Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Kivule
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
1
Ministries
nil
MHE. DOUGRAS D. MASSABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema, leo kwa mara ya kwanza ninasimama ndani ya Bunge hili Tukufu kwa ridhaa ya wananchi ya Jimbo la Kivule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kumpongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, mwanadiplomasia nguli Afrika na dunia ambaye alichaguliwa na Watanzania kwa zaidi ya 97%.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uchaguzi ule ulitafsiriwa na kazi kubwa aliyoifanya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa miaka yake minne ya uongozi, lakini alionekana kwenye mikutano mbalimbali ya wananchi kwa namna ambavyo wananchi walifurika kadiri ambavyo alikuwa akitembea katika mikoa yote takribani 32.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuzunguka kwake, ahadi zake zilisheheni matarajio ya Watanzania, na ahadi zake zilimgusa Mtanzania mmoja mmoja. Wakati Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan anaingia madarakani, alikuja na falsafa ya 4R.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika falsafa yake ya 4R ilimfanya kutambulika duniani na Mataifa ya nje na kupelekea kuwa kinara kwenye masuala ya haki za binadamu, uhuru wa habari, uhuru wa dini na kadhalika. Kiongozi ni lazima uwe na ngozi ya mamba. Hata nyakati ambazo zilikuwa ngumu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan alituvusha salama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mtakumbuka tulipata fedha za IMF kwa ajili ya kuzuia na kujikinga kipindi kile cha Covid. Tunao Ushahidi wananchi wa Jimbo la Kivule tulipata takribani shilingi bilioni 4.6. Dkt. Samia Suluhu Hassan aligeuza kuwa fursa na tukapata zaidi ya madarasa 232, wananchi wa Jimbo la Kivule wanapata elimu iliyo bora. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana tukasema ya kwamba Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kazi kubwa aliyoifanya na mageuzi makubwa aliyoyaleta katika mashirika ya umma ilikuwa ni chachu ya kuwaletea maendeleo kwa wananchi wa chini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitasoma kwa haraka haraka mambo makubwa na mageuzi aliyoyafanya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kipindi cha miaka yake minne. Kwanza aliongeza Government Investment Value kukutoka shilingi trilioni 67 hadi shilingi trilioni 92, sawa na 36% ya ongezeko la mitaji katika mashirika ya umma. Kwa maarifa hayo ya Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ilimpelekea kuvuna fedha nyingi za gawio la Serikali kutoka shilingi bilioni 637 hadi shilingi trilioni 1.028 mwaka 2020/2025.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi kubwa imefanyika kwenye mageuzi. Tumeona namna ambavyo Serikali imewekeza katika mashirika yasiyokuwa ya kiserikali. Tumepata ongezeko kutoka shilingi bilioni 153 mwaka 2020/2021 hadi shilingi bilioni 263 mwaka 2024/2025, sawa na ongezeko la 72%. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ameendelea kuimarisha mashirika ya kimkakati. Shirika la TANESCO lilikuwa linajiendesha kwa hasara, lakini leo hii faida imeongezeka kutoka shilingi bilioni 8.9 hadi shilingi bilioni 21.9 yenye capital ya shilingi trilioni 2.4. Tumeona mashirika mengine kama TPDC ambao wametoka profit ya shilingi bilioni 159 hadi shilingi bilioni 306 kwenye mtaji wa shilingi trilioni 2.7.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona mashirika ambayo yalikuwa hayatoi gawio, mfano TAZAMA Pipeline leo hii imeendelea na Serikali inapata faida kutoka kwenye magawio na maeneo hayo. Pia tumeona namna gani tumeendelea kuongeza hisa katika kampuni za madini ikiwa ni utekelezaji wa Sheria ya Madini ya Mwaka 2017. Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan amekuwa akifanya hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, haya ni mageuzi makubwa, lakini hayakuishia tu kwenye Kitaifa, mageuzi haya yameshuka chini na kumgusa mwananchi mmoja mmoja. Hivi leo mimi ninavyozungumza hapa Jimbo letu jipya la Kivule halikuwa na maji, kwa maana maji yalikuwa ni asilimia sifuri. Leo tunapozungumza ndani ya miaka yake minne maji yamefika 48%. Amejenga tenki kubwa la maji la lita milioni tisa lenye thamani zaidi ya shilingi bilioni thelathini. Maji yale yanatembea Ilala nzima, kwa maana Jimbo la Segerea, Jimbo la Ukonga zamani, pamoja na Jimbo letu jipya la Kivule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia mitambo ile ya maji aliyoinunua kwa kila mkoa takribani mwezi mmoja uliopita, kaka yangu Mheshimiwa Juma Aweso alikuja Jimbo la Kivule na watu wa Kivule tukapata mitambo ile, na sasa visima takribani 10 vinaendelea kuchimbwa ndani ya Jimbo letu Jipya la Kivule (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiacha masuala ya maji, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan amefanya kazi kubwa katika sekta ya elimu. Leo hii sisi wananchi wa Kivule tulikuwa hatuna kidato cha tano na cha sita, lakini sasa zimejengwa shule za sekondari mpya za kutosha, tena nyingine zenye hadhi ya gorofa. Tunayo Shule ya Sekondari ya Kitunda Relini, tunayo Shule ya Sekondari ya Kipunguni zenye hadhi ya ghorofa ndani ya Jimbo leu jipya la Kivule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwenye sekta ya afya, jimbo lile ni jipya, wakati Mheshimiwa Rais anaingia madarakani hakukuwa na kituo cha afya hata kimoja, leo tunapozungumza kwenye kata zetu zote sita tuna kituo cha afya kimoja kikubwa kwenye Kata ya Kivule chenye mfano wa hospitali ya Kiwilaya, na kingine kikubwa zaidi Kata ya Mzinga zenye thamani ya shilingi bilioni 4.9 chenye thamani hiyo, na vifaa vya kutosha. Wananchi wa Kata ya Mzinga na Jimbo la Kivule wanapata huduma ya afya kwenye maeneo hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nijikite sasa, kwenye mpango ambao tumeuona kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Tarehe 14 Novemba, Mheshimiwa Rais ametoa dira lakini pia ametupatia hotuba. Hotuba yake ilisheheni mahitaji ya Watanzania hasa vijana na akina mama. Utaona namna gani alikuwa anajaribu kuunganisha ujenzi wa vyuo vya VETA pamoja na mikopo ya 10% ya akina mama na vijana ili kuweza kutengenza matajiri wa baadaye.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nitumie fursa hii kumshukuru sana Dkt. Samia Suluhu Hassan, baada ya kuona congestion kubwa kwenye Chuo cha VETA cha pale Chang’ombe ambacho kipo Wilaya ya Temeke, nasi watu wa Ilala sasa tunakwenda kupata Chuo chetu cha VETA ndani ya Wilaya ya Ilala.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari tumepata fedha kutoka kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, kaka yangu Elihuruma, tumenunua eneo kubwa la hekari tisa kwa ajili ya ujenzi wa Chuo cha VETA ili kuweza kuwanyanyua na kuwasaidia vijana wanaoishi ndani ya Wilaya yetu ya Ilala. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba tunaomsaidia Mheshimiwa Rais, tunapaswa ku-walk the talk; yaani kutembea mle ambapo Mheshimiwa Rais anatarajia. Hapa imetajwa sekta yetu ya ujenzi, amesema anakwenda kuongeza bajeti TARURA na kuongeza bajeti kwenye Wizara ya Ujenzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kaka yangu pale, Mheshimiwa Chaurembo aliuliza swali, Barabara ya Msongola kuelekea Mbande mpaka Chamazi, tukapata majibu ya Naibu Waziri kuwa ni kusuasua na uwezo wa mkandarasi. Sisi watendaji tunapaswa kupata wakandarasi watakaotusaidia kupata value for money na ku-achieve zile 5R of procurement ili miradi yetu iweze kukamilika kwa wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru Mheshimiwa Rais, katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi Barabara yetu ya kutoka Banana – Kitunda – Kivule – Msongola tayari mkandarasi anaifanyia kazi, na tumeahidiwa kufikia mwezi wa Nne lami ile itakuwa imekamilika na wananchi watakuwa wanaitumia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kuwaomba viongozi wetu wa Kiserikali, Waheshimiwa Mawaziri, waendelee kuliangalia kwa jicho la kipekee Jimbo letu Jipya la Kivule. Barabara ya kutoka Pugu kuelekea Majohe kuelekea mpaka Mbondole; Barabara ya kutokea pale Kitunda kuelekea Magole kupitia Nyangasa; Barabara hiyo hiyo kutokea Kitunda kuelekea Mwanagati ni takribani kilomita thelathini na nane, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ameziorodhesha kwenye Ilani ya Chama cha mapinduzi. Kazi yetu sisi ni moja tu, kusimamaia mradi ule wa DMDP uweze kukamilika kwa wakati na barabara nyingine zilizobakia takribani kilomita 50 ndani ya Jimbo letu Jipya la Kivule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema hayo, itoshe kusema ya kwamba, sisi wananchi wa Kivule tunamshukuru Mheshimiwa Rais kwa kutupatia jimbo letu jipya, na kutupatia mwakilishi ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nasi tupo tayari kumsaidia Mheshimiwa Rais kuisimamaia Serikali kutekeleza wajibu wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga hoja, ahsante. (Makofi)