Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. Dougras Didas Massaburi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kivule

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. DOUGRAS D. MASSABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nami nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema, kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza nachangia hotuba ya Mapato na Matumizi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, nichukue fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, jana tumetoka kwenye Mwenge Ilala na tumezindua miradi yenye thamani ya shilingi bilioni 54 na sehemu kidogo. Nasi watu wa Kivule pia tulipata shule za sekondari na nyingine za ghorofa ndani ya Jimbo letu la Kivule, ikiwemo Shule ya Sekondari ya Kitunda Relini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, Mheshimiwa Rais amefanya kazi kubwa ndani ya jimbo letu. Tunavyo vituo vya afya vya kutosha. Tunazo kata sita, na ndani ya kata sita tayari kata tano zote zina vituo vya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, nachukua fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kupitia Wizara ya Maji, pale kwenye Kata ya Kivule ndugu yetu Mheshimiwa Aweso alitutembelea na akatuahidi visima takribani 10 vya maji, na tayari tunacho kisima juzi vimeshaanza kutoa maji kwenye kata ile ya Kivule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizo, najikita kwenye changamoto za Jimbo la Kivule. Juzi dada yangu Mheshimiwa Bonnah alizungumza hapa masuala ya AFCON; na kimsingi Jimbo la Kivule ni Jimbo linaloendesha uchumi wa eneo lile. Lipo Katikati, yaani ukitoka Mbezi ukapita Segerea ni lazima upite Jimbo la Kivule ndipo utokee Chamazi ambako watu wa AFCON watakapokuwa wanafanya mazoezi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kushangaza, Jimbo hili la Kivule halina barabara ya lami hata moja. Wenzangu hapa wamekuwa wakililia kukarabatiwa barabara zao za lami, ni sawasawa na mtoto analilia kiatu kizuri wakati mimi familia yangu mtoto wangu hana hata mguu. Kwa hiyo, naomba sana nifikishie salamu za wananchi wa Jimbo la Kivule, wanalia na barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata juzi Mheshimiwa Kwagilwa alikuja pale akiwa Naibu Waziri wa TAMISEMI na mkandarasi wa Barabara ya kutoka Banana – Kitunda – Msongola, barabara hiyo hiyo kuelekea Nyantira na Mwangati, inapita njia nne kutoka Majohe mpaka Pugu Sekondari. Ziliahidiwa kufika tarehe 30 Aprili, 2026 zitakabidhiwa kwa wananchi, lakini cha kustaajabisha, kama anavyoongea kaka yangu Baba Levo, bado ni matope yasiyokuwa na mwisho. Sasa hivi zimebaki siku 16 peke yake kutimiza siku hiyo ya tarehe 30 Aprili, 2026, lakini sioni jitihada yoyote inayofanyika ili kuhakikisha barabara hizo zinapitika kiangazi na masika, na vilevile madaraja pamoja na vivuko kwenye maeneo ya Mto Mzinga

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema, 70% ya mayai yanayokwenda Dar es Salaam yanatoka ndani ya Jimbo la Kivule. Vilevile tunalima mbogamboga kama mchicha, na spinach, maana pale tunapitiwa na Bonde la Mto Mzinga. Akina mama wanafanya shughuli zao za kiuchumi ili kuweza kulisha Mkoa wa Dar es Salaam na Serikali kupata kodi kwenye malisho hayo. Sasa inafika mahali, wanazalisha lakini hawapati nafasi ya kusafiri umbali mrefu kupeleka mazao yao huko mjini kwa ajili ya ubovu wa barabara na kupanda kwa gharama za usafirishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimeona niwasilishe changamoto hizo kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wamewasilisha. Nami nina kilio kikubwa sana cha Jimbo letu jipya la Kivule. Kwa hakika mtufikirie, tuone namna gani tunakwenda kulikomboa jimbo lile kwa miundombinu ya barabara ili wananchi wetu waendelee kufanya shughuli zao za ufugaji na kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakubaliana na Mpango, Dira 2050 na Mapato na Matumizi ya Mwaka 2026/2027. Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ndiye Rais pekee ambaye baada ya sisi Bunge kutunga Sera mwaka 2009, mwaka 2010 tukatunga Sheria ya PPP, halafu mwaka 2014 tuka-review Sheria ya PPP tukaelekeza tuanzishe kituo cha PPP.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa, tangu 2014 hadi 2024 kituo hicho cha PPP hakikuwahi kuanzishwa isipokuwa alipokuja Mheshimiwa Rais Dkt. Samia, akakianzisha, na akamkabidhi kaka yetu Mheshimiwa Kafulila kama sehemu ya kuwa Mkurugenzi wa Kituo kile. Ninampongeza Mheshimiwa Kafulila, na hivi juzi kwenye gazeti la AgMP Tanzania tumetambuliwa kuwa nafasi ya tisa duniani kama watu ambao tunao professionals wa kutosha kwenye kitengo hicho cha PPP.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mpango wetu huu ukiuangalia unaelekeza kuwa 70% utokana na vyanzo mbadala kwa maana ya PPP, shares, na bond. Hizo ndizo alternative financing. Hata hivyo, katika sheria yetu hakuna mahali ambapo inazungumzia bonds na shares zinakuwa managed vipi? Isipokuwa PPP peke yake ambayo ina dedicated center na ina policy pale, ambayo sisi tuliitunga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado PPP yenyewe hii tunayoisema hapa hatuipi meno ya kutosha. Tunazungumza kuwa miradi mingi itokane na vyanzo mbadala (alternative financing). Lengo letu ni kwamba, kiasi kinachobaki Serikali ikiwekezee nguvu kwenye primary objective ya kusaidia wananchi katika kupata afya bora, elimu bora, na barabara bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia bajeti ile ya PPP tumeona imepitishwa shilingi bilioni moja kila mwaka. PPP maana yake ni maandalizi ya mradi. Sasa kama tunafikiria kuanzisha mradi wenye thamani ya shilingi trilioni kumi, kwa mfano mradi ule Mbambabay kwenda Mtwara wenye thamani siyo chini ya shilingi trilioni 10, au 15, lakini feasibility study yake inahitajika siyo chini ya dola 2,500,000. Eti Serikali inasubiri SADC watoe fedha hiyo kwa ajili ya kufanya feasibility study kwenye mradi ambao unaweza kuwa na tija kwa Serikali yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo haja ya kushikamana ili tuweze kukipa nguvu kitengo cha PPP ili miradi hiyo iende kwenye hizo alternative financing na fedha nyingi ibaki kuweza kuwahudumia Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona wenzetu wa Kenya pale nchi jirani, samahani, wao wanatumia siyo chini ya dola milioni 60 kwenye uandaaji wa miradi, lakini sisi tunatumia bilioni moja kwenye uandaaji wa miradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona hapa Wizara ya TAMISEMI wameorodhesha miradi zaidi ya 400 kwa ajili ya alternative financing. Sasa tujiulize, je, wanazo feasibility study? Je, miradi hiyo are they bankable projects? Ni kwamba tunayo list, tunayo majina ya miradi, lakini hatuna list ya miradi. Kwa hiyo ipo haja ya kuona namna gani bora tunaweza tukawashikilia ndugu zetu wa PPP, tukawapa nguvu, na tuka-coordinate hizi alternative financing kama ndugu zetu wa Rwanda wanavyofanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Rwanda wana kitu kinaitwa Rwanda Board of Directors. Kwamba mtu akienda pale, ana jambo la PPP, au shares, ama bonds, kila kitu kinamalizikia pale. Ningeshauri, hiyo iwe chini ya Ofisi ya Rais ama Waziri Mkuu ili kuweza kupunguza miluzi mingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakubaliana kwamba uchumi wa nchi yetu upo kwenye mashirika, na ndiyo maana Mheshimiwa Rais aliweka zaidi ya shilingi trilioni 92.5 kwa ajili ya kunyanyua mitaji ya mashirika. Hata hivyo, bado kuna changamoto katika kufanya maamuzi. Yaani kuna multi approvals centers nyingi. Unakuta mtu anakuja, anataka kufanya uwekezaji, ni lazima aende kwa TR halafu arudi kwa PPP. TR yuko Wizara ya Mipango, PPP tuko Wizara ya Fedha, Waheshimiwa Mawaziri tofauti, hakuna coordination of the Government.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuone kuwa kuna haja ya kuichukua PPP yenyewe iunganishwe na watu wa TR ili kusudi waweze kuleta ufanisi wa mashirika, kwa sababu lengo la TR na PPP ni kuleta ufanisi kwenye mashirika ya umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliona nishauri hilo ili kuweza kuona namna bora ya kuweza kuyashirikisha mambo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, tunalenga kujenga uchumi. Serikali yetu hii inazo assets nyingi. Ipo haja ya kufanya tathmini ya assets za Serikali. Zile ambazo hazizalishi na tunaona zitahitaji capital ambayo inaweza ikatoka ama foreign ama kwenye private sector, tuingize ili kuweza kuongeza ajira, kuchangia uchumi na kufanya mnyororo mpana wa kibiashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utakubaliana nami kwamba, yapo mashirika mengine lakini hayazalishi. Ipo sababu sasa ya ofisi za Serikali kufanya evaluation ya maeneo hayo...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Massaburi, muda wako umeisha, ninaomba uunge mkono hoja. Unaweza ukachangia kwa maandishi, haina tatizo.

MHE. DOUGRAS D. MASSABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaunga mkono hoja. (Makofi)