Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

Hon. Salehe Mbwana Mhando

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilindi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027

MHE. SALEHE M. MHANDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru kwa kupata nafasi hii ya kuwa miongoni mwa wachangiaji wa Hotuba ya Makadirio ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Ninaomba kuanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa kibali kusimama katika Bunge lako Tukufu kuchangia hotuba hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaungana na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kutoa pongezi kwa viongozi wetu Wakuu wa Nchi yetu wakiongozwa na Jemedari wetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, sambamba na Mheshimiwa Makamu wa Rais na pia Mheshimiwa Waziri Mkuu wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, itoshe tu kusema, “Kusema sana si hoja, kutenda ndiyo hoja”, hii ndiyo dhima ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. Tunashuhudia namna siku 100 tu katika awamu hii ya pili ya kipindi chake cha pili anachomaliza, ahadi alizozitoa na utekelezaji wake huhitaji hata kutafuta kwa tochi. Unaona kwa vitendo na kwa matokeo na haya ndiyo ambayo Watanzania wanampenda na wanamtumainia sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sasa na mimi kujielekeza kwenye kuchangia hoja ya Hotuba ya Waziri Mkuu. Katika kuchangia hoja hii, mimi nimejipa muda mwingi sana wa kupitia Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, lakini ikiongozwa na dhima ile ya Dira ya Maendeleo ya Taifa letu ya 2050 ambayo Bunge hili na bajeti hii ambayo tunaanza kuijadili leo, inatuanzishia safari hiyo chini ya Mpango wa Nne wa 2026/2027 na 2030/2031 yenye maudhui yanayosema: “Mageuzi katika kukuza uchumi na kuzalisha ajira.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kutafsiri dhima hii ya mageuzi katika kukuza uchumi, moja kwa moja kwa mawazo yangu na kwa fikra zangu, nimeyatafsiri maono ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa miaka mitano iliyopita. Huu ni mwendelezo, kazi ilishaanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili, ninataka kufungamanisha, kwa mfano tu, mageuzi makubwa yaliyofanyika katika uwekezaji wa bandari zetu, Bandari ya Tanga, Bandari ya Dar es Salaam na Bandari ya Mtwara, tayari ni safari ambayo imeanzishwa katika kutekeleza Mpango huu wa Nne wa Dira ya Maendeleo wa 2050.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mageuzi yale yaliyofanywa ndiyo yanayokuja kuunganishwa na jambo linalozungumzwa na Waheshimiwa Wabunge wengi humu ndani. Mapinduzi makubwa ya bandari na mimi kama Mheshimiwa Mbunge ninayewakilisha wananchi wa Jimbo la Kilindi kutoka Mkoa wa Tanga na Tanga tuliguswa na uwekezaji mkubwa wa zaidi ya shilingi 400,000,000,000 kwenye uwekezaji wa Bandari ya Tanga ambayo sasa inatoa matokeo makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka kusema, kiunganishi kikubwa katika zoezi hili, hatua hii ni uwekezaji mkubwa kwenye miundombinu ya barabara. Pengine niseme tulichelewa, ilibidi wakati ule hatua ya uwekezaji kwenye bandari ilitakiwa iende sambamba na uwekezaji mkubwa kwenye barabara zetu hasa hizi za TANROADS.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuzungumzia Barabara ya kimkakati ambayo inaanzisha kuunganisha Bandari ya Tanga kutoka Tanga – Segera, Segera – Korogwe, Korogwe – Handeni na hatimaye kutoka Handeni – Kibirashi - Kiteto – Chemba – Kwa Mtoro, Singida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii korido ambayo ilikuwa inatakiwa ipokee makontena, mizigo kwa njia rahisi kabisa, ilitakiwa iwe hii Barabara ya lami ambayo kipande chake kilichobaki ni kutoka Handeni – Kibirashi – Kiteto – Chemba – Kwa Mtoro. Ninamshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa ziara aliyofanya katika Jimbo letu la Kilindi na akajionea kwa macho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan alishaanzisha kwa maono hayo akiwa anaangalia uwekezaji mkubwa wa bandari, akaanzisha ujenzi wa Barabara kwa kiwango cha lami kutoka Handeni – Kibirashi – Chemba na akaanza na kilometa 20 mwaka 2023 kutoka Handeni – Mafuleta, hatimaye akaagiza tena zijengwe kilometa 30 kutoka pale Mafuleta kwenda Kileguru kilometa 30, jumla ni kilometa 50.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana Serikali, twende tukatekeleze maono haya ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. Tumechelewa, hivi tunavyozungumza, katika zile kilometa 20, kilometa 10 tu zimekamilika kwa miaka minne. Ninaomba sana, katika kutafsiri mageuzi katika kukuza uchumi, barabara hii ni ya muhimu, ni ya kimkakati na katika bajeti hii inayoanza katika kutekeleza Dira ya 2050 na huu Mpango wa Nne wa dira hii. Hii barabara iwe kipaumbele katika mipango yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii inaondoa sasa hivi mizigo inayoshuka Bandari ya Tanga inalazimika tena kurudishwa Dar es Salaam kwenye mizigo mingi inayopokelewa kwenye Bandari ya Dar es Salaam. Huu ni mgogoro, lakini njia rahisi ambayo ilikuwa tungekuwa tumeanza mapema na sasa hivi hatujachelewa, tukiamua tunaweza tukaenda kwa speed, tukaitoa Barabara ile mpaka Kibirashi, Kibirashi ikaendelea kwenda Kiteto, Kiteto kwenda Chemba kule Kwa Mtoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba pale Singida ianzishwe Bandari ya Kwala namba mbili, ipokee mizigo pale iingie kwenye SGR, iendelee na safari kwenda mikoa mbalimbali na nje ya nchi kule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na barabara hii kwa kiwango cha lami kwa Wanakilindi bado tuna uhitaji na hii wilaya ina changamoto kubwa sana za barabara hizi hizi za TANROADS kutoka pale Songe kwenda Gairo, lakini kutoka Songe kwenda kwa Lugulu, barabara hizi hazipitiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nitoe ushauri twende na mipango na kazi zinazotoa matokeo, tutoke sasa kwenye barabara kujengwa kwa kiwango cha tope, tuwe na mpango madhubuti wa kila mwaka kwamba hizi barabara zifanyiwe matengenezo kwa kiwango cha moram au changarawe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua inayoendelea sasa hivi ya surface grading unaondoa hata ile changarawe ya mwaka juzi, mwaka jana unaleta tope, unajaza mvua inakuja tunarudi palepale, fedha za umma zinapotea na matokeo hayaonekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninatamani nione tuje na mpango kwa TANROADS tuseme sasa matengenezo ya kawaida yawe kwa kiwango cha changarawe, tuone ma-tipper yanamwaga changarawe kipindi ambacho tunatengeneza barabara ili ziweze kupitika mwaka mzima, lakini huu mpango wa surface grading tunapoteza fedha, hakuna matokeo na mwisho wa siku tunazorotesha uchumi wa wananchi wetu na uchumi wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la TARURA, Jimbo la Kilindi lina mtandao wa barabara za TARURA kilometa 1,520. Bajeti ya TARURA bilioni 2.5, jiografia ya Kilindi ni ya milima na makorongo mapana. Mimi nina madaraja nane, Daraja la Lukole, Tamota, Sambu unakwenda pale Gombero, unakwenda kule Saunyi, unakuja hapa Vunila, barabara moja limefanyiwa usanifu ni bilioni 4.3 wastani, unapokea bilioni 2.5!

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tunavyozungumza kata nne zimejifunga hazifikiki; Kata za Kilwa, Lwande, Hagwi, Saunyi na changamoto yake ni madaraja. Sasa niulize kwa bajeti ya bilioni 2.5 hiki kitendawili kinakwenda kuteguliwa vipi? Kwa hiyo, ninaunga na Wabunge wenzangu wote, tuhakikishe kwamba TARURA inaongezewa na bajeti na tufanye zoezi, sasa hivi tunakwenda ku-phase out REA, ule mpango wa REA na usimamizi wake urudi kwenye barabara za TARURA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa eneo la barabara ninaomba niishie hapo, ninaomba sana tuchukue juhudi na tuamue, kupanga ni kuchagua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ninaomba niingie kuhusu migogoro ya ardhi ya wakulima na wafugaji. Ukurasa wa 27 umeeleza vizuri sana. Hili ninataka niwaambie miongoni mwa Wilaya zenye changamoto kubwa na Kilindi imo, lazima tukubali tatizo na ili uweze kutatua tatizo ni lazima utambue kwamba nina tatizo na hili tatizo ninaamini ni la nchi nzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa leo ninataka niwaambie Waheshimiwa Wabunge wenzangu na Mwenyekiti wa Bunge na Serikali, migogoro ya wakulima na wafugaji, lipo tatizo la msingi, lakini tu hatutaki kuli-address. Wapo wafugaji wakorofi wachache ambao wao wanaleta matatizo kwa ukorofi wao, lakini hiyo siyo hoja ya msingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya msingi ni kwamba sisi tuna mifugo, tuna watu wanaojishughulisha na shughuli za ufugaji, hizi ni shughuli za kiuchumi lakini hakuna sehemu za malisho. Wote tunatoka kijijini hapa, asimame mtu aseme mifugo yetu kwenye kijiji chetu inalishiwa sehemu fulani, asimame hakuna. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu zinaonyesha hapa tuna mifugo milioni 76, mifugo maeneo rasmi ya malisho hayapo nini kinatokea? Mifugo inahudumiwa kwenye maeneo yenye matumizi mengine kama ya kilimo hifadhi na kadhalika. Sasa utakwepaje migogoro hiyo kama hali ndivyo ilivyo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niiombe Serikali hili jambo ni kubwa, ni mtambuka, linahitaji kukaliwa chini kufanya tafakari. Leo hata kule kwenye matumizi yaliyotengwa matumizi bora ya ardhi, kwenye maandishi utaona kumetengwa maeneo ya mifugo, kwenye uhalisia kule hakuna huo ndiyo ukweli. Kwa hiyo, lazima tukakae tutafute ufumbuzi wa eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii ukienda kwa Afisa Mifugo atakupa takwimu ya mifugo na ni kweli kwenye kata hiyo mifugo ndiyo hiyo, ukienda atakupa idadi ya majosho na ukienda utayaona, ukienda atakupa idadi ya minada na ukienda utaiona, nenda kamwambie nipeleke kwenye malisho ya mifugo, hutapata jibu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Salehe…

MHE. SALEHE M. MHANDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nitoe wito au nitoe ushauri kwa Serikali, Wizara husika TAMISEMI, Ardhi, Mifugo tukae tutafakari huu uchumi, lazima hii shughuli iwe na maeneo rasmi ya kufanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuunga mkono hoja na ninashukuru sana. (Makofi)