Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. Lucy Edward Mwakyembe

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. LUCY E. MWAKYEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante nami kwa kunipa nafasi ya kuongea tena katika Bunge lako hili Tukufu kwa ajili ya kuchangia hoja ambayo imewasilishwa na Waziri Mkuu ya makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka 2026/2027.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kwa upekee ninapenda nimpongeze Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutunukiwa shahada ya heshima ya udaktari ambayo imetoka katika Jimbo la Chuo Kikuu Nasarawa Nchini Nigeria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa uongozi wake thabiti; ambapo aliweza kuahidi kabla ya kuingia madarakani; kwamba atakapoingia madarakani ndani ya siku 100 ataweza kuyatekeleza mambo mengi. Mambo hayo ni pamoja na elimu, afya, mambo ya maji, na miundombinu. Pia tumeona kuwa hata kwa upande wa bima ya afya ameweza kuwafikia wananchi zaidi ya milioni moja na laki nne pamoja na kaya laki mbili na sabini na sita elfu na nne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende pia kumpongeza Mheshimiwa Rais ameweza kutoa ajira za walimu 7,000 na ajira 5,000 kupitia upande wa afya. Ameweza kuhakikisha kuwa analeta fursa ya vijana kwa kuanzisha Wizara ya Vijana na kuwamwagia mabilioni ya shilingi. Bilioni 200 ameziweka kwa ajili ya vijana ili kuweza kuongeza uchumi katika maisha yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda pia kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Emmanuel Nchimbi ambaye anamsaidia Mheshimiwa Rais katika kutekeleza majukumu yake. Tunaona kuwa amezindua mpango wa kitaifa wa pamoja kati ya waajiri, vyuo vya ufundi stadi pamoja na vyuo vikuu kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ukurasa wa tisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kumpongeza Dkt. Mwigulu Nchemba ambaye ni Waziri Mkuu pamoja na watendaji wote wanaomsaidia kazi, bila kumsahau Profesa Shemdoe ambaye yupo katika Wizara ya TAMISEMI, nami nikiwa mjumbe wa Wizara ya TAMISEMI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nichangie upande wa ajira kwa vijana. Tumeona lengo la Serikali kutaka kukuza ajira kwa vijana na wanafanya kazi kupitia ajira zilizo rasmi na zisizo rasmi, ajira za Serikali na za sekta binafsi. Kwenye upande huu ninaomba Serikali pamoja na sekta binafsi pale zinapotangaza fursa za ajira basi ninaomba kwanza tuangalie vijana wa kizalendo ambao wanajitoa kutumikia sekta hizo, sekta binafsi na sekta za Serikali bila kulipwa posho zozote, wameamua kwa uzalendo wao kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa inapotokea ajira kupitia sehemu hii, ninaomba sana nishauri Serikali waangalie vijana hawa, itafute namna ya kuwaingiza kwenye ajira. Idara ambazo wanazitumikia vijana hawa ni idara hizo hizo zinazoletwa katika kuhitaji wafanyakazi. Ni idara zile zile wanazozifanyia kazi lakini kitendo kinachokuja kujitokeza wakati kazi zinapotangazwa wanakuwa hawafai katika idara zile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninaomba sana Serikali iwasaidie vijana hawa wa Kitanzania ambao ni wazalendo katika kuwaingiza sehemu hizo za ajira. Pia, ninapenda kuipongeza zaidi Serikali; inaendelea kuzitoa fursa za ajira kwa vijana kwa asilimia nyingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nigusie kwenye 10% zinazokusanywa kwenye halmashauri kupeleka kwa vijana, watu wenye ulemavu pamoja na wanawake. Hapa mimi nitagusia kwa upande wa wanawake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona halmashauri nyingi zinajitahidi kutoa mikopo kwa ajili ya wanawake. Mama Samia Suluhu Hassan, Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, amehakikisha maisha ya wanawake yanakuwa mazuri. Mama amewatua wanawake ndoo kichwani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuwatua ndoo kichwani wanawake, Mama ameamua kuleta tabasamu kwenye familia, lakini kwa upande huu wa mikopo ambao halmashauri inatakiwa itoe kwa ajili ya wanawake, mikopo hii haiwafikii wanawake, tabasamu lile linaishia njiani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lile tabasamu ambalo Mama anataka kulipeleka kwa ajili ya Watanzania hawa linaishia njiani. Maisha ya familia yanakuwa ya kujikokota na tunajua mama ni nguzo muhimu naye kwa Taifa la sasa kwenye familia. Kwa hiyo, tunaomba Maafisa Maendeleo ya Jamii, wamebaki kukaa ofisini, hawawafuati wanawake, wakawapa elimu jinsi ya kuomba mikopo, jinsi ya kufanya biashara kutokana na hiyo mikopo, jinsi ya kutumia hizo pesa kwenda kwenye biashara ili ikuze biashara zao na jinsi ya kurudisha mikopo hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba sana Serikali na ninatoa ushauri, Maafisa Maendeleo ya Jamii, washuke, wasimame kutoka ofisini, wasibaki ndani ya ofisi. Kazi ya sasa ya Mheshimiwa Dkt. Samia anataka watu kuwafikia wananchi. Tumemwona Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba, amefika ndani ya mikoa na wilaya kuwasikiliza wananchi, kusikiliza kero za wananchi na Maafisa wa Maendeleo ya jamii, wanatakiwa wafike kwa wananchi, kwa wanawake hawa wa Kitanzania ili kuhakikisha wanawafikishia mikopo hii ambayo inatolewa na Serikali, lakini bila ya kuwasahau vijana na watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanatakiwa wakatoe elimu kule, wamejifungia na hapa ninaona ule utaratibu wa upimaji malengo ambayo ni PEPMIS inawahusu wafanyakazi ambao ni Maafisa wa Maendeleo ya Jamii, ambao wengine hawatoki katika idara zao kuwafuata wanawake. Tunaomba, tunaomba sana, wanawake hawa wafikishiwe tabasamu ambalo Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amewaahidi wanawake wa Kitanzania kuwafikishia ndani ya mwaka wa fedha 2026/2027. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba pia nigusie kwenye madeni ya watumishi. Ninajua sasa hivi Serikali inapitia changamoto kubwa, lakini kuna madeni ya watumishi ambayo yapo yanaonekana. Hapa niwapongeze sana baadhi ya halmashauri, wamehakikisha wanafuta madeni ya watumishi pamoja na madeni ya wazabuni. Wamepunguza madeni kwa asilimia kubwa sana madeni haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninaomba sana na lengo la Serikali ninajua kwenye bajeti yake hii imetenga fedha nyingi kwa ajili ya kupunguza madeni hayo. Mimi niiombe tena Serikali wasaidie mzigo ule kwa halmashauri kupunguza madeni yale, hususan madeni yasiyokuwa ya mishahara, yafutwe na ikiwezekana yasizalishwe tena au yazalishwe kwa uchache, kwa sababu, madeni yanafutwa, lakini yanaendelea kuzalishwa. (Makofi)


Mheshimiwa Mwenyekiti, yanazalishwa vipi? Katika kipindi ambacho watumishi wamepewa ajira ile hamahama ya watumishi, amefikishwa wilaya nyingine anataka kuhama kurudi wilaya nyingine; hii nayo inazalisha madeni ya watumishi. Kwa hiyo, ninaomba hapa kwa kuishauri Serikali iongeze nguvu ya kulipa madeni ya watumishi, lakini iongeze nguvu ya kulipa madeni ya wazabuni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa kunipa muda huu, nami ninaunga mkono hoja. (Makofi)