Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. Sigrada Wilhem Mligo

Sex

Female

Party

CHAUMMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. SIGRADA W. MLIGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Ukiniuliza swali la haraka haraka nimegundua nini kwenye hotuba ya Waziri Mkuu? Nimegundua ni hotuba ambayo kama hujaijua, Serikali ya Chama cha Mapinduzi unaweza ukasahau tabu zote. Ni hotuba moja, kwa kuizungumza ni hotuba nzuri sana, unaweza ukasahau tabu zote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naweza nikasema neno moja kabla sijaenda kwenye hoja yangu. Kama hotuba hiyo itaenda kutekelezwa, ukiilinganisha na hotuba ya Mheshimiwa Rais aliyohutubia Bunge kwa mara ya kwanza, sijui huwa kinatokea nini hapa katikati, sijui ndio machawa wanaharibu mchongo! Kwa sababu speech ni nzuri, lakini njoo kwenye utekelezaji, tunapoteana, matatizo ndio yanaanzia hapo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitasema kwa nini speech ni nzuri na utekelezaji wake ni mgumu kwa hoja zangu zifuatazo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja ya kwanza, tumesema dira yetu inasema uchumi na ajira lengo ni kukuza uchumi na ajira. Leo hii utakuzaje uchumi na ajira ya nchi hii wakati changamoto yoyote ikitokea mtu wa kwanza kumtazama wa kufidia ile changamoto ni mwananchi wa kawaida?

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii ukianzisha hata biashara ya maandazi, umefungua kioski hapo kesho, utakutana na Osha, utakutana na watu wa afya, utakutana na TRA, utakutana sijui na mtu anaitwa Mipango Miji, utakutana na mtu wa Leseni ya Halmashauri, kodi zaidi ya sita. Huyu kijana ambaye mmempa shilingi milioni mbili unamtoaje hapo? Swali dogo tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, tuna wawekezaji ambao wanakuja kuwekeza kwenye nchi hii. Wale tunawapa grace period, yaani eti tunawapa miaka 10 ya kuchechemea wajitafutetafute. Wakishachuma miaka 10 imeisha, wanaondoka anauza kampuni, ameenda na fedha zetu, tunapiga hesabu gani? Tunapiga hesabu gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, issue za kodi ambazo kimsingi nimeshazungumzia kidogo hapo, nchi hii inakodi nyingi, na kama ina kodi nyingi, nilitarajia kwenye changamoto za ghafla zinazojitokeza kwenye nchi hii, kwa sababu Mungu ametujalia kila kitu kwenye nchi hii, kila kitu hata ukitaka mwanamke mzuri, mdada mzuri, mbaba mzuri, wapo; ametupa madini, ametupa mito, ametupa maziwa, ametupa madini kila kona; Njombe ndio kuna madini haijawahi kutokea; lakini leo wafadhili wametoka kufadhili UKIMWI, tumechukua ile kodi, mimi nimenunua gari. Ndiyo maana najua, mwananchi wa kawaida anayenunua gari ndio akafidie gharama za matibabu ya Virusi vya UKIMWI na kudhibiti UKIMWI, kisa USA wamejiondoa kwa 100%.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja yangu ni kwamba tunahitaji kuwasaidia hawa watu, je, kama Serikali, ndiyo limekuja ghafla, wafadhili wametoka, kwa nini tufikirie mtu wa kufidia ni mwananchi? Kwa nini tusifikirie kwamba zile akiba zetu, yale madini yetu ya Njombe tukayachimbe yafidie hiki kitu? Mmeingiza kodi, mmeingiza gharama za madawa ya UKIMWI kwenye kodi tena za wananchi, yaani huyo huyo anaumwa, huyo huyo mnajidai mnamsaidia, halafu mnamchukua hela yake yenyewe mkamnunulie dawa.! Tunafanya kitu gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni kilimo. Sisi Mkoa wa Njombe Mungu ametubariki tuna kila kitu. Sasa Mungu ametubariki zaidi; ninavyozungumza hivi, Waziri wa Kilimo anatokea Njombe, lakini Mwenyekiti wa Kamati ya Biashara na Viwanda ni Mheshimiwa Deo Mwanyika Mbunge wa Jimbo la Njombe Mjini, lakini ndiyo mkoa pekee unaoongoza kwa migogoro ya ardhi, unaoongoza kwa wawekezaji wa viwanda. Kunyanyasa wananchi wa Njombe, hawalipi, kuna huyo Mwekezaji wa Chai anaitwa DL, kila siku ni kelele.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais amekuja Njombe akamwagiza yule mwekezaji kuwalipa wale wafanyakazi, na akampa masharti nafuu ya kuchukua fedha CRDB benki, lakini mpaka leo hawajalipwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, niliangalia muda wangu, sihujumiwi leo. Niliangalia, nilianza na dakika 27, kwa hiyo, zimeisha dakika nne.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa jambo lingine…

MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Sigrada, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Taletale.

TAARIFA

MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumpa taarifa mwongeaji, Wenyeviti na Mawaziri wapo kwa niaba ya Bunge na Kamati, siyo kwa niaba ya mikoa yenu, ahsante.

MHE. SIGRADA W. MLIGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante…
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa subiri. Taarifa unaipokea?

MHE. SIGRADA W. MLIGO: Mheshimiwa Naibu Spika, siwezi kuipokea kwa sababu hakuna nilichokosea. Hatuwezi kukataa kwamba Waziri ni Serikali, lakini Mwenyekiti wa Bunge ana maamuzi kwenye jambo hilo. Kwa hiyo, siwezi kuipokea taarifa na muda wangu unilindie.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hoja nyingine ni ardhi. Tunalalamika hapa migogoro ya ardhi. Kwenye speech ya Mheshimiwa Waziri Mkuu amezungumzia migogoro ya ardhi. Mnatatuaje migogoro ya ardhi, hampangi miji, na mna Maafisa Mipango wa Miji, mna Maafisa Ardhi wa Miji, mnatatuaje changamoto ya ardhi ambayo Njombe mpaka leo Hakimu wa Mahakama ya Ardhi mkoa mzima yupo mmoja? Ukianza kesi yako leo, mpaka unajifungua mtoto miezi tisa, anazaa na vijukuu na vijukuu kesi yako Mahakamani haijaisha mnatatuaje? Hamtaki kupima ardhi, hati leo hii kutafuta ardhi kwenye nyumba yako ni bora kutafuta mwanamke wa kuoa kuliko kutafuta hati. Utatafuta hiyo hati miaka mitatu. Mchumba unamwahidi tu, keshokutwa nakuoa, unampata, kwenye nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nilindie muda wangu. Jambo lingine ni elimu. Hii Tanzania ni moja, tuna mifumo ya elimu miwili. Mtu mwenye hela kidogo, na siku hizi kwenye nchi hii ukiwa na hela unafuatiliwa kuliko maskini. Yaani badala ya kujadili maskini tunamsaidiaje ajinyanyue, tunajadili hivi hili gorofa huyu mtu amelitoa wapi? Yaani natamani Serikali iumize kichwa kujadili kwa nini Tanzania ina umaskini na si…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu.

KUHUSU UTARATIBU

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Naibu Spika, hili Bunge lina utaratibu wa kuzungumza. Sasa humu ndani utafikiri tunagombana. Tunaomba anayetoa hoja azungumze kiustaarabu, tutamwelewa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mbunge, endelea.

MHE. SIGRADA W. MLIGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nafikiri ni sauti ambayo Mwenyezi Mungu amenijalia. Mwombe Mwenyezi Mungu, amekujalia kitu kingine, pengine amekupa mwenzangu mwili, mimi amenipa sauti, lakini nina maana nzuri. Kila mtu Mungu amempa karama yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, tumezungumzia utawala bora. Nakumbuka Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano aliahidi issue ya Katiba mpya. Niwaombe Waheshimiwa Wabunge, tusimchocholeshe, naye anataka kuacha alama kwenye nchi hii, lakini sasa hivi mmembana mmembana, mnamsogelea sogelea ili ajisahaulishe, ili itakavyofika 2031 mje hapa mseme watu wote waliahidi Katiba hawakuleta, ila wewe umeleta; atakayekuja, tunawajua! Tunawajua!

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba, mimi binafsi na wananchi wa Mkoa wa Njombe, tunaomba msimamo wa Mheshimiwa Rais wa kufanya nchi hii iwe na utawala bora, na kwenye hili naomba asiyumbishwe. Hiyo ndio legacy pekee itakayomfanya Mheshimiwa Dkt. Samia akumbukwe na siyo kusikiliza watu. Eti mkileta Katiba mpya tutatoka madarakani! Aliyesema mtatoka, ni nani? Ni ninyi mtekeleze mlichoahidi, hakuna mtu atatoka kama mtatekeleza. Simple tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, issue nyingine…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Sigrada, muda wako umeisha naomba umalizie.

MHE. SIGRADA W. MLIGO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimalizie. Wengine walikuwa wanapewa grace period, nipendelee tu yatima mimi.

NAIBU SPIKA: Malizia Mheshimiwa, muda umekwisha.

MHE. SIGRADA W. MLIGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahadi zisizotekelezeka …

NAIBU SPIKA: Usianze jambo jipya Mheshimiwa, malizia tu.

MHE. SIGRADA W. MLIGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, ahsante, naheshimu kiti, ahsante sana nitaongea siku nyingine.