Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyoitoa wakati wa Ufunguzi Rasmi wa Bunge la Kumi na Tatu, Tarehe 14 Novemba, 2025

Hon. Ado Shaibu Ado

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Tunduru Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hotuba ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyoitoa wakati wa Ufunguzi Rasmi wa Bunge la Kumi na Tatu, Tarehe 14 Novemba, 2025

MHE. ADO S. ADO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili niweze kutoa mchango wangu juu ya hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambayo aliitoa katika Bunge hili Tukufu. Kwa sababu, hii ni mara yangu ya kwanza kusimama rasmi katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuchangia hoja, ninaomba nitumie fursa hii kwanza kuwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Tunduru Kaskazini ambao kwa muda mrefu sana wamekuwa wakiniunga mkono kisiasa na leo ninasimama katika Bunge hili kama mwakilishi wao, ahsanteni sana Wanatunduru. Ahadi yangu kwa Wanatunduru, nitasimama imara, kwa ajili yao, kwa ajili ya kutetea maslahi yao bila kuchoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kuchukua fursa hii kukishukuru Chama changu cha ACT-Wazalendo ambacho kimefanya uamuzi wa kuniruhusu mimi na Wabunge wenzangu nane wa ACT-Wazalendo, ili tuweze kushiriki katika Bunge hili la Kumi na Tatu. Kwa mazingira ya Uchaguzi wa Mwaka 2020 uamuzi huo haukuwa mwepesi, lakini kama inavyofahamika siasa ni hesabu na uwepo wetu ndani ya Bunge hili ni hesabu za kulitumikia Bunge hili, kama chombo cha mapambano ya kupaza hoja na kuwasilisha sera mbadala. Historia itatuhukumu kama uamuzi huo wa kimkakati ulikuwa ni uamuzi sahihi ama la.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahadi yangu na wenzangu ni kwamba, sisi tutatekeleza wajibu huo ndani ya Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania bila hofu wala kusita, lakini pia tutatoa michango yetu kwa hoja badala ya vioja. Hiyo ndiyo ahadi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais amezungumzia mambo mengi katika hotuba yake, mimi nitajikita katika maeneo makubwa matatu, la kwanza nitazungumzia juu ya mwelekeo wa kisiasa wa nchi yetu. Tangu tulivyoanza kutoa mawazo yetu ndani ya Bunge hili, Wabunge wengi wamezungumza kwa haki kabisa juu ya umuhimu wa amani na juu ya umuhimu wa vijana kupenda Taifa lao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nukta moja ambayo imeachwa katika mijadala yetu na mimi ninaisema ni juu ya umuhimu wa haki, ili kupata amani ya kweli. Amani ni zao la haki na demokrasia, bila demokrasia hakuna haki, bila haki hakuna amani, bila amani hakuna maendeleo. Hiyo ndiyo principle. Kwa hiyo, ukiwa unazungumza juu ya amani hata kama utakesha kusisitiza watu wapende amani na watu waipende nchi yao, kama husisitizi juu ya haki huwezi kupata amani ya kweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumefarijika ndani ya hotuba ya Mheshimiwa Rais, ukiacha zile hatua za kutibu majeraha ya uchaguzi wa 2025 amezungumza juu ya ahadi ya Serikali kufufua mchakato wa Katiba mpya. Hilo ni jambo jema kabisa, lakini nakisi ambayo sisi tunaiona, huwezi kuwa na mchakato bora wa Katiba mpya kwa kutaja ahadi ya Katiba mpya peke yake. Sisi tunaona kwamba, Katiba mpya inashughulikiwa kwa vipandevipande; kipande ambacho tumepewa sasa ni kwamba, kutakuwa na Tume ya Usuluhishi ndani ya siku 100.

Mheshimiwa Mwenyekiti, rai yetu sisi ni mchakato huu ushughulikiwe comprehensively. Tunataka Serikali ije na ratiba kamili ndani ya Bunge hili ya namna mchakato wa Katiba mpya utakavyoendeshwa. Pia, tunataka Serikali itueleze juu ya approach au mtindo ambao itautumia kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kujipatia katiba yake na sisi tumekuja na mapendekezo. Hatua ambazo tunazipendekeza ni za muhimu sana katika mchakato huo na ni vizuri mapema sana Serikali inapotoa ahadi itueleze, kama hiyo ndiyo route ambayo itaipitia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, tunahitaji kuzifanyia mapitio Sheria zinazosimamia mchakato wa Katiba mpya, kwa maana ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba Mpya pamoja na Sheria ya Kura ya Maoni; hiyo ni hatua ya kwanza muhimu sana. Ya pili ni tunahitaji kuwa na Mkutano wa Kitaifa, kwa maana ya National Sovereign Conference, kwa ajili ya kupata muafaka wa pamoja juu ya masuala ya Kikatiba, ambayo mpaka sasa hayajapata muafaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua ya tatu ya muhimu ni lazima tuwe na timu ya wataalam, kwa maana ya Committee of Experts, ambao wataandaa Rasimu ya Katiba Mpya na hatua ya mwisho ni tunahitaji kuwa na kura ya maoni. Kwa hiyo, tunavyoitamka Katiba mpya tusiishie kuitaja kwa ujumla wake, tuwe na road map ambayo itawafanya wadau wote wa Katiba Mpya wajue mchakato utakwenda namna hii. Hilo ni la kwanza ninataka kulisisitiza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, jana limezungumzwa kidogo na ninaheshimu taratibu. Ninafahamu kwa mujibu wa Kanuni ya 81, Mwongozo wa Spika ni wa mwisho juu ya suala. Kwa hiyo, sitoliibua tena suala hilo, isipokuwa nina rai kwamba, ahadi ambayo Mheshimiwa Rais ameitoa ya kuachiwa huru kwa wale ambao walikamatwa katika matukio ya tarehe 29 ni ahadi njema. Vyombo ambavyo vinahusika, Wizara ya Mambo ya Ndani na Wizara ya Katiba na Sheria, zifanye uchunguzi wa kina, zijiridhishe kama watu wote wameachiwa huru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapofungua ukurasa mpya wa kisiasa ukiwa na mtu mmoja umemwachia huru, siyo yeye peke yake, unakuwa umeigusa roho yake, familia yake na ukoo wake. Unawatoa kwenye masononeko, unaifanya nchi iwe na furaha na kinyume chake ukiwa na mtu mmoja amewekwa ndani, ametekwa au amepotezwa, siyo yeye peke yake bali ukoo mzima unakuwa kwenye masikitiko na unatengeneza Taifa lenye huzuni. Huo ni mchango wangu wa pili niliotaka kuusema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu na la mwisho, ninawakumbusha mabosi wangu, wananchi wa Tunduru, kwanza imesemwa juu ya kuboresha huduma za maji; Tunduru tuna mradi mkubwa sana wa maji. Pale Tunduru Mjini usambazaji wa maji hivi sasa upo kwa wastani wa kilomita 3.3, hivi mtandao wake. Tuna mradi mkubwa wa maji wa shilingi bilioni 3.4 ambao ungeweza kusaidia mtandao wa usambazaji wa maji Tunduru ufikie kilomita 92, lakini ule mradi mpaka sasa unasuasua. Tunaitaka Serikali ilitazame hili kwa sababu, tunaamini ni game changer katika kuboresha maisha ya Wanatunduru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine linalowahusu mabosi wangu, Wanatunduru, ni suala la umeme. Mbunge mwenzangu Mheshimiwa Chilombe yupo hapa na tunashirikiana vizuri, ataendelea, ni mtaalam wa umeme, lakini niseme hivi kwamba, pale Tunduru tuna mradi mkubwa sana wa umeme ambao ukikamilika utatupa megawatts 120 wakati mahitaji yetu ni megawatts nne. Maana yake ni Tunduru tutakuwa na umeme mwingi sana wa ziada, tunasubiri kwa hamu mradi huo uweze kukamilishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa ukitazama mradi unasuasua kwa sababu, mkandarasi hajapata fedha za kuendelea na mradi. Vifaa viko site amekwishapeleka vifaa vingi pale, lakini umeme wa uhakika hujapatikana, ndiyo maana hivi sasa ukienda Tunduru, mimi nina hakika, tutakuta eneo ambalo linaweza kuingia katika kitabu cha historia ya maajabu ya kukatikakatika kwa umeme. Tunduru inaweza ikawa namba moja kwa sababu, umeme unakatika mara 20 kwa siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wataalam wanatwambia ni kwa sababu, njia ya umeme inapita katika miji mingi. Haya ni maelezo ya kitaalam, mwananchi wa kawaida hayaelewi hayo, yeye anadhani Serikali imelala na imefeli. Kwa hiyo, tunaomba mkandarasi yule apewe fedha.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MHE. ADO S. ADO: ...ili mradi uendelee. Ahsante sana.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa.


TAARIFA

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ninampongeza anayetoa hoja, lakini ninatokea Tunduru, umeme haukatiki mara 20 kwa siku. Ahsante. (Makofi/Kicheko)

MWENYEKITI: Unaipokea hiyo Taarifa?

Muda wako pia, umeisha.

MHE. ADO S. ADO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu, muda wangu umeisha watakaotuhukumu kama umeme unakatika mara 20 ama la, siyo Bunge hili ni Wanatunduru, tukutane site. Ahsanteni sana. (Makofi)