Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Peramiho
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
0
Ministries
nil
MHE. DKT. LAZARO K. KOMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa nafasi. Nami kwa kuwa ni mara ya kwanza kusimama katika Bunge lako hili Tukufu, nitumie nafasi hii kwanza kumshukuru sana Mwenyezi Mungu ambaye amenifikisha katika Bunge hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninatumia nafasi hii pia kumshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wetu wa Chama cha Mapinduzi kwa kuniteua kugombea nafasi ya Ubunge kupitia Chama cha Mapinduzi na hatimaye wananchi wa Jimbo la Peramiho kunichagua na kuwa mwakilishi wao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii pia kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Emmanuel John Nchimbi, Makamu wa Rais, kwa kazi kubwa anayoifanya ya kumsaidia Mheshimiwa Rais katika kuwaletea wananchi wa Tanzania maendeleo, wakiwemo wananchi wa Jimbo la Peramiho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie pia fursa hii kumpongeza Waziri Mkuu, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba kwa kazi kubwa anayoifanya, kazi ya kuwatembelea Watanzania kule kwenye mikoa, kuwasilikiliza na kutatua changamoto zao pale inapobidi afanye hivyo. Kazi hii kwa hakika siyo nyepesi, ni kazi ngumu na inayohitaji kujitoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kufanya hivi, Mheshimiwa Waziri Mkuu anaendelea kuimarisha imani ya Watanzania dhidi ya Serikali yao, Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais mbeba maono, Rais mpenda maendeleo, Rais mpenda haki, na zaidi Rais mpenda Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kumpongeza pia Mkuu wetu wa Mkoa, Mheshimiwa Kanali Ahmed Abbas Ahmed kwa kazi nzuri anayoifanya akiwa anashirikiana na viongozi wenzake, wasaidizi wake, akiwemo Mkuu wa Wilaya ya Songea Mheshimiwa Wilman Kapenjama Ndile, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Songea Vijijini dada yangu Elizabeth Gumbo, pia na Mwenyekiti wake wa Halmashauri, Mheshimiwa Ponera.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nijielekeze katika kuchangia Hotoba ya Waziri Mkuu ya Bajeti, na kama muda utaniruhusu nitakwenda katika maeneo matano. Eneo la kwanza nitazungumza kuhusu barabara, eneo la pili nitazungumza kuhusu afya, na eneo la tatu nitazungumza kuhusu elimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na hili la barabara. Sisi wananchi wa Jimbo la Peramiho, sehemu kubwa ya maisha yetu yanategemea kilimo. Niseme tu, ili kilimo kiweze kuimarika ni lazima tuwe na barabara ambazo zinapitika wakati wote wa mwaka. Ikifika nyakati za Novemba, Disemba na Januari sisi tunatumia barabara kwa ajili ya kupeleka pembejeo, zikiwemo mbolea, katika mashamba yetu. Ukifika wakati wa mavuno pia tunatumia barabara kwa ajili ya kurudisha mazao kutoka mashambani kupeleka sokoni na baadaye kupeleka katika maeneo mengine ya kuhifadhia mazao hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ya barabara katika Jimbo la Peramiho kwa hakika siyo njema sana. Ubovu wa barabara umezungumzwa na Wabunge takribani zaidi ya 90%. Takribani kila Mbunge aliyesimama amezungumza, na jambo hili pia liko katika Jimbo letu la Peramiho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, iko barabara ya kutoka Njiapanda ya Likuyufusi – Mpitimbi – Mkenda ambako ni mpaka kati ya Taifa letu hili la Tanzania na majirani zetu wale wa Msumbiji. barabara hii ina kilometa 120. Barabara hii imezungumzwa kujengwa kwa kiwango cha lami kwa miaka mingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Pamoja na kuzungumzwa kwa miaka mingi, utekelezaji wake kwa hakika umekuwa wa kusuasua kwa muda mrefu. Hii barabara ina mchango mkubwa katika kuleta maendeleo ya Taifa hili na pia maendeleo ya wananchi wa Mkoa wa Ruvuma na maendeleo ya wananchi wa Jimbo la Peramiho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa barabara hii ina mchango wa kusafirisha bidhaa zinazoshuka katika Bandari ya Mtwara na kuelekea kaskazini ya Msumbiji. Gari zinapita katika barabara hii ya Likuyufusi – Mpitimbi – Mkenda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana, barabara hii tarehe 10 Juni, 2025 mkandarasi alipata nafasi ya kusaini mkataba ili kuweza kuanza ujenzi wa barabara hii, lakini hivi ninavyozungumza, ni takribani mwaka mmoja, mkandarasi hayuko site kwa sababu hajapata fedha za kuanza ujenzi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba sana Serikali itusaidie sisi wananchi wa Jimbo la Peramiho, barabara ile ijengwe kwa kiwango cha lami ili nia ya Serikali ya kuhakikisha eneo lile linaendelea kuimarisha uchumi wake liweze kutimia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hizi ni nyingi, ningeweza kuzitaja zote, lakini niseme tu, iko barabara ya Njia Panda ya Ndongosi kwenda Ndongosi hadi Nambendo; Barabara ya kutoka Ndongosi kwenda Mpingi hadi Kikunja; Barabara ya kutoka Magagura kwenda Mipeta; Barabara ya Magagura kwenda Ngahokora; Barabara ya Kutoka Peramiho kupita Maposeni kwenda Kilagano ile ya kutoka Kilagano kwenda Mwepai. Barabara hizi ni nyingi na hali yake siyo nzuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba tu pia kuitaja barabara ile ya kutoka Songea kwenda Mpingi, barabara hii hazipitiki. Ninaomba sana, pamoja na ongezeko hili la bajeti ya TARURA ya shilingi trilioni 1.2, bado kwa mahitaji ninayoyasikia katika Bunge hili, hatutafanikiwa kuweza kuzijenga barabara hizi kwa kiwango kinachotakiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kupata matokeo ambayo hatujawahi kuyapata katika ujenzi wa barabara, tunapaswa kuja na mawazo ambayo hatukuwahi kuwa nayo huko nyuma kuhusu namna ya kupata fedha za ujenzi wa barabara zetu katika nchi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, itakuwa ni jambo jema na la busara sana Serikali ikatumia mbinu ile ile iliyotumika katika kuweka umeme vijijini kwa maana ya REA, njia ile ile iweze kutumika kupata fedha za kwenda kujenga miradi ya barabara ili mwisho wa siku barabara zetu ziweze kuimarika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tusipofanya hivi, katika kipindi hiki cha miaka mitano, ni imani yangu hata zile ambazo zinapitika leo, ikifika miaka mitano ijayo hazitakuwa na nafasi ya kupitika sawa sawa, na hivyo tutapeleka mzigo mkubwa kwa Serikali jambo ambalo tungeweza kupunguza mzigo huo kwa kutafuta fedha kwa wakati mmoja ili ziweze kuimarisha barabara katika eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende katika eneo la afya…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Mheshimiwa bahati mbaya muda wako umeisha…
MHE. DKT. LAZARO K. KOMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi na ninaunga mkono hoja. Ahsante sana… (Makofi)