Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. Thomas Maganga Kampala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. THOMAS M. KAMPALA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru. Ninaomba nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa uzima na afya aliyonijalia na kupata nafasi ya kuja kuchangia kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii kumpongeza sana Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan. Leo wakati ninajiandaa kuchangia moja ya mchango wangu ilikuwa ni suala la mafuta. Nimpongeze Mheshimiwa Rais, ametoa ufafanuzi wa changamoto ya mafuta kwa kinagaubaga. Mheshimiwa Rais ametoa historia fupi ya changamoto ya mafuta na akatoa mwelekeo. Ninataka nichukue fursa hii kumpongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii kumpongeza sana Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania home boys ndugu yangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Madelu Nchemba kwa hotuba nzuri aliyoitoa, hotuba ambayo kwa kweli imegusa kwenye kila idara.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaipongeza sana Serikali kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya. Sisi kwenye Jimbo la Katavi mwaka wa fedha uliokwisha tumepata fedha nyingi sana. Eneo la afya tumepata milioni 928, ukienda upande wa elimu msingi tumepata milioni 674, ukienda upande wa elimu sekondari nako jumla ya fedha zote zilizokuja kwenye Jimbo la Katavi ni 2,688,000,098, fedha hizi ni nyingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninataka nichukue fursa hii; wakati mwingine tunaposimama hapa kumpongeza Rais wapo watu wengine wanadhani tunafanya mzaha mzaha. Tunampongeza Rais kwa kazi anazozifanya. Sisi kule Jimbo la Katavi, ukifika leo Katavi ukitoka hapa na basi usiku mtu akakushusha kwenye Jimbo la Katavi usiku akakufungua macho akakwambia uko Katavi utashangaa. Imefanyika kazi kubwa na nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii kwenye Jimbo la Katavi upande wa elimu tumefanya vizuri sana. Ninataka nichukue fursa hii na kaka yangu Profesa, Waziri wa TAMISEMI yuko hapa; tumefanya kazi kubwa na nzuri ya kujenga shule za msingi na sekondari mpya. Hata hivyo, bado tunayo kazi ya kufanya upande wa elimu. Kazi kubwa tumeifanya ya kujenga shule nzuri mpya na za kisasa, lakini tumesahau; kwamba wakati tunajenga shule mpya huku tunazo shule za zamani ambazo kwa kweli hali yake siyo nzuri. Ni vizuri Wizara ya TAMISEMI ikaja na mpango kabambe wa kwenda kukarabati shule hizi za primary na secondary ambazo ni kongwe ili ziendane na kazi ya shule hizi mpya tunazozijenga, zifanane walau hata kidogo na hizi shule mpya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende upande wa TARURA, fedha za road funds. Kule kwetu mvua zinanyesha kweli kweli. Kama kuna eneo linapata mvua nyingi na kutosha; na tunamshukuru Mwenyezi Mungu; ni Jimbo la Katavi. Nafuu hii ya kupata mvua nyingi hiyo hiyo imetuletea matatizo makubwa upande wa barabara. Tunaomba fedha za road fund zifike kwa wakati na zisifike kwa kusuasua.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninamshukuru na ninataka nimpongeze sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, wakati anazindua Bunge hapa alipigiwa makofi mengi sana na Waheshimiwa Wabunge wote baada ya kuongelea suala la TARURA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, TARURA wanazo barabara nyingi na zote ni za kiwango cha changarawe. Kwa maana hiyo kinapokuja kipindi hiki cha mvua barabara zote zile zinakuwa ni mbovu na hazipitiki. Hivi tunavyoongea, leo ukienda kwenye Jimbo la Katavi hakuna mawasiliano kati ya Kati za Mapili, Ilela, na Inyonga; hakuna mawasiliano kutoka Uzega kwenda Kijiji cha Mazelizeli. Maeneo mengi kwenye nchi nzima tatizo ni barabara. Tunaomba sana, sana sana kupitia Hotuba hii Serikali ikajipange kuhusu suala la TARURA kuongezewa fedha; hakuna mjadala

Mheshimiwa Naibu Spika, ninataka nikwambie, hakuna Mbunge hapa ambaye atasimama ambaye ametoka kijijini akasema barabara zake zina afadhali, barabara zote ni mbaya na zimechoka kweli kweli. Ninataka niwaambie Mheshimiwa Waziri Mkuu na Waziri wa TAMISEMI, asikae hapa Mzee aka-relax akafikiri huko kuko shwari; kuna hali mbaya, barabara hazipitiki. Wajipange kweli kweli baada ya hizi mvua za masika kukata waende wakarudishe mawasilinao kwenye vijiji vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninataka niongelee suala Mipango Miji. Wakati mwingine ukikaa unajiuliza, hawa watu wa mipango miji; hawa hawa Maafisa Mipango Miji unaweza kufikiri kama wamezaliwa na baba mmoja. Hawa watu matatizo yote ya mafuriko kwenye miji yetu mikubwa ukitazama chanzo chake kikubwa ni mipango miji. Hawa watu wa mipango miji (TAMISEMI) wanasomea vyuo gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, ukitazama mafuriko ya Mkuyuni pale, mimi nimesoma Shule ya Msingi Mkuyuni; wakati tunakua sisi pale Mkuyuni hakukuwa na mafuriko lakini leo, ukienda kutazama pale kwenye Kata ya Mkuyuni kila mwaka mvua zinaponyesha kunakuwa na mafuriko ya kutosha; kwani tatizo ni nini?

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo watu wa Mipango Miji wamekwenda kutoa vibali vya ujenzi maeneo ambayo wanajua kabisa hapa kuna mto unatoa maji milimani kupeleka Ziwa Victoria. Wao wamekwenda kumpa mtu kibali cha kujenga ghorofa kwenye daraja. Sasa unajiuliza, Mwenyezi Mungu amrehemu kaka yangu Marehemu Didas Massaburi, aliwahi kusema na watu wakamnukuu, hao watu sijui wanafikiri kwa kumtumia Massaburi? Sitaki kuendelea Mwenyezi Mungu amrehemu.

Mheshimiwa Naibu Spika, unajiuliza hawa watu wanafikiri kwa kutumia nini? Hapa kuna daraja, anaona kabisa huu ni mkondo wa maji, hapa anatoa kibali cha kujenga ghorofa. Maji yakija unategemea yapite wapi? Kwa kawaida maji huwa yanatafuta njia yake ya asili. Lazima kama yalipita mwaka huu, yatakuja yatapita hata baada ya miaka 100, lakini unakuta watu wa Mipango Miji wanakwenda kutoa vibali, maeneo ya mito wameweka viwanda, wameweka gereji, matokeo yake maji yanakosa njia.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninataka niende kwa haraka haraka sana kuzungumzia barabara yetu inayotoka Inyonga – Majimoto – Kibaoni – Sumbawanga. Niliwaeleza mwanzo, sisi kule ni wakulima wakubwa kweli kweli. Ili tuweze kufanya biashara vizuri, ni vizuri barabara hii ikatengewa fedha, na kila mwaka barabara hii inawekwa kwenye mpango na fedha kidogo, lakini hakuna ujenzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaiomba Serikali, mwaka huu mnapokuja kufanya majumuisho, mtueleze mna mpango gani na Barabara ya Inyonga – Majimoto – Kibaoni. Sitaki kuhangaika na mshahara wa Waziri yeyote, ninawaonea huruma watoto wake. Aje na mpango, atueleze ana mpango gani kuhusu Barabara ya Inyonga – Majimoto – Kibaoni? (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Kampala.

MHE. THOMAS M. KAMPALA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hayo machache ninaomba niunge mkono hoja. Ahsante. (Makofi)