Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyoitoa wakati wa Ufunguzi Rasmi wa Bunge la Kumi na Tatu, Tarehe 14 Novemba, 2025

Hon. Bakari Bakari Shingo

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Ukonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyoitoa wakati wa Ufunguzi Rasmi wa Bunge la Kumi na Tatu, Tarehe 14 Novemba, 2025

MHE. BAKARI B. SHINGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii tena. Awali ya yote nitoe shukrani kwa Mwenyezi Mungu aliyenijaalia afya njema na leo nipo hapa. Pia nitoe shukrani kwa wananchi wangu wa Jimbo la Ukonga kwa maamuzi sahihi ya kunichagua kuwa mwakilishi wao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kupongeza hotuba ya Mheshimiwa Rais, ni hotuba nzuri ya kiutu uzima yenye kujali yenye kuthamini watu wake. Hakika ni hotuba ambayo inatoka kwa mama mwenye kuwa na sifa ya kuwa mzazi na mzazi ana sifa ya ulezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na uzuri wa hotuba hiyo, Mheshimiwa Rais siyo mtendaji wa kila eneo. Ili Mheshimiwa Rais vazi ambalo amelivaa kwenye hotuba hii, vazi ambalo limempendeza liweze kuendelea kuwa vazi zuri mbele ya macho ya Watanzania, ninawaomba wasaidizi hasa Mawaziri, Manaibu wao, Makatibu Wakuu, Wakurugenzi na watendaji wengine waweze kuendelea kumvisha vazi hili Mheshimiwa Rais kwa kutekeleza haya ambayo Mheshimiwa Rais amewaahidi Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikiwa watachukua vyeo hivyo kama sehemu ya show, maana halisi ya hotuba ya Mheshimiwa Rais haitaonekana na tutajikuta na mwaka kesho tunakuja tukiwa tunarudi kwenye changamoto hizi hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninatoa wito sana huo na ninampongeza tena Mheshimiwa Rais. Nimeona Mawaziri wengi ni vijana; pia Mawaziri wengine wengi ni akinamama. Ninaomba watambue Mawaziri na Manaibu wao kwamba huko mitaani kuna wananchi wengi wamekaa wanaishi kwa matumaini kutokana na hotuba ya Mheshimiwa Rais. Kwa hiyo, ninaomba wanapokaa kwenye vikao wafikirie kwamba huko watu wanasubiri matarajio ya Mheshimiwa Rais, wakiishi kwa imani. Kwa hiyo, ni vizuri waangalie hapo. Vinginevyo tutarudi hapa kuulizana mara mbili mbili wapi wametekeleza kama Mheshimiwa Rais alivyotuletea wito wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo na kuwaomba ndugu zangu hao Mawaziri na Manaibu na Makatibu Wakuu, ninaomba nijikite kwenye sehemu mbili:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu ya kwanza ni katika kitabu hiki cha hotuba ya Rais ukurasa ule wa 23 unaozungumzia habari ya urasimishaji maeneo ya makazi. Katika Jimbo langu la Ukonga, hasa Kata ya Zingiziwa, Chanika, Buyuni, Pugu na Pugu Stesheni, kumekuwa na changamoto zisizoisha zinazotokana na mkwamo wa Mradi wa Urasimishaji Ardhi, mradi ambao ukiongea na baadhi ya wazabuni wanazungumza kwamba unatokana na migogoro ya mipaka baina ya Halmashauri ya Wilaya ya Ilala na Wilaya ya Kisarawe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia hapa ni kama watu tunagombea fito moja na huu mradi unavyochelewa pia Serikali inachelewa kupata mapato kutokana na urasimishaji ardhi. Ninaomba kwa sababu Kisarawe ni Tanzania, Ilala ni Tanzania, mamlaka inayotawala ni moja hebu watuondolee huu mvutano usiokuwa wa lazima kwetu ili wananchi waweze kupata hii huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili liwezekane, ni viongozi niliowataja miongoni mwao wenye dhamana ya hii kitu waweze kukaa kumaliza hili tatizo ambalo ni la muda mrefu. Nami pia ni mhanga wa matatizo haya ya mipaka kati ya Kisarawe na Ilala. Eneo ninaloishi Pugu Kajiungeni mguu mmoja upo Ilala mguu mwingine upo Kisarawe, lakini unapofika kwenye utendaji wa Kiserikali wao kwa wao wanavutana, Kisarawe wanavuta, Ilala wanavuta. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana tuangalie namna ya kuondokana na hiyo hali ili kweli tuweze kuishi kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais nina hakika Rais wote tunampenda ni Rais wetu wa nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua inayofuata ni Kifungu ukurasa wa tisa: ukurasa wa tisa unazungumzia Sheria ya Uchaguzi wa Wabunge inayoeleza kuwa mashauri yote ya uchaguzi yatafunguliwa kwenye Masjala ya Mahakama Kuu ambapo jimbo husika la uchaguzi lilipo. Kwa maana ya kwamba ukiwa unapinga matokeo, basi utachagua unafungua kwenye Masjala ya Mahakama Kuu katika Jimbo lako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa, kwa upande wa Zanzibar Mahakama Kuu ya Tanzania haina Masjala. Hivyo basi, hali hiyo hutoona kuwa hilo nalo ni sehemu ya kero ya Muungano na inafifisha upatikanaji wa haki hasa suala zima la uchaguzi, ukizingatia kwamba sheria ama miongozo inasema tufungue kesi mahali ambapo Masjala Kuu ilipo na kule Zanzibar Mahakama yetu ya Tanzania haina masjala. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kinachofuatia hapo ni kwamba wananchi ambao wanakuwa na haki ya Kikatiba ya kukata rufaa kwenye vyombo vyetu vya kisheria wanashindwa kuitekeleza kwa sababu huo mlango wako umefungwa. Hivyo basi, ninavyoona kwa maslahi mapana ya Taifa letu na tumeona habari ya Muungano unavyosifiwa na kadhalika. Hili nalo tulione ni sehemu ya kero. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninaomba pia watu wenye dhamana ya jambo hili waliangalie kwa mapana yake, kwamba kuna mlango watu wanakosa sehemu ya kupumulia. Kama unavyojua Waswahili wanavyosema, paka ni mnyama dhaifu sana, lakini ukimfungia kwenye chumba na wewe ukajifungia humo ndani ukafunga mlango, paka anageuka kuwa adui mkubwa sana wa mwanadamu. Ninaomba tufungue milango ili hiyo ahadi iweze kukaa sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hilo ninashauri kwa umuhimu wa pekee wakati tunasubiri mchakato wa Katiba Mpya kama Mheshimiwa Katibu Mkuu wetu alivyosema hapa, ni vizuri hili jambo liingizwe makusudi kwenye mchakato wa Katiba marekebisho madogo ili tuweze kuwapa haki Wazanzibari ambao imenyimwa ama imefungwa kwa mujibu wa miongozo ya makao makuu yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeweka nia ya kuleta hoja binafsi juu ya jambo hili ili tufikie mustakabli mzuri wa Taifa letu, kwa nia ile ile ya kumuunga mkono Mheshimiwa Rais juu ya uendeshaji wetu wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongeze pia sehemu ndogo. Hapa nilipokuwa nimekaa wananchi wangu wamenikumbusha na nilikuwa ninaongea na Naibu Waziri wa Ujenzi, lakini nimeongea na Naibu Waziri upande wa DAWASA na kadhalika, suala la Barabara yetu moja ya kutoka Pugu Kajiungeni – Pugu Kirumba – SGR.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ile ni ya vumbi japo Naibu Waziri ametwambia kwamba ina mpango wa kutengenezwa kwa lami. Katika kipindi hiki ambacho tunasubiri barabra hiyo ya lami, pale yanapita magari makubwa malori, yanapita na mizigo na ile barabara ni ya vumbi na ni katikati ya makazi. Tumekuwa na shida ya vumbi, nyumba za pale zimechoka. Wakazi wa pale wako hatarini kupata TB. Hali yao si nzuri.


Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kwa makusudi kabisa, wakati Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana wanaendelea kuchakata mpango wa kupitisha lami, basi upatikane mpango mahsusi wa makusudi. Aidha, pawe panamwagiwa maji kila siku ili vumbi liwe halipo, ama malori yale ya mradi yahamishwe badala ya kupita njia ile basi yazungukie Kilitex kutokea kwenye barabara ya lami ya Nyerere kuja huku yanakoelekea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuwasilisha, lakini mwisho wa yote nifunge kwa kusema Taifa letu amani yetu. Ninaomba wote kwa pamoja tuishi katika maneno kama hayo. Ahsante sana. (Makofi)