Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Male
Party
ACT
Constituent
Ukonga
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
1
Ministries
nil
MHE. BAKARI B. SHINGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kupata nafasi hii. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kunijalia afya njema. Pia nitoe pongezi kwa Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa uteuzi mzuri wa Mheshimiwa Waziri Mkuu. Niseme wazi kwamba, mimi ni muumini wa utendaji na ziara; watanisamehe Waheshimiwa, ninakohoa kidogo; za Mheshimiwa Waziri Mkuu na maelekezo anayoyatoa; na ananikumbusha enzi na Mheshimiwa Waziri aliyepita muda wake juu ya maagizo mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri; ili nchi yetu iweze Kwenda Mheshimiwa Waziri Mkuu ni mmoja katika Jamhuri yetu ya Muungano wa Tanzania na wasaidizi wake wa karibu ni Waheshimiwa Mawaziri na Waheshimiwa Manaibu wao wakisaidiwa na watendaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, haipendezi na haileti sura nzuri kwamba mambo ambayo yanaweza yakamalizwa na Waheshimiwa Mawaziri yanaweza yakamalizwa na Makatibu Wakuu, yanaweza ya kamalizwa na Wakurugenzi, Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya yanasubiri hadi Mheshimiwa Waziri Mkuu afanye ziara ndipo wananchi waende wakalalamike kwake. Ili tuweze kuvuka ni lazima tuambiane ukweli, tusimchoche Mheshimiwa Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri Mkuu ni binadamu kama tulivyo sisi. Sasa tumpunguzie hizi ziara kwa kumwekea wepesi wa watendaji chini kutenda haki. Nina hakika tukifanya vizuri Mheshimiwa Waziri Mkuu atapata nafasi nzuri ya kufanya tathmini kwa vyombo vyake. Pia itampa nafasi Mheshimiwa Rais kuona kwamba alifanya chaguo sahihi na hivyo kwenye Serikali inayojali wananchi wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, asubuhi hapa nilimsikia Mheshimiwa Waziri wa Maliasili akizunguka mambo mbalimbali. Niweze kusema tu kwamba nilipata nafasi ya kuteta naye kidogo na amenihakikishia kwamba changamoto zilizopo kwenye Jimbo langu la Ukonga, hasa Kata za Buyuni, Chanika na Zingiziwa inayotokana na mipaka ya Hifadhi ya Kazimzumbwi, Mheshimiwa Waziri amenipa uhakika kwamba tunaenda kulimaliza baada ya kuwa limejadiliwa kwa muda mrefu sana, kwa zaidi ya miaka mitatu kwenda nyuma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, nitoe shukrani kwa Mheshimiwa Spika wetu kwa kuonesha msimamo katika jambo letu hili na wajibu wetu kama Waheshimiwa Wabunge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, kutokana na hali ya polisi wetu nilipata nafasi ya kutembelea Jimbo langu la Ukonga hizi siku chache za mapumziko na kufanya ziara kwenye Kituo cha Polisi cha Wilaya Chanika. Kituo cha Polisi cha Wilaya Chanika kinahudumia zaidi ya kata nane kwenye jimbo langu kinahudumia kata tatu. Kwa kweli kituo kile kina uhaba mkubwa wa magari kwa ajili ya kutuhudumia sisi wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kituo kile kina gari moja maalum kwa ajili ya doria na gari moja ya kiutawala; na hiyo gari moja lililobaki ni bovu, ambapo kwa maelezo ya kaimu OCD ambaye nilimkuta pale ofisini, imekuwa ikitengenezwa mara kwa mara, kwa hiyo imekuwa inapoteza ufanisi katika kutekeleza majukumu yake. Kwa hiyo ningeomba tu kwamba Serikali iangalie kwa jicho la pili umuhimu wa kuongezea gari mpya kile Kituo cha Wilaya cha Polisi pale Chanika. Kituo hiki ni muhimu sana kwa watu wa huko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hili suala la huduma za afya. Nimekuwa ninalirudia, hii ni mara ya pili. Ninalirudia hili kwa sababu inawezekana, au ninaamini kuwa Serikali ilifanya uamuzi sahihi kuweka au kufuta tozo ama gharama za kuchangia matibabu kwa watoto wa miaka zero hadi mitano na akinamama wajawazito. Ninaamini imefanya uamuzi sahihi. Hata hivyo, huko chini hicho sicho kinachotekelezeka. Nimeuliza hili kwa sababu katika ziara yangu siku chache hizi nilitembelea hospitali mbili zipo katika jimbo langu na nimekuta matendo haya bado yanaendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia katika ziara zangu tulimtembelea mzazi mmoja, alikuwa na mtoto mdogo mwenye miaka mitatu akiwa na kadi ya kliniki. Alivyofika hospitali bado alichajiwa fedha shilingi 10,000 kwa ajili ya vipimo. Hadi nilipoingilia kati ndipo ikaonekana kwamba hatakiwi kulipia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitembelea pia na kituo kingine cha afya pale kwetu, changamoto hizi zipo. Nimekuwa nikizungumza hapa mara kwa mara, kwamba wakati mwingine Serikali inaweza ikawa inachelewa kuweka fedha, lakini wakati mwingine watendaji wetu huko chini wanakuwa changamoto. Sasa sielewi, kwamba hawa watendaji; baadhi yao, si wote; vichwa ni vigumu ama tunakwama wapi? Kwa sababu Serikali ni ya umma, hospitali ni ya umma, kodi ni za umma, Serikali yetu inaiongozwa na Chama Cha Mapinduzi ama iliyoundwa na Chama Cha Mapinduzi imeweka Ilani ipo wazi, watu watibiwe bure, shida iko wapi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kule chini kuna Viongozi wa Chama Cha Mapinduzi wa Kata, wa Jimbo, wa Wilaya na wa Mkoa. Viongozi wa vyama vyetu ndiyo viwanja wetu, wanashindwa nini? Sasa ningeomba tufikie mahali sasa, Bunge litamke ama Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu itueleze wazi, kwamba tunadanganywa? Kama Serikali imeamua, tunakwama wapi ilihali sisi ni wawakilishi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa sitegemei na wala hakuna Mheshimiwa Mbunge atategemewa kuleta taarifa za uongo hapa, tunatoa tarifa za ukweli na tuna ushahidi nazo. Sasa ninaomba hili nalo lifikie mwisho. Ni aibu kwa Tanzania yetu, tunazungumzia habari ya afya kwa akinamama wajawazito, habari ya afya kwa watoto wetu, bado tukienda huko chini wanatozwa, hii ni aibu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala hili pia la watu wazima wenye miaka 60 na kuendelea; hivi bado tunahitaji mganga wa kienyeji kupiga ramli kwamba huyu mzee anakuja mezani kwako daktari akiwa na kadi yake ya NIDA inaonyesha umri wake ni miaka 60 plus, unamwambia bado aje na barua ya msamaha? Hapana, ninaomba tubadilike, twende kwenye kutafsiri matendo yetu. Tukifanya hivi hata kelele mitaani zitapungua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuendea haya mambo tunayoyazungumza humu Bungeni, watendaji huko chini wakiya-support tutakaa raha mustarehe na majimbo yatakuwa mazuri na hakika mitaani utapita utaona nyuso za wananchi zikiwa zimekunjuka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, ningependa nizungumze suala la mafuta, ambalo ni issue kubwa sana. Suala la mafuta katika nchi yetu limekuwa ni changamoto na hii si changamoto ya kujiitegemezea na hatuwezi kuwalaumu wanasiasa ama watendaji wetu; ni kulingana na mazingira ya dunia tuliyonayo kwa sasa wababe huko wanaonyeshana nguvu. Waswahili wanasema wapambanapo fahari wawili ziumiazo ni nyika. Kwa hiyo nafikiri sisi kama nyika tunaumia. Ningeomba tu, kwanza ninakubaliana na hatua ambayo inachukuliwa na Serikali katika kuhakikisha kwamba mafuta yanapatikana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mabadiliko ya bei kuongezeka ya wastani kati ya shilingi 800 hadi shilingi 1,000 ningeiomba sasa Serikali ihakikishe kuwa inakazia mkazo hapo, mafuta yasiongezeke tena; na badala yake Serikali iondoe kodi, baadhi ya kodi ifute ili bei ya mafuta isimame.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hivyo tunapozungumzia habari kidogo ya fedha iliyopanda kwenye price ya lita moja ya mafuta, tukubaliane kimsingi kwamba tunaenda kuongeza pia mfumuko wa bei. Si mfumuko wa bei bidhaa zetu tu, ni pamoja na mfumuko wa bei wa gharama zingine zote za binadamu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mazingira hayo, kama Taifa na nchi kwa ujumla, tunaomba Serikali iweze kuongeza pia posho kwa wastaafu wetu, wafanyakazi wetu ili kwenda sambamba na hali halisi ilivyo. Tukiacha bei imesimama kama ilivyo na wafanyakazi wetu ama wafanyakazi wa Serikali na kwenye viwanda binafsi na mishahara ile tunatengeneza kundi lingine la wahalifu kutafuta namna ya kumwibia mwajiri. Ninaomba sana Serikali iangalie hapo upande wa pili pia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sana. (Makofi)