Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyoitoa wakati wa Ufunguzi Rasmi wa Bunge la Kumi na Tatu, Tarehe 14 Novemba, 2025

Hon. Thomas Maganga Kampala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyoitoa wakati wa Ufunguzi Rasmi wa Bunge la Kumi na Tatu, Tarehe 14 Novemba, 2025

MHE. THOMAS K. MAGANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuchukua fursa hii kumshukuru sana Mungu wa Mbinguni kwa kunipa kibali cha kusimama siku ya leo ili nichangie kwenye hotuba nzuri ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo kwa msingi mkubwa inatupa mwelekeo wa tulipotoka na wapi tunakwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka kuchukua fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; lakini kwa sababu ni mara yangu ya kwanza, ninaomba kuwapongeza sana na kuwashukuru wananchi wa Jimbo la Katavi kwa kura nyingi za kishindo walizonipa ambazo zimeniwezesha mimi leo kuwa mbele yako hapa kuchangia katika Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Mheshimiwa Rais anakuja kwenye Jimbo la Katavi tulimwambia Mheshimiwa Rais kakae kwa kutulia sisi Jimbo la Katavi tutakupigia kura kama tumechanganyikiwa, tulikuwa tunazo sababu. Katika kipindi cha miaka minne tangu Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ameingia kwenye nafasi 2021 – 2025, Jimbo la Katavi tulipokea fedha shilingi bilioni 27.665 kwa ajili ya shughuli za maendeleo. Wakati Mheshimiwa Rais anaingia, katika nafasi yake ya urais, Jimbo la Katavi fedha hizi nyingi tuliziwekeza kwenye shughuli za maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya elimu, wakati Mheshimiwa Rais anaingia, katika Halmashauri ya Wilaya ya Mlele tulikuwa na shule za msingi 13. Katika kipindi cha miaka minne tumetoka shule 13 hadi 29. Tunaposimama hapa tunampongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, hatuji kufanya mbwembwe, tunapongeza yale ambayo mama huyu amyafanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda upande wa elimu hapohapo, elimu ya sekondari amekuta shule za sekondari tano. Hadi mwaka 2021 – 2025, tumetoka kwenye shule za sekondari tano mpaka 11 katika kipindi cha miaka minne. Hizi tano ninazoziongea ni tangu uhuru, hizi sita ni katika kipindi cha miaka minne; kwa nini tusimpongeze mama huyu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya afya, wakati mama huyu anaingia 2021 – 2025 tulikuwa na vituo vinavyotoa huduma za afya tisa; leo katika kipindi cha miaka minne vituo vya afya vinavyotoa huduma za afya viko 17. Kwa ongezeko la zahanati sita, kituo cha afya kimoja, hospitali ya wilaya moja, magari ya kubebea wagongwa manne ndani ya miaka minne. Kila anayefanya kazi anastahili kupongezwa. Tunaposimama kumpongeza mama huyu, hatusimami kumsifia, tunampa moyo kwa kazi alizofanya ili aendelee kufanya zaidi na zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya kilimo, kulikuwa kuna changamoto nyingi sana. Hivi leo tunavyoongea wakulima wa Jimbo la Katavi wanapata mbolea ya ruzuku. Nikija kwenye kitabu hiki cha Hotuba ya Mheshimiwa Rais, ninaomba ninukuu; ukijikita kwenye sekta ya uzalishaji ukurasa wa 20, Mheshimiwa Rais; hapa ninataka kuweka msisitizo; Mheshimiwa Rais amesema:

“Katika miaka mitano ijayo tunakwenda kufanya uwekezaji mkubwa kwenye sekta za uzalishaji tukianza na kilimo. Tutaongozwa na dhana ya kilimo ni biashara ni mwekezaji. Lengo letu ni kuongeza kasi ya ukuaji wa sekta hii kutoka asilimia nne ya sasa hadi kufikia 10% ifikapo 2030. Kwa kufanya hivyo tunalenga si tu kujihakikishia utoshelevu wa chakula bali pia tunawekeza kwenye mnyororo wa thamani ili kuwanufaisha Watanzania wengi walioajiriwa kwenye sekta hii. Tunakusudia kufanya Watanzania wengi kuwa miongoni mwa wazalishaji wakubwa wa mazao ya mahindi, mchele na mbogamboga (horticulture) Barani Afrika. Tutafanya hivyo kwa kujielekeza kwenye kilimo cha kisasa kwa kuongeza pembejeo kama mbegu bora, mbolea, viatilifu kwa ruzuku. Tutaongeza upatikanaji wa maji kuhakikisha kuongezeka eneo la kilimo cha umwagiliaji kutoka ekari milioni 3.4 hadi milioni tano”.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa ninataka kusisitiza; kwenye upande wa kilimo cha umwagiliaji, sisi Jimbo la Katavi tuna maeneo mengi yanayofaa kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji. Kilimo cha umwagiliaji si tu kinakwenda kutuongezea mazao ya chakula na ya biashara, kinakwenda kutoa suluhu ya ajira kwa vijana na kuwazuia vijana wanaotoka vijijini kukimbilia mijini. Serikali ikifanya proper investment kwenye irrigation scheme vijana watavutika kuingia kwenye kilimo cha umwagiliaji na badala yake hawatatoka vijijini kuja mjini. Tunaiomba sana Serikali kufanyia mkazo maneno haya ya Mheshimiwa Rais. Maneno haya yakifanyiwa kazi vizuri, hata wimbi la vijana kwende mjini hawatakuja kuwaona tena. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapoongelea mafanikio ya eneo lolote lile na kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, wapo viongozi kwenye maeneo yetu wanafanya kazi vizuri sana. Kwenye eneo langu la Jimbo la Katavi kwa mahsusi ninaomba kuchukua fursa hii kuwapongeza viongozi wafuatao, Alhaj DC Majid Mwangala na Mkurugenzi dada yangu Singlida Mndema. Ninawapongeza hawa makusudi. Haya yote tunayoyaona yamefanyika kwenye eneo letu, wamesimamia vizuri fedha zilizokuja kwenye Jimbo la Katavi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, safari bado ni ndefu; mama huyu anayo dhamira ya dhati ya kuwatumika Watanzania. Tusimame tumsemee, hakuna kiongozi anaweza kusimama akasema mwenyewe, twende tukamsaidie mama huyu kusema yale yaliyofanyika. Ninataka niwaambie, katika kipindi cha hii miaka mitano tunayoianza na kwa hotuba hii tunakwenda kuona matokeo makubwa katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia ninataka pia kuwashukuru sana viongozi wenzangu na ninaendelea kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan na kumtia moyo. Mama aendelee kufanya kazi, sisi viongozi na Waheshimiwa Wabunge tuko nyuma yake na tutamlinda kwa gharama yoyote ile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)