Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Ilemela
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
1
Ministries
nil
MHE. KAFITI W. KAFITI: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba nichukue nafasi hii kuchangia hotuba muhimu ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Kwanza kabisa, ninampongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kusimamia Dira yetu ya 2050 katika kuhakikisha wanakuza uchumi na kuzalisha ajira nyingi nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninampongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba yake nzuri na vilevile kwa ziara yake ambayo ameendelea kuifanya katika mikoa mbalimbali ambayo imeleta tabasamu kubwa kwa wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati huo huo, kupitia ziara zake, ninapenda kutoa rai kwa watendaji walioko maeneo ambayo Mheshimiwa Waziri Mkuu amepita, basi wasisubiri kwanza Waziri Mkuu aje ndiyo wananchi waweze kusikilizwa kero zao. Kwa hiyo, ninaomba sana waendelee kuwasikiliza wananchi, ili waendelee kupata tabasamu ambalo ameahidi Mheshimiwa Rais.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninachukua tena fursa hii kuwapongeza Mawaziri wote wa Wizara hii kwa kazi nzuri wanayoifanya, Mheshimiwa Deus Sangu na Mheshimiwa kaka yangu Mheshimiwa Profesa Shemdoe, kwa kazi nzuri wanayoifanya. Ninaomba nichangie hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu katika maeneo mbalimbali, hasa nitajikita katika maeneo mawili, lakini kubwa nitaongelea zaidi katika eneo la ajira.
Mheshimiwa Naibu Spika, ikumbukwe kwamba, Mkoa wa Mwanza ni miongoni mwa mikoa ambayo ina makusanyo makubwa na inachangia kwa kiwango kikubwa kwenye pato la Taifa. Zaidi ya asilimia 7.2 ya pato la Taifa yanachangiwa na Mkoa wa Mwanza, nyuma ya Dar es Salaam. Kwa maana hiyo, Mkoa wa Mwanza, pamoja na kuwa ni mkoa wa kimkakati na sisi kama Wabunge, tunalo jukumu la kuhakikisha tunaendeleza yale mazuri ambayo Mheshimiwa Rais ametaka kuyafanya katika Mkoa wa Mwanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, Wilaya ya Ilemela, ambayo mimi ndiye Mbunge wa jimbo hilo, ni wilaya ya kimkakati. Ukiangalia katika Mkoa wa Mwanza ni wilaya ya pili ambayo inaongoza kwa makusanyo. Wilaya yetu ya Ilemela ukiangalia miundombinu yake ya barabara kiukweli inasikitisha na tunatakiwa tupewe kipaumbele kikubwa na Mkoa wa Mwanza kwa sababu, ndiyo hub ya kiuchumi ya Ukanda wa Maziwa Makuu. Tunaomba sana Serikali iendelee kuweka jicho la pili kuhakikisha tunarekebisha sana miundombinu yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaipongeza sana Serikali kwa kuendelea kuboresha miundombinu ambapo tumesikia Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba sasa TARURA wanakwenda kuongezewa fedha na sisi tunaamini, kama wawakilishi wa wananchi, tutaendelea kusimamia na kuhakikisha miundombinu hii inarekebishwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, kwa sasa hivi barabara nyingi, hasa za Jimbo langu la Ilemela, zimekuwa ni changamoto kubwa. Barabara zimeharibiwa na mvua, tunafahamu pamoja na kuwa mvua ni baraka, lakini barabara nyingi zimeharibika. Kwa hiyo, ninaomba sana ndugu zangu wa TARURA kuangalia barabara za wakazi wangu wa Jimbo la Ilemela na wananchi wote kwa ujumla, kuhakikisha barabara hizi ziweze kupitika.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo ninaomba niongelee Barabara yangu ya Ilemela ya kimkakati, Serikali naomba iiangalie kwa jicho la pili. Barabara hii ya Airport – Kayenze ni muhimu sana na kiungo kwa Wilaya hii ya Ilemela. Barabara hii endapo itafunguka, itahamasisha maeneo makubwa ya kiuchumi, hasa kwa wavuvi wanaopatikana Mkoa wa Mwanza na Wilaya ya Ilemela.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba niongelee eneo la miundombinu ya uwekezaji wa viwanda. Tunafahamu kwamba, nchi hii imekuwa mstari wa mbele kuhakikisha ina-promote uanzishwaji wa viwanda vingi. Kwa hiyo, naendelea kuipongeza sana Serikali na ndugu zetu wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii wakiwemo NSSF, PSSSF pamoja na WCF kwa kuwa, mstari wa mbele kuhakikisha kwamba, wanaunga mkono juhudi ya Serikali kuhakikisha wanaimarisha uanzishwaji wa viwanda.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia mfano, NSSF, Kiwanda chetu cha Mkulazi zaidi ya wananchi 10,000 wameajiriwa pale. Zaidi ya tani 50,000 zimeendelea kuzalishwa pale. Kwa hiyo, ninaiomba Serikali iendelee kutumia Mifuko hii kwa sababu, imeonesha kufanya vizuri. Hata watu wa PSSSF, ukiangalia Kiwanda cha Kilimanjaro Leather kinafanya vizuri katika utengenezaji wa viatu, lakini vilevile katika eneo hilo hilo bado tuendelee kuiomba Serikali iendelee kushika Mifuko hii, ili iendelee kufanya vizuri kwa sababu, mifuko hii ndiyo inasimamia maslahi ya wazee wetu ambao wanastaafu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo hilo hilo, ninaomba nielezee yafuatayo kwa sababu, mifuko hii imekuwa ikileta tija katika jamii yetu. Mifuko hii imekuwa ikiongeza chachu ya uwekezaji katika maeneo mbalimbali, basi tuiombe Serikali kwa madeni ambayo Mifuko hii inadai, iweze kuyamaliza na kuongeza mafao kwa wastaafu wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo hilo hilo ninaiomba sasa Serikali, kama itaridhia, Daraja la Kigamboni tunafahamu uwekezaji mkubwa umefanyika pale. Basi ni jukumu la Serikali iweze kulipa fedha zile pale na lile daraja liweze kurudi Serikalini na baadaye wananchi wa eneo hilo waweze kupita bila kuwa na kipingamizi cha aina yoyote.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni uwekezaji. Pamoja na mazingira mazuri ambayo Serikali imeyaweka kuhakikisha kwamba inalinda maeneo ya uwekezaji na wananchi kujikwamua kiuchumi, napenda kuipongeza sana TISEZA kwa juhudi inazofanya katika kuhakikisha maeneo mbalimbali yanapatikana, kwa ajili ya uwekezaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia Halmashauri nyingi na Waheshimiwa Wabunge watakuwa ni mashahidi hapa, asilimia nyingi zina maeneo mengi ya kuwekeza, lakini hazina uwezo wa kulipa maeneo hayo ya kimkakati, kwa ajili ya uwekezaji. Sasa ninaiomba Serikali, kupitia TISEZA, itafute yale maeneo strategic ambayo TISEZA inaweza ikalipa fidia kwa niaba ya Halmashauri, ili wawekezaji wanapokuja waweze kuwekeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya yangu ya Ilemela tuna maeneo mazuri ya uwekezaji. Kulingana na uwezo wa manispaa yangu, haiwezi kulipa hizo fidia kwa ajili ya wakazi hao kuyaachia, kwa ajili ya uwekezaji. Kwa hiyo, ninaiomba sana Serikali, kupitia TISEZA, itakuwa ni vizuri yale maeneo yote ambayo ni strategic, kwa ajili ya uwekezaji tuweze kuwatumia wadau hawa, ili waweze kuimarisha ajira na uanzishwaji wa viwanda vingi.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninachukua nafasi hii kuliongelea kundi ambalo nasema nitakuwa mchoyo wa fadhila nisipowaongelea ndugu zangu wa bodaboda pamoja na bajaji. Mimi nikiwa kama Rais wa Bodaboda na Bajaji Mkoa wa Mwanza, ninalo jukumu la kuhakikisha kwamba, tunawajengea uwezo na kuwatetea, ili nao waweze kujikwamua kiuchumi.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu vijana wengi wamejiajiri na ni kundi kubwa. Ukiangalia katika wilaya yangu tu, ni zaidi ya vijana 12,000 wamejiajiri katika eneo hili. Kwa hiyo, ni wakati sasa kuiomba Serikali, kundi hili nalo tuweze kulirasimisha wawe Maafisa Usafirishaji kamili.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba vilevile kusema kitu kimoja, katika eneo hili vijana wengi wanataka kujiajiri, lakini gharama za leseni kwao zimekuwa ni kero kubwa kwa vijana wetu. Watu wanataka kuendesha pikipiki hizi, lakini wanakosa uwezo wa kulipia hizo leseni. Ninaiomba Serikali hii sikivu ya Chama cha Mapinduzi katika eneo hili waweze kuangalia.
Mheshimiwa Naibu Spika, miaka miwili iliyopita, yalitolewa mapendekezo kwamba leseni iweze kushuka kutoka shilingi 70,000/= mpaka shilingi 30,000/=. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri Mkuu naomba sana, katika kundi hili la vijana ambao wengi wako huku na mimi siku zote nimekuwa nikihimiza kundi hili kwa sababu, ni kubwa ni lazima sasa, kama Serikali, tuwatoe sehemu moja kuwapeleka sehemu nyingine, ili waweze kujikwamua kiuchumi. Kwa hiyo, tuna mengi ambayo tunahitaji kuongea hapa.
Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, ninaomba sana Mfuko huu wa PSSSF uliwekeza katika eneo la Msamvu pale, ile Msamvu Bus Stand, ambalo kila mmoja tunapafahamu. Lile eneo limejengwa kwa fedha za wastaafu. Kwa hiyo, ninaiomba sana Serikali itoe fidia kwa Mfuko huu wa PSSSF, ilipe lile eneo ili liweze kuachiwa katika Halmashauri ile ya Morogoro na PSSSF iendelee na mikakati yake ya uwekezaji maeneo mengine, ili kuweza kulinda mafao ya wastaafu hawa.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa, ninaomba niongelee eneo la vijana, hasa katika eneo la kilimo. Tunafahamu nchi hii kilimo ndiyo uti wa mgongo, kwa hiyo, vijana wengi tunahitaji wajiajiri hapa. Kwa hiyo, katika eneo hilo ninaiomba sana Serikali tuendelee ku-promote, ili vijana wengi waweze kuingia hapa na kufanya uzalishaji unaotokana na maendeleo ya nchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kuwasilisha na ninaunga mkono hoja. (Makofi)