Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. Rashid Mohamed Mtima

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Newala Mjni

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. RASHID M. MTIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru wewe kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja hii ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Pia, ninamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kuwa mbele yako hapa na kutoa mawazo yangu kwa hoja hii, ambayo ipo mbele yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka nichangie katika maeneo kadhaa; moja, ni eneo la Wizara ya Kazi, Ajira na Mahusiano. Eneo hili kwanza ninachukua nafasi kumshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa anayoifanya katika sekta hii. Na-declare interest, mimi kwa miaka 10 nimekuwa Katibu wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali za Mitaa Tanzania, kwa hiyo, nimeona namna anavyowashika mkono wafanyakazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepitia taarifa hii, ninampongeza sana Mheshimiwa Rais katika eneo la kuendelea kujenga maisha ya wafanyakazi baada ya kustaafu kwa maana eneo la hifadhi ya jamii, Mheshimiwa Rais ametatua tatizo ambalo lilikuwa linafanya wafanyakazi wakose amani baada ya kumaliza kazi. Hapa nasema suala la Serikali hii ya Awamu ya Sita kuamua kulipa deni lile la pre-99 la michango ya watumishi ambao hawakuchangia huko mwanzo kabla ya kuanzisha Mfuko wa PSPF, ambao ilifika shilingi trilioni 4.7. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais alivyopewa tu kijiti hiki kwa mara ya kwanza alilipa shilingi trilioni 2.15 kwa non cash bond, lakini sasa hivi ukiangalia thamani ya Mfuko huu wa Utumishi wa Umma umefika shilingi trilioni 13.9 baada ya kumaliza deni hili la pre-99. Hili tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais, ninampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda tena kumpongeza Waziri Mkuu, ambaye Wizara hii ipo chini yake na Waziri wa Kazi, ndugu yangu Mheshimiwa Sangu, nimeona ameanza vizuri. Nimekaa kwenye sekta hii kwa miaka 10, kwa mara ya kwanza wakati bajeti hii inaandaliwa Waziri aliwaalika viongozi wote wa vyama vya wafanyakazi na kubadilishana nao mawazo na baadaye kushiriki katika kushuhudia bajeti hii wakati inasomwa. Hili ni jambo kubwa sana kwa maana limewaweka karibu wafanyakazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vyama vya wafanyakazi ni sehemu ya kuandaa mazingira bora ya wafanyakazi sehemu ya kazi na sisi kwa sababu, tumejishirikisha kwenye shirika la kazi duniani na mikataba tukaikubali, basi suala la kuhakikisha kwamba, tunakuwa karibu na tunasimamia vizuri vyama vya wafanyakazi ni suala ambalo ni la muhimu sana. Ninataka nishauri jambo kidogo hapa, kule kwenye vyama vya wafanyakazi yapo masuala hayaendi vizuri; huko mwanzo tunakumbuka tulikuwa na JUWATA, baadaye tukawa na OTTU, tukawa na TFTU, baadaye tukaenda vyama vya kisekta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tunaenda kwenye vyama vya kisekta, mfumo ulikuwa mzuri sana kwamba, kila chama kilipewa sekta maalum, lakini katikati hapa toka 1995 mpaka sasa Katiba za vyama zikabadilishwabadilishwa katika hatua ambayo sekta moja, chama kimoja, kikaenda kwenye sekta zingine. Kwa hiyo, kuna migogoro ambayo haitoi taswira nzuri ya hivi vyama kwenye kutenda kazi na kuwatumikia wanachama wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, badala ya kuwatumikia wanachama wao, basi wao wanagombana, kwa maana ya kugombania wanachama na hasa chama kinachoshughulikia Serikali za Mitaa na kile ambacho kinashughulikia Wafanyakazi wa Serikali kuu, wanagombania sana wafanyakazi wa sekta ya afya. Kwa hiyo, katika eneo hili ninashauri kwamba, ofisi hii au Wizara ione kwa namna gani inaweza ikaweka mipaka, ili vyama hivi vi-concentrate kwenye kuwahudumia wanachama badala ya kugombania wanachama. Huo ndio ulikuwa ushauri wangu kwenye sekta hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ni Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Hapa ninataka nioanishe ni kwa namna gani tunaendana na mipango yetu kwenda kule kwa wananchi. Kama tunakumbuka, tumechangia hapa Mpango wa Miaka mitano, tumepata taarifa au Hotuba ya Mheshimiwa Rais; hotuba yake ukiangalia kama kuna kitu cha mwisho cha ku-conclude, katika hotuba yake alisema ni tabasamu kwa Watanzania kwa miaka mitano hii, lakini ukisema miaka mitano hiyo, tutaenda kutoa tabasamu kwa nyenzo ipi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutaenda kutoa tabasamu kwa nyenzo ya Mpango wa Miaka Mitano, huu ambao nao tumeuzungumzia hapa. Tunapoelekea kwenye Mpango wa Miaka Mitano maana yake ni tunatekeleza kwa mpango wa mwaka mmoja hadi mwingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti hii ndiyo landing ground ya mipango yetu inayokuja, nikajiuliza nikisema tabasamu kwa Mtanzania ni maeneo yapi ambayo ukiweza ukifanya utawagusa, nikasema kama kuna maeneo ya msingi ya kwanza ni pale ambapo tunaenda kum-assure Mtanzania eneo lake la kujishughulisha katika maisha yake, huyu Mtanzania anafanya nini? Kama tutaenda kugusa pale tutamtengenezea tabasamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili, ni eneo la huduma, ustawi. Je, akitaka kumpeleka mtoto shuleni anapokelewaje? Anapata mazingira ya namna gani? Anapougua anapata mazingira yapi? Maeneo haya mawili tuki-capitalize tukaweka juhudi kubwa ndipo tutatengeneza tabasamu kwa Watanzania. Tabasamu hii tutaitengeneza kwa miaka mitano, huu ni mwaka wa kwanza tunataka tuanze, ninadhani ni eneo la kwanza ambalo tunatakiwa tuweke mazingira mazuri ya kwenda huko mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nikaangalia kwenye bajeti ya TAMISEMI nimeona maeneo mengi ambayo yamezungumza mafunzo katika level ya Mkoa na nini, lakini nikasema hapa na nishauri kidogo. Ushauri wangu ni kutengeneza eneo zuri la kuanzia kwenda kutengeneza tabasamu na tabasamu hili kule tukisema eneo la uzalishaji na eneo la ustawi wa jamii, walioko maeneo haya ni wafanyakazi wa Serikali za Mitaa, ni watu ambao wananchi wanafanya nao kazi moja kwa moja, sasa je, katika bajeti hii tumeliwekaje hilo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Serikali tunapelekaje kule kwenye Halmashauri namna ya kutekeleza mazingira mazuri kwa mwaka huu wa kwanza ili baada ya miaka mitano tuone tabasamu. Nilitamani kuona namna ya kwenda kuwajengea uwezo kule kwenye Serikali za Mitaa ili watafsiri haya mawazo ya mpango wa miaka mitano wa kuleta tabasamu kwa wananchi. Kwa hiyo, nilitamani kwenye bajeti hii tuone ni mikoa inaandaliwaje kwenda kuwawezesha Serikali za Mitaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukifika kwenye Serikali za Mitaa je, tunaandaje kutoka kwenye halmashauri yenyewe kwenda kwenye kata? Leo tuna Afisa Kilimo kule Mcholi chini kabisa Jimbo la Newala Mjini...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa, muda wako umekwisha.

MHE. RASHID M. MTIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kidogo. Ninatamani twende tukamwekee malengo ambayo yataenda kumgusa mwananchi ili aweze kupata tabasamu kwa kuzalisha korosho vizuri na akaona faida ya yeye kuwa na akampenda huyu mtumishi kuwa sehemu ya maisha yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)