia. Sisi watu wenye ulemavu nchini Tanzania; kuna aina 13 za watu wenye ulemavu. Kuna aina moja ya ulemavu ambayo ni ya ulemavu wa akili, hawana sifa ya kupata huu mkopo, lakini ikumbukwe kwamba kuwa na ulemavu maisha yanaendelea kama kawaida. Atahitaji kula, atafanya biashara; na tukumbuke kwamba kuna dawa ambazo wanatumia, akitumia anakuwa sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Serikali imewatoa kabisa kwamba hawa watu hawapati hii mikopo. Ikumbukwe kwamba sisi wenye ulemavu hatuishi peke yetu, tunaishi na ndugu zetu, either ni mama, ni baba, ni mume, mke, tunaishi nao. Serikali inaweza ikaja na mpango mwingine wa kuwafikiria hawa walemavu wa akili ili nao waingie kwenye kuwapatia mikopo hii ya asilimia mbili ili nao waweze kufaidika na keki hii ya Taifa, ambayo wenye ulemavu wengine wanaipata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikishindikana hilo, ushauri mwingine basi wafikiriwe wapewe ruzuku, ilimradi tu kurahisisha maisha yao, waendelee kuishi kama watu wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hotuba pia ya Mheshimiwa Waziri amezungumza kabisa kwamba Serikali imewezesha kituo atamizi kilichopo Singida pale Sabasaba. Chuo hiki ni miongoni mwa vyuo vingi ambavyo Serikali imeviboresha. Ninamwomba Mheshimiwa Waziri Mkuu, kama ataona inafaa aweze kuvitembelea vyuo hivi, vina changamoto, ikiwemo wakalimani wa lugha ya alama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mzuri Chuo cha Luanzali Mkoani Tabora, hakina mkalimani. Hata juzi likizo nimetoka huko nimeona bado mkalimani hayupo. Hawa wanafunzi wanasomaje bila mkalimani? Ninaomba hili lichukuliwe kwa uzito ili kusaidia; na tutashukuru kama watatembelea na kutatua changamoto nyingi ambazo zinahusiana na hivyo vyuo vyuo vya watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kwa moja nizungumzie watumishi wenye wa umma ulemavu. Kuna mwongozo upo, mwongozo wa watu wenye ulemavu mahali pa kazi. Mwongozo huu hautambuliki kwa waajiriwa. Ninaomba Serikali, Ofisi ya Utumishi na Utawala Bora waweze kuwatambulisha waajiri wote huu mwongozo ili wafanyakazi wenye ulemavu waweze kupata haki zao kutokana na mwongozo, ambao Serikali ilikaa na kufikiria na kuona kutengeneza huu mwongozo na si kuuweka tu kapuni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hiyo, kupitia Ofisi ya Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, tunaomba waajiri wasiwanyime wafanyakazi wenye ulemavu fursa za safari za kazi kwa sababu ya mitazamo chanya ambayo wanayo kichwani mwao. Sisi watu wenye ulemavu tunafanya kazi na sisi tunatamani tupate hiyo fursa ya kusafiri ili tuweze kupata hicho kipato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, kuna waraka wa per diem kwa mwanamke ambaye ananyonyesha, akisafiri kikazi analipwa nusu per diem kwa ajili ya kumsaidia mtoto anayesafiri naye kazini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, sisi watu wenye ulemavu, mimi mwenyewe siwezi kutembea peke yangu, ninahitaji msaidizi. Wafanyakazi wengi wa watu wenye ulemavu wanapokwenda safari za kikazi wanapewa fedha iliyo sawa na mtu mwingine. Kwa hiyo, yeye atamchukua mtu wa nyumbani amsaidie kwenda naye. Atamkatia ile ile per diem ambayo ndiyo anayopata; of which inakuwa sasa hela anayoipata ni kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba ofisi ifikirie kutengeneza basi na waraka mwingine kwa watu wenye ulemavu, watambulike kuwa na msaidizi mahali pa kazi na hasa wakisafiri kwenye kuelekea kwenye safari za kikazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, Ofisi ya Waziri Mkuu inaandaa maazimisho ya siku ya Kimataifa na pia sisi watu wenye ulemavu tuna siku yetu maarufu kama D Day (Disability Day) ambayo ni tarehe 3 mwezi Desemba. Siku hii imekuwa ikidorora siku hadi siku. Mfano mzuri, mwaka jana tulifanyia Morogoro, ikawa kama ni kikao tu cha walemavu kutoka kata fulani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Ofisi ya Waziri Mkuu waendelee kuratibu hii Siku ya Watu Wenye Ulemavu Duniani kama siku nyingine za kimataifa za UKIMWI na maadhimisho mengine. Waichukulie kwa uzito na sisi tutafurahi; maana siku hiyo ndiyo siku ambayo wadau wanaweza kutoa mambo yao na pia tunaweza tukawajua wadau wanaojishughulisha na mambo yetu. Sisi wenyewe pia tutajulishana mambo mengi ambayo yanatuhusu sisi watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kusema hayo ninaunga mkono hoja, ninashukuru kwa kunipa fursa. Ahsante. (Makofi)