Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Male
Party
ACT
Constituent
Tunduru Kaskazini
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
2
Ministries
nil
MHE. ADO S. ADO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru kwa kuniona, ili niweze kutoa mchango wangu katika Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Nina imani kwamba, kutokana na nafasi yetu tumekuwa tunapewa hapa uwiano wa kuchangia; kwa siku sisi ACT tumeambiwa, kwa nafasi yetu ya Waheshimiwa Wabunge tisa, tuna nafasi ya kuchangia angalau mchangiaji mmoja kwa siku, huwa tunapewa hivi kutoka Ofisi ya Katibu pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naona hizi ni dakika za jioni, isije ikahesabiwa dakika za jioni tukakatwa juu kwa juu tukashindwa kujipambanua. Ule msingi wa kwamba, nafasi yetu ya kuchangia mchangiaji mmoja izingatiwe, ili Bunge lipate kusikia mawazo yetu pia. Nimepata faida ya kuwasikia wachangiaji wenzangu, Waheshimiwa Wabunge na wengi wamejikita katika kuchambua hoja mbalimbali ambazo zipo katika Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, lakini mimi nitachukua njia tofauti nikitambua kwamba, Hotuba ya Waziri Mkuu katika Bunge la Bajeti siyo hotuba ya kawaida.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii siyo hotuba ya kisekta, hii siyo hotuba itayojikita kwenye maduhuli tu ya Serikali na namna ya kuyatumia. Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ndani yake inabeba tafakuri ya mwaka uliopita wa fedha. Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu inabeba maono ya Serikali katika mwaka ujao wa fedha kwa hiyo, mimi nitajielekeza katika maeneo ambayo kwa maoni yangu yamebeba ukimya mkubwa sana katika Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Yako maoni, yako maeneo, mimi ninaona yalipaswa kuwemo kwenye Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu au yalipaswa kupewa uzito wa kipekee.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaona hotuba hii imebeba ukimya katika maeneo hayo na kwa ajili ya muda nitayataja machache. Eneo la kwanza, nimesoma Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, Kurasa zote 122; sijaona kwenye ukurasa wowote, sijaona kwenye aya yoyote, sijaona kwenye sentensi yoyote, kuhusu Katiba Mpya, Tume Huru ya Uchaguzi na mageuzi ya kisiasa nchini kwetu. Hatua hii ya Hotuba ya Waziri Mkuu kukaa kimya juu ya jambo hili muhimu sana sisi tunaipa tafsiri kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hitimisho ninalolijenga mimi, mpaka nitapokuwa proved wrong wakati ujao, hii inanipa ishara kwamba, Serikali imeipuuza, hailipi uzito na haitaki ajenda ya Katiba Mpya, huo ndiyo msimamo wangu. Sasa ninatoa ujumbe kwa Serikali na Chama Cha Mapinduzi, ujumbe wa kwanza ni Watanzania si wajinga wanaelewa hali halisi ya kisiasa ya nchi yetu na wanajua bila Katiba Mpya, bila Tume ya Uchaguzi na bila mageuzi ya kisiasa ndani ya nchi yetu…
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.
MWENYEKITI: Mheshimiwa Ado, kuna Taarifa.
Mheshimiwa Ester Bulaya.
TAARIFA
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru tu kwa mchango wake, Mheshimiwa Ado, mdogo wangu na mimi nilikaa sana hapo. Ninaomba nimpe Taarifa kwamba, kwenye Ilani ya Chama Cha Mapinduzi chini ya Mwenyekiti, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, tumedhamiria ndani ya miaka hii mitano ya Awamu ya Sita Watanzania watapata Katiba Mpya. Ukimuangalia anavyozungumzia suala la Katiba Mpya amemaanisha, ndiyo maana kwenye ilani ya chama chetu tumeiweka. Ninaomba nimpe hiyo Taarifa.
MWENYEKITI: Mheshimiwa unaipokea Taarifa hii?
MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa nyingine.
MHE. ADO S. ADO: Mheshimiwa mwenyekiti, Taarifa ya Mheshimiwa Bulaya siipokei. Siipokei kupitia hoja yangu namba mbili, ambayo ninaelekea kuitaja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujumbe wangu kwa Serikali na Chama Cha Mapinduzi, ujumbe namba mbili, Katiba Mpya sio ajenda ya CCM, Katiba Mpya sio ajenda ya Serikali, Katiba Mpya ni ajenda na mali ya Watanzania. Ukimya huu katika Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu unamaanisha Serikali imeihodhi ajenda hii.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.
MWENYEKITI: Mheshimiwa Ado, kuna Taarifa. Mtoa Taarifa yuko wapi? Sawa, Naibu Waziri.
TAARIFA
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kumpa Taarifa Mheshimiwa Ado kwamba, Serikali iliyopo madarakani ni ya Chama Cha Mapinduzi na inatekeleza Ilani ya Chama Cha Mapinduzi kwa hiyo, hakuna namna utatofautisha Chama Cha Mapinduzi na Serikali iliyoko madarakani na Watanzania. Ahsante.
MWENYEKITI: Mheshimiwa Ado, unaipokea Taarifa hiyo?
MHE. ADO S. ADO: Mheshimiwa mwenyekiti, siipokei Taarifa hiyo. Sijasema Serikali ni mali ya nani, hilo ni somo lingine la Katiba, mkufunzi yuko pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema Katiba Mpya ni mali ya Watanzania. Watanzania wana haki kwenye hotuba kama hizi zinazobeba maono, kujua mchakato wao wa Katiba Mpya unakwenda wapi.
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.
MWENYEKITI: Inatoka wapi Taarifa. Ndiyo, Mheshimiwa Kihenzile.
TAARIFA
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ninakubaliana na Mheshimiwa mchangiaji kwamba, Katiba Mpya ni mali ya Watanzania, lakini pia ninamkumbusha mali za Watanzania ni pamoja na ardhi, fedha na vinginevyo. Kwa sasa mwenye mkataba wa kuvisimamia ni Serikali na Serikali ya sasa ni ya CCM kwa hiyo, huwezi kuvitenganisha.
MWENYEKITI: Mheshimiwa Ado unaipokea taarifa hiyo?
MHE. ADO S. ADO: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei taarifa hiyo. Kwa sababu ninaona nakwamishwa kwamishwa hapa, gari lina nasanasa niiache ajenda hiyo ujumbe umefika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ajenda ya pili ambayo ninaona ni ukimya kwenye hotuba ya Waziri Mkuu ni vita dhidi ya ufisadi, rushwa na ubadhirifu. Sijaona kama imepewa kishindo kinachostahili. Ninaamini Hayati Sokoine angefufuka leo wala nisingepata shida kujua ajenda yake namba moja ingekuwa ni ajenda gani. Ninafahamu... (Makofi)
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa, niko hapa taarifa.
MWENYEKITI: Taarifa.
TAARIFA
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kumpa taarifa Mheshimiwa Ado kwamba, unapozungumzia mtu ambaye tangu ameapa, tangu tumemdhibitisha kwenye Bunge hili kwa kinywa chake, kwa vitendo kuzungumzia masuala ya ufisadi na kukemea ubadhirifu na kukemea uzembe ni Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba. Kwenye hotuba yake Waziri Mkuu amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini yake yeye, kama Msimamizi Mkuu wa Serikali atahakikisha wazembe, wabadhirifu watachukuliwa hatua na wananchi wa Tanzania waweze kupata maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, inawezekana mdogo wangu leo alikuwa hajajiandaa kuchangia. (Makofi/Kicheko)
MWENYEKITI: Mheshimiwa Ado unaipokea taarifa hiyo?
MHE. ADO S. ADO: Siipokei taarifa hiyo. Mimi ninafahamu rejea ya uchambuzi, ni hotuba ya Waziri Mkuu. Ninaweza kumweleza Waziri Mkuu wapi amezungumzia juu ya rushwa na ufisadi. Alizungumzia ripoti ya CAG na commitment ya Serikali, kwa maoni yangu mimi, Waziri Mkuu hajatoa uzito unaostahili kwenye hotuba yake kwa ajenda ya rushwa na ufisadi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, uniruhusu nitoe mfano tu nimepigwa breki sana hapa.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.
MWENYEKITI: Mheshimiwa Ado kuna taarifa. Kanuni zetu zinaruhusu. Kuna taarifa ninaomba uipokee.
TAARIFA
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nimpe taarifa mzungumzaji rafiki yangu Mheshimiwa Ado, ninadhani atakuwa hajaisoma vizuri hotuba ya Waziri Mkuu. Ukisoma hotuba ya Waziri Mkuu kwenye eneo lote alilozungumzia utekelezaji wa shughuli za Serikali ameeleza kuhusu vita dhidi ya rushwa na ufisadi kwa ujumla, lakini ameeleza kwenye maeneo mahsusi.
Mheshimiwa Mwenyekiyi, Waziri Mkuu alipozungumza kuhusu ripoti ya CAG amesema, alipozungumza kuhusu kasi ya kuongeza ukusanyaji wa mapato amesema, kuhusu kuzuia kuvuja kwa mapato, hiyo ndiyo lugha ambayo Waziri Mkuu amesema (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba ya Waziri Mkuu ya masaa mawili lisaa limoja asingeweza kusema kila kitu, huwezi kumpangia aiseme kwa namna gani, lakini Waziri Mkuu ameisema na ujumbe umeenda nasi kama Wabunge tunatakiwa tuifanyie kazi hotuba ya Waziri Mkuu. Ninakushukuru. (Makofi)
MWENYEKITI: Mheshimiwa Ado ninakupa nafasi upokee taarifa hiyo na muda wako pia umekwisha.
MHE. ADO S. ADO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nitawaacha kwa tafakuri ndogo tu na ninaomba unitendee haki kwa dakika moja tu halafu mtaona kama mimi nilikuwa naelekea wapi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mazingira ya sasa ambayo tunapokea taarifa kwamba Serikali imeingia katika mtindo wa kuwa na makubaliano ya pembeni nje ya Mahakama za Kimataifa kuwalipa wanaotudai mabilioni ya fedha, mazingira ambayo yana harufu ya ufisadi, kwa mfano malipo ya bilioni zinazofikia 268 kwa Benki ya Standard Charter ambayo hiyo...
MWENYEKITI: Mheshimiwa Ado muda wako ulishaisha.
MHE. ADO S. ADO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kuhusu taarifa na muda, mimi ninavyoyaona mazingira ya ufisadi nchini sijaridhika na uzito ambao Waziri Mkuu ameuweka kwenye hotuba yake kwa ajenda ya ufisadi, mengine tutachangia kwa maandishi. (Makofi)