Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Mpanda Mjini
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
1
Ministries
nil
MHE. HAIDARY H. SUMRY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Awali ya yote, ninapenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya na uhai.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile niendelee kuwashukuru wananchi wa Jimbo la Mpanda Mjini kwa kuniamini na kunichagua kuwa Mbunge wao, niendelee tu kuahidi kwamba sitawaangusha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kumshukuru Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa na nzuri ambayo ameifanya kwenye Jimbo letu la Mpanda Mjini. Katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, Jimbo letu la Mpanda Mjini limepiga maendeleo makubwa sana. Ninaomba tumpongeze sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu na Mawaziri ambao anashirikiana nao katika Ofisi yake. Ni ukweli usiopingika kwamba Mheshimiwa Waziri Mkuu anafanya kazi nzuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 16, Machi, Mheshimiwa Waziri Mkuu alikuwa kwenye jimbo langu la Mpanda Mjini. Kwa namna ya pekee ninamshukuru sana sana sana kwa kazi kubwa aliyoifanya kwenye jimbo hili. Ametatua kero za wananchi wengi, lakini amesikiliza changamoto za wananchi wengi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, mimi kama Mbunge wa jimbo nilipata fursa ya kufikisha hoja zangu kwa maana ya changamoto za Jimbo la Mpanda Mjini, na Mheshimiwa Waziri Mkuu alizichukua na ninaamini katika bajeti ijayo zitafanyiwa kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya shukrani hizo, ninapenda kuwashukuru viongozi wangu wa Mkoa wa Katavi, kwa maana ya Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mheshimiwa Mwanamvua Hoza Mrindoko kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya kwenye Mkoa wetu wa Katavi. Pia, na dada yangu Jamila Yusuf Kimaro, Mkuu wa Wilaya ya Mpanda, naye kwa kazi nzuri anayoifanya kwenye wilaya yangu ya Mpanda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu imeeleza wazi mambo mengi ambayo yalitekelezwa katika kipindi kilichopita ambacho tunaenda kuishia mwezi Juni, lakini matazamio na matarajio ya bajeti ijayo. Sasa mimi nitajikita kwenye maendeleo kwa sababu Mkoa wa Katavi ni mkoa mpya na mambo mengi yalikuwa hayajafika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na eneo la nishati kwa maana ya umeme. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa na nzuri aliyoifanya kwenye mkoa wetu kwa kuhakikisha Mkoa wa Katavi, unaunganishwa na gridi ya Taifa. Kwa kweli watu wa Mpanda sasa hivi nao wamekuwa kama watu wa mikoa mingine, lakini kubwa zaidi imepunguza mzigo kwa TANESCO.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo langu na mkoa wetu wa Katavi tulikuwa tunatumia generators ambazo zilikuwa zinaendeshwa kwa gharama kubwa, lakini kwa namna Serikali ilivyofikisha gridi ya Taifa, tunaamini sasa gharama za TANESCO zimeondoka na tunaamini sasa TANESCO inaanza kupata faida kwenye eneo letu la Mkoa wa Katavi, na pia kwenye jimbo langu la Mpanda Mjini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hilo hilo la TANESCO, niendelee kuwaomba watu wa TANESCO, Mheshimiwa Waziri Mkuu atusaidie na watu wa Wizara ya Nishati watusaidie kupeleka kwenye maeneo ambayo yanahitajika ujazilizi wa umeme. Pale kwenye eneo langu la Mpanda Mjini kuna kata ambazo bado zina changamoto, ni kata ambazo ziko mjini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mji wa Mpanda unakua kwa kasi. Kwa mujibu wa Sensa, Mkoa wa Katavi unakua kwa karibia asilimia saba kila mwaka. Kwa hiyo, utaona ni namna gani Mkoa wa Katavi unavyokua kwa kasi na Mpanda Mjini ndiyo kitovu cha maendeleo ya mkoa wetu. Kwa hiyo, tunapoongelea kukua kwa asilimia saba, tafsiri yake ni kwamba asilimia saba hiyo itatafsirika kwenye jimbo langu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ningeomba sana kwenye Kata za Shanwe ambapo umeme umefika lakini kuna maeneo mapya ambayo yanajengwa bado umeme haujafika na ningeomba ufike. Vilevile, kwenye kata ya Kazima nako umeme umefika lakini bado kuna maeneo mapya ambayo yamejengwa na umeme bado haujafika. Kata ya Nsemulwa, Kata ya Misunkumilo, Kata ya Magamba, Kata ya Kakese, na kata ya Mwamkulu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo hayo bado tumefikishiwa umeme, lakini kwa kuwa kuna makazi mapya yanajengwa, kwa hiyo, kuna uhitaji mkubwa wa maeneo yale mapya. Kwa hiyo, ningeomba sana Wizara ya Nishati katika bajeti ijayo waangalie namna ya kutuongezea bajeti ili umeme uweze kufika kwa wananchi, nao wafurahi na watabasamu kama Mheshimiwa Rais alivyotuahidi tabasamu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hilo hilo ningeomba kuiomba Serikali itusaidie kujenga ile njia ya umeme ambayo sasa hivi kuna kazi inaendelea kufanyika pale Mkoa wa Ruvuma kwa maana ya Sumbawanga, lakini mradi huu unatakiwa uje Mkoa wa Katavi ufike pia mpaka Kigoma ili sasa tuondokane na changamoto kabisa kwa sababu tutakuwa na maeneo mawili ambayo tunategemea ya umeme hata ikipata changamoto, njia hii tutakuwa tunatumia njia nyingine ili kuendelea kupata umeme.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kutoka eneo hilo, niende sasa kwenye eneo la TARURA. Ninakiri wazi kwamba TARURA inafanya kazi nzuri, na kwenye jimbo langu imefanya kazi nzuri, madaraja mengi yamejengwa na tunafurahi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi na Mheshimiwa Lupembe tunapakana majimbo yetu, na juzi tu hapa tumepata mkandarasi anakwenda kujenga daraja la karibia shilingi bilioni tatu ambalo linapakana na Kata ya Itenka - jimbo la Mheshimiwa Lupembe na Kata ya Mwamkulu ambayo ni jimbo langu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa fedha hizi alizotuletea, lakini bado tuna changamoto kwenye eneo hilo la jimbo langu na Mheshimiwa Lupembe, kuna daraja lingine ambalo linaunganisha Kata ya Kakese kwenye jimbo langu na Kata ya Itenka kwenye jimbo lake Mheshimiwa Lupembe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, daraja hili lilijengwa, lakini bahati mbaya lilisombwa na maji. Kwa hiyo, tunaiomba Serikali irudishe huduma pale kwa sababu tunaamini daraja hili likijengwa litawasaidia sana wananchi wa majimbo yetu haya mawili kuweza kufanya biashara na kuongeza uchumi wao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo la TARURA niendelee kuiomba sana TAMISEMI watusaidie kwa kweli kutuangalia kibajeti. Sisi Mkoa wa Katavi kwa neema ya mvua, basi sisi tunaweza tukawa ni namba moja kwenye nchi hii. Tumepata neema ya mvua kubwa na mazao yamelimwa sana na tunaamini wananchi wetu watavuna mazao kwa wingi katika msimu huu, lakini mvua hizi zimebadilika kuwa changamoto kwenye miundombinu yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuwaombe ndugu zetu wa TARURA waweze kutuongezea fedha ili tuweze kwenda kukarabati hizi barabara ambazo zimeharibika katika kipindi hiki cha mvua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaendelea kuwashukuru, wanafanya kazi nzuri na kwa kweli Mungu awabariki sana na Mungu ambariki Mheshimiwa Waziri, Mungu aendelee kumbariki Mheshimiwa Rais, hata Mtendaji Mkuu wa TARURA anafanya kazi nzuri. Sisi Waheshimiwa Wabunge tukimpigia simu amekuwa ni msikivu, anatusikiliza na anatatua changamoto zetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hilo hilo la barabara, Mji wa Mpanda ndiyo kitovu cha Mkoa wa Katavi kama nilivyosema awali. Tunazo barabara za lami karibia kilometa 20 zimejengwa kwenye jimbo langu, lakini hazina taa za barabarani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninaomba sana ndugu zangu viongozi wangu wa Wizara hii ya TAMISEMI watusaidie angalau kila mwaka tupate bajeti kidogo ambayo itaendelea kuzipunguza hizi barabara, at least katika miaka mitano ijayo basi tuwe tumemaliza hizi barabara kuziweka taa za barabarani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika, tunapoweka taa za barabarani kwenye maeneo ya miji yetu, tunasaidia wananchi wetu, wafanyabiashara wadogo wadogo, wachoma mahindi, wachoma ndizi na wafanyabiashara wadogo wadogo wananufaika na haya maeneo hasa wakati wa jioni wanaweza kufanya biashara zao. Kwa hiyo, niendelee kuomba sana sana sana kwenye eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo la TARURA pia tuna fedha za mfuko wa jimbo...
MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa, muda wako umekwisha.
MHE. HAIDARY H. SUMRY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaunga mkono hoja, nashukuru sana.