Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Nachingwea
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
2
Ministries
nil
MHE. FADHILI A. LIWAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nitumie fursa hii adhimu sana kuungana na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia afya njema na uzima iliyotuwezesha sote kuweza kukutana kwenye jengo hili Tukufu kwa ajili ya kujadili mustakabali wa Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba uniruhusu kipekee kabisa na kwa shukrani za unyenyekevu kutoka ndani ya sakafu ya moyo wangu kuwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Nachingwea kwanza kwa kukubali, kuridhia na kunichagua mimi kuwa Mbunge wa Jimbo la Nachingwea. Pili, kwa kumchagua kwa kura nyingi na za kishindo, na za heshima Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Tatu, kwa kushiriki na kuendesha vizuri zoezi la Uchaguzi Mkuu toka katika kipindi cha kampeni mpaka siku ya kupiga kura wakiwa wamejijengea utulivu wa kuchagua viongozi waliowapenda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nami pia nitumie fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu moja kwa kuchaguliwa kwake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nimeisoma na nimeipitia hotuba aliyoitoa Bungeni tarehe 14. Katika hotuba ile Mheshimiwa Rais amejielekeza katika vipaumbele, ameonyesha umadhubuti, ameonyesha nia na amefungua mwanga wa Tanzania kubwa tunayoitarajia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais ameweka vipaumbele mahususi na amejipambanua kutokana na mwelekeo wa nchi ya dunia ya sasa inavyotakiwa kwenda kwa kuzingatia masuala mtambuka mbalimbali yanayoijenga dunia ya leo katika masuala ya kimaendeleo katika maeneo ya teknolojia, huduma za jamii, hali za vijana na mambo ya usalama wa nchi. Mheshimiwa Rais kila kitu amekiweka vizuri. Naomba kutumia fursa hii kumpongeza sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka nimhakikishie Mheshimiwa Rais kwamba hotuba hii aliyoitoa hapa Bungeni ndiyo itakuwa dira, itakuwa mwelekeo na ndiyo itakuwa tochi itakayotuangazia Watanzania kuyaelekea maendeleo ya kweli katika siku zote za kuitumikia nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba Mheshimiwa Rais amejipambanua wazi kabisa, lakini ninaomba uridhie niweke jambo moja kutoka katika kitabu kitakatifu. Kwa wale wasomaji wa Biblia watakubaliana na mimi kwamba baada ya Musa kuwachukua Wanaisraeli kutoka nchi ya utumwa alipowapeleka kwenye nchi yao ya utawala na kuishi, Musa ndiyo alikuwa kiongozi aliyetumainiwa, aliyetegemewa na ambaye alionekana ndiyo mustakabali wa Taifa la Wanaisraeli. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Biblia inaeleza na hadithi iko wazi kabisa Musa naye alikufa sambamba na kuwa alipendwa na alihitajika. Wakati Musa anawaacha Wanaisraeli ni kama Taifa ambalo liliulizana nani anakuja kuwa Musa wa pili atakayetuvusha na kutupeleka kwenye nchi ya asali iliyoahidiwa. Mungu akamwinua mtu anaitwa Joshua akamwambia wewe ninakupa kazi ya kuwachunga kondoo wa Israeli na wafike kwenye nchi ya asali na maziwa wakiwa salama na wenye furaha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukimsoma vizuri Joshua katika maandiko matakatifu anasema wakati anapokea nafasi ya uongozi hata yeye mwenyewe alibaini kwamba wako watu wanaweza wasielewe na kuamini kuwa ni Joshua mwenye nguvu atakayevusha wana wa Israeli ndipo Mungu akamwambia Joshua uwe hodari na moyo wa ushujaa, usiogope wala usifadhaike kwa kuwa Bwana Mungu wako yuko pamoja nawe kila uendako. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka niyachukue maneno haya niyaweke katika fikra, mwelekeo, mtazamo na dhima ya Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwamba amepokea kijiti kutoka kwa Musa na wakati anapokea inawezekana yako mashaka lakini kwa kazi, huduma na mwelekeo aliouonesha katika kipindi cha miaka minne mpaka sasa inatosha kabisa kutupa matumaini ya kuvuka bila mashaka yoyote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, basi na Watanzania wenzangu kama leo dunia itatuamsha na kuuliza Rais wa Tanzania anapenda nini? Jibu nitakalolitoa nikiwa nimeamka anaipenda nchi yake kuliko kitu chochote. Kama leo dunia itaniuliza unajivunia nini kwa Rais wako, nitawaambia nitajivunia kuwa na Rais aliyewatoa watoto wa kimaskini kutembea umbali mrefu kufuata elimu kwa kuwajengea mabweni na shule karibu na maeneo yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama dunia itaniuliza kwa nini unamsemea Rais wako nitawaambia ninamsemea Rais aliyeendeleza na kufufua miradi mipya ya kimkakati ambayo ingeweza kukatisha tamaa. Nitawapa ushuhuda wa Bwawa la Mwalimu Nyerere, Daraja la Kigongo Busisi, Miradi mikubwa ya Hospitali za Kanda, Hospitali za Mikoa, Hospitali za Rufaa, Hospitali za Wilaya, Zahanati pamoja na Vituo vya Afya ambavyo Dkt. Samia Suluhu Hassan amevijenga kwa nguvu, uwezo na mapenzi makubwa kwa nchi yake ya Tanzania. (Makofi)
MHE. ZAINABU R. KAWAWA: Taarifa.
MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa.
TAARIFA
MHE. ZAINAB R. KAWAWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ninampongeza msemaji, mdogo wangu Fadhili Liwaka, lakini ninataka kumwongezea taarifa kwamba nami pia nitamsemea Mheshimiwa Rais kwa mradi mkubwa wa Bandari ya Uvuvi katika Wilaya ya Kilwa, hii ni bandari ya kimkakati ambayo iko katika 90% na zaidi, hivi karibuni inakaribia kumalizika, lakini ni Bandari kubwa katika ukanda huu wa Nchi za Afrika Mashariki ambayo haijawahi kujengwa popote pale. (Makofi)
MWENYEKITI: Mheshimiwa ahsante, Mheshimiwa Fadhili unaipokea taarifa hiyo?
MHE. FADHILI A. LIWAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipokea taarifa hiyo Mheshimiwa Mwenyekiti kwa dada yangu ninayemheshimu sana na bado ninamwongezea kwamba dunia ikiniamsha juu ya Uchumi wa Bluu nitawaambia ninamsemea Rais aliyethubutu kujenga Bandari za Uvuvi, kujenga meli za usafirishaji za watu na mizigo na aliye tayari kuhakikisha kwamba wavuvi kwenye Ukanda wa Maziwa na Bahari Kuu wanapata mafanikio makubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya utangulizi huo na kuweka mwelekeo wangu na mtazamo ambao ninatamani kila Mbunge na Mtanzania auone kwa Rais wetu, ninaomba nijielekeze kwenye mambo matatu ambayo kwenye hotuba Mheshimiwa Rais ameyaweka vizuri na sisi tunahitaji msisitizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza nitumie fursa hii sasa kumpongeza sana Dkt. Samia Suluhu Hassan, pia niwapongeze Mawaziri waliotoa huduma kwenye Wizara ya Madini. Moja kati ya jambo kubwa ambalo nchi yetu inaweza kujivunia ni uwepo wa rasilimali ya madini, tena madini yenye thamani kubwa sana hata pale nchi yetu inapotoa sauti duniani juu ya kwamba tunayo thamani ya madini ambayo inamezewa mate hatutoi kwa bahati mbaya au kujifurahisha, tunatoa kwa sababu mlio wa mgonjwa, anayeujua ni muuguzi na sisi ndio wauguzi wa nchi yetu.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, katika eneo hili Serikali imeweka mikakati madhubuti; moja, kuhakikisha tunavutia uwekezaji katika eneo hili la madini na tumeona pato la Taifa limeongezeka kutoka kwenye Sekta ya Madini kutoka asilimia 6.8 mpaka 10.1%. Hii ni kazi kubwa sana na imefanywa na sekta pamoja na Wizara ya Madini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kumpongeza sana kaka yangu Mheshimiwa Mavunde na Naibu Waziri kwa kazi kubwa ya usimamizi na sisi sote tutakuwa mashahidi tumeona Wizara ikihangaika. Jambo la kwanza ni kuweka utaratibu mzuri wa uwekezaji kwenye eneo la madini, lakini eneo la pili, kuhakikisha Watanzania wanakuwa matajiri kwa kuwa wachimbaji wazuri kupitia maeneo ya wachimbaji wadogo wadogo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka niungane nao na kuwatia shime kwamba moja ya jambo litakalolitoa Taifa na kusogea mbele zaidi kwenye eneo la Sekta ya Madini pamoja na mikakati iliyoelezwa katika Hotuba ya Mheshimiwa Rais ya kuhakikisha tunaongeza thamani ya madini, tunafungua kituo cha uzalishaji wa madini East Africa. Hata hivyo, ni sharti letu la msingi na ni muhimu kuwatambua, kuwaelekeza na kuwajenga wachimbaji wadogo nchini ili waweze kupata ngazi ya utajiri na kuwa wachimbaji wakubwa ili tuwe na Taifa lenye thamani ya mali zilizopo hapa chini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwelekeo wa uchimbaji wa madini nchini unakwenda vizuri kwa sababu tumeona leo tukihesabu idadi ya Watanzania waliopata uwezo wa kujisimamia na kuweza kufanya shughuli za uchimbaji haiwezi kulinganishwa na miaka 15 iliyopita, kwa sasa tumepiga hatua kubwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ninaomba niweke maneno yangu kwenye jambo moja. Nimesoma vizuri hotuba Mheshimiwa Rais na nimeona mwelekeo katika suala la kupambana na kusaidia kuwaondoa wanyama waharibifu ambao ni ndovu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninatoka jimbo ambalo 75%, wakati ninaomba kura ya wananchi kila nilipokwenda moja ya hoja niliyokutana nayo ni wanyama waharibifu aina ya Ndovu. Ninafahamu ndovu hawa wanalindwa na sheria maalum ya kimataifa. Ziko nchi ambazo ziliwahi kupitia changamoto kubwa ya wanyama wengi wa aina hii kama vile Sri-Lanka, India, Sierra Leone na nchi zingine nyingi sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, yako mambo mahususi ambayo kama nchi tukiamua kuyaweka tunaweza kusaidia kuwaondoa wananchi wetu kwenye adha ya hawa wanyama ambao sio tu wanamaliza mazao ya watu bali wanahatarisha usalama na maisha ya Watanzania kwa sababu wanaua. La kwanza ziko njia ikiwemo zile ambazo zimeainishwa na Wizara. (Makofi)
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kuwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Mheshimiwa muda wako umekwisha.
MHE. FADHILI A. LIWAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sana na ninaunga mkono hoja. (Makofi)