Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Ikungi Mashariki
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
1
Ministries
nil
MHE. THOMAS M. KITIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia japo kidogo kwenye hoja aliyoleta Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kifupi ameweka hoja ambayo imesheheni mambo mbalimbali. Kwa hiyo, ninachukua fursa hii kwanza kabisa kumpongeza yeye, kuipongeza Serikali hii ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambayo inaongozwa na Mheshimiwa Rais wetu, mama yetu, kwa hatua kubwa na katika kupanga safu ambayo ndiyo inakwenda kuweka msingi wa awali wa Dira yetu ya Miaka 25 ijayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hoja hii iliyoletwa na Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa, maana ya bajeti ya kwanza kabisa, ndiyo inayoweka msingi imara. Wanasema, nyumba bila msingi imara, hiyo nyumba huenda isiwe imara, kwa maana hiyo, hapa ndiyo tunaanza kuweka ule msingi wa miaka 25 kwa Bunge hili. Bunge hili litaweka historia kama tukiweka msingi wa zege, msingi wa mawe, basi msingi huu ndiyo utakaotuhakikishia hii miaka 25 tunaenda kuivuka vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninampongeza pia Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa ziara yake aliyokuwa akiifanya mikoani. Pia, ninatumia fursa hii kumpongeza Mkuu wangu wa Mkoa na Mkuu wangu wa Wilaya kwa sababu, wamekuwa wakitembea kutatua kero na kuzisikiliza. Kwa namna nyingine wameweza kusaidia kuhudumia wananchi wa Mkoa mzima na Wilaya yetu ya Ikungi, ninawapongeza sana na watendaji wote wa Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tukienda kwenye hoja aliyoleta Mheshimiwa Waziri Mkuu, amesema katika dhima hii ambayo ameiita “Mageuzi Katika Kukuza Uchumi na Kuzalisha Ajira” kwa maana ya Mpango wa Nne wa hii miaka mitano, ambayo tunaianza sasa hivi. Tunategemea kwamba, haya yote Waheshimiwa Wabunge waliyozungumza yataakisi haya mageuzi, ambayo Mheshimiwa Waziri Mkuu amekwishayataja, ambayo ni mageuzi katika uchumi, mageuzi katika kukuza viwanda vyetu na mageuzi katika kushirikisha sekta binafsi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaungana na wenzangu kwa suala ambalo wamelizungumza takribani Waheshimiwa Wabunge wote. Waheshimiwa Wabunge wote wameongelea kuhusiana na barabara na ninaanzia hapohapo; tuna Barabara ambayo inatajwa kwamba, inatokea Handeni kupitia Kiberashi – Chemba – Kwamtoro na hapo Singida, ambapo inagusa moja kwa moja Jimbo la Ikungi Mashariki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pale kwenye Jimbo la Ikungi Mashariki ni takribani kilometa 40 tu. Katika hizo kilometa 40, kama kweli tunataka kuwasaidia watu wetu, kuna kama kilometa 15 kutoka njia panda, kupitia Unyankhanya mpaka Siuyu na Makiungu. Pale Makiungu kuna hospitali kubwa ambayo mwekezaji huyo amejenga ile hospitali ambayo inahudumia watu kutoka mikoa mbalimbali, Simiyu, Manyara na mikoa ya jirani, lakini ni hospitali ya rufaa, ni hospitali kubwa sana ambapo, hata Serikali mle ndani tuna watumishi wetu ambao wanafanya kazi pale. Pamoja na yote ina upungufu wa watumishi upande wa Serikali, lakini ni hospitali kubwa ya Kitaifa, ambayo inatumika kusaidia hospitali hizi ambazo tunazijua za rufaa, kama Muhimbili, Benjamin, pamoja na Bugando.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hiki kipande cha kilometa 15, kama kitawekwa lami, kitasaidia sana kuepusha adha ambazo wanakutana nazo wagonjwa, hasa mama zetu, wanapokuwa pale hospitali, wanapofanyiwa operesheni, wanapojifungua na wanaporudi makwao kupitia hiyo barabara, ina rasta nyingi, yaani ina mashimo mengi makubwa hata inafika wakati ile mishono inafumuka. Hawa wagonjwa wanapata tabu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba hii barabara pamoja na kwamba ina urefu wa kilometa 340, hiki kipande cha takribani kilometa 15 kiangaliwe kwa jicho tofauti, kwa sababu huyu mwekezaji amewekeza pale na sisi tuna-promote PPP kwa maana ya ubia kati ya Serikali na sekta binafsi. Kama huyu amekwishawekeza hospitali kubwa pale tena ya rufaa inahudumia watu kutoka mbali, hiki kipande kifupi kuwasaidia hawa wagonjwa wasipate taabu ama wasidhurike na madhara yatokanayo na barabara, ninaomba sana katika hili liwekewe msisitizo mkubwa na hiki kipande cha kilometa 15 kiweze kujengwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii barabara Wabunge wote inapopitia wamekwishaitaja, Mbunge wa Kilindi juzi alitaja, Mbunge wa Chemba juzi alitaja, lakini Mbunge wa Kiteto naye pia aliitaja na mimi pia kwa kumalizia kwa sababu inaenda kuishia kwangu, ninaomba kama ikiwezekana wapatikane wakandarasi tofauti tofauti; wengine waanzie huko Handeni lakini wengine waanzie hapa Singida pale njia panda ili huduma iweze kupatikana kwa wepesi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakumbuka toka nipo darasa la nne mwaka 1997 huku, nyumba zilikwishawekwa X muda mrefu sana na kipindi hicho watu wakawa wanajua kuna matumaini makubwa ya kwamba hii barabara inaenda kuwekwa lami na watu wakawa wameshajiandaa kuhama. Bahati mbaya kwa sababu zile nyumba nyingi ni za tope kila mara ile X huwa inafutika na pengine watu wa sasa hivi wasijue kwamba zilishapigwa X. Zimeshapigwa X muda mrefu toka 1997 huko mwaka 2000, mwaka 2005, lakini bado haikujengwa kama ilivyokusudiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Rais tarehe Mosi Machi, 2025 akiwa Handeni aliitaja hii barabara, akaiagiza Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi wakae wamtafute huyu Mbia ili hii barabara iweze kujengwa. Sasa kama Rais anatoa maagizo, sisi watendaji huku hatuoni kwamba mfalme ameshasema na kauli ya mfalme huwa haipingwi na kauli ya mfalme huwa ndiyo final? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nilitegemea kwamba nione Wizara inakimbizina kuhakikisha kwamba hii barabara inajengwa mara moja kwa sababu ni agizo na ni kauli ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akiwa kule Handeni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kipindi hapa niliwahi kumshuhudia Mbunge mmoja, kipindi mimi sijaja Bungeni, huyo Mbunge aliwahi kupiga sarakasi hapa Bungeni, baada ya kupiga sarakasi muda siyo mrefu ile barabara yake ikajengwa. Sasa kwa sasa hivi tunaongea kwa upole kwa sababu tunaamini Serikali hii ni sikivu, inaenda kuhakikisha kwamba inasikiliza maombi ya Wabunge wote. Kwa hiyo, sina haja ya kupiga sarakasi kama yule alivyopiga kwa sababu ninaamini watakwenda kuijenga hii barabara ya lami. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumza kwa upole ila wakati utakuja tutazungumza kwa nguvu kubwa… (Makofi)
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante sana muda wako umeisha, naomba uunge mkono hoja.
MHE. THOMAS M. KITIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sana, kwa sababu kuna wakati mwingine tutapata nafasi ya kuzungumza na bado kuna Wizara nyingi, bado hoja ambazo ninazo nitazizungumza wakati huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)