Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Sex
Female
Party
CCM
Constituent
Momba
Contributions
nil
Answers
nil
Commettees
0
Ministries
nil
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru kwa nafasi. Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo jipya la Uyole ujaye nakushukuru sana kwa nafasi. Pia, tuliona uliwauliza Wanauyole pale, wamekwishakuchagua tumeona kabisa hadharani. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ninaomba nitumie nafasi hii kwanza kabisa, nimemsikia Mheshimiwa Waziri akisoma hotuba yake na akisema mafanikio makubwa sana ya kimbunga cha Tsunami. Nami kwa mafanikio hayo hayo ambayo yamefanywa na Serikali yangu ya Chama Cha Mapinduzi ambayo inaongozwa na mwanamke jemedari na mahiri sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Mheshimiwa Spika, ninaomba nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu pamoja na Serikali yake yote kwa ujumla ya chama chetu, kwa kuendelea kuwekeza sana kwenye afya ya Watanzania ambapo tukiamini kwamba afya ndiyo msingi wa mafanikio yote. Mtu anaweza asiende shule, lakini akiwa na afya anaweza akatafuta njia mbadala ya kuweza kuishi. Kwa hiyo, tunashukuru sana kwa uwekezaji mkubwa sana kwa ajili ya ustawi mkubwa wa Watanzania. Ahsante sana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, tumpongeze pia Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri ambayo unafanya na kipekee hapa Mheshimiwa Waziri ninaomba nikushukuru sana. Tunashukuru sana kwa ile ambulance aliyotupatia Kituo cha Afya Kapele. Sisi Wanakapele na Wanamomba tunashukuru mno na tunaamini kwa kushirikiana na Wizara ya TAMISEMI wataweza kutusaidia kupata ambulance kwenye hospitali ya wilaya pale Chitete pamoja na ambulance kwenye Kituo cha Afya Mkulwe. Shangazi katika hilo tunakutegemea sana utaongea na pacha wako. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kipekee sana ninaomba nimpongeze Naibu Waziri wake. Mheshimiwa Dkt. Mollel ni mtu muungwana ambaye kwa kweli ana mazuri yake. Nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. Mollel. Kwa kweli amekuwa ni daktari. Tunapompigia simu hata usiku wa manane tunapokwama na wagonjwa wetu kwenye hospitali za mikoa, amekuwa ni mtu mwenye msaada, anapokea. Amewasaidia Wabunge wengi sana. Kwa kweli katika wema huu ambao amewatendea watu, Mwenyezi Mungu azikumbuke na kuzitakabali hizo sadaka zake, amkumbuke Naibu Waziri Dkt. Mollel, aendelee kupokea simu hivyo kwa sababu unapomsaidia mgonjwa yule ni mhitaji, umekuwa umemkopesha Mwenyezi Mungu. Mungu ambariki sana na aendelee hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, pongezi hizi tunaomba tushauri mambo kadhaa kwenye eneo hili. Tunatambua kwamba wako kwenye mkakati wa namna gani tulete huduma ya afya kwa wote, kwenye Bima ya Afya kwa wote, lakini tuombe, kwa kuwa afya haiwezi kusubiri, wananchi wa Tanzania wameamua kuwasubirisha ili mambo yakamilike, lakini kuna mtu mwingine ameumwa leo, yawezekana Mwenyezi Mungu alikuwa amempa siku saba tu za ku-survive kwenye huo ugonjwa. Sasa na kama jambo hili litakamilika miezi mitatu ijayo au mwaka mzima ujao, mtu huyo anaendeleaje kupata huduma? Mtu huyo anaendeleaje kusaidika?
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunaomba, wakati michakato yote inaendelea na maboresho mengine kwenye Bima ya Afya yanaendelea, tunaomba vile vifurushi walivyovitoa vya Watanzania kupata huduma ambao wako kwenye Bima ya Afya ya NHIF tunaomba virudishwe, virejeshwe kwa sababu, siyo Watanzania wote ambao wana uwezo na Watanzania wengi kwa ujumla matibabu yamekuwa ni changamoto kubwa sana. Kwa hiyo, tunaomba hivi vifurushi virejeshwe kama ilivyokuwa hapo awali. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, hata mtu anapoenda kupima umeme kwenye moyo ana bima, lakini inabidi tena aongeze pesa nyingine aweze kurejesha. Mtu alijinyima akakata bima na familia yake ili iweze kumsaidia. Kwa hiyo tunaomba na nimekuwa nikiongea hapa na nimeuliza swali la nyongeza, vifurushi hivyo ambavyo wameviengua viweze kurejeshwa.
Mheshimiwa Spika, mafanikio makubwa ambayo yameweza kutajwa hapa; kuongeza majengo, kuongeza vifaa tiba, kuongeza na mambo mbalimbali, viko baadhi ya vifaa hapa Mheshimiwa Waziri amevitaja kwamba Tanzania ndiyo nchi peke yake ambayo tuna hivyo vifaa (tunaongoza kwenye baadhi ya hizo nchi ambazo zinamiliki hivyo vifaatiba).
Mheshimiwa Spika, sasa, sisi tuwaombe. Wapo vijana wenzetu wa Kitanzania ambao wamesoma vizuri na wamemaliza masomo ya udaktari. Tunaomba katika ile changamoto ya kupungukiwa na watumishi, tunaomba vijana hawa waajiriwe kwa wingi ili tunatamani kwa kuwa vifaa vile vimeweza kuongezeka, matibabu yaweze kufanyika masaa 24. Kwa sababu, kuongezeka kwa vifaa hivi pia hatuwaombei Watanzania waumwe, lakini tunaamini na nchi za jirani ambao watakuja kutibiwa kwenye nchi yetu tutumie kama chanzo cha mapato.
Mheshimiwa Spika, sasa, ninashauri, watu wakienda kutibiwa usiku kunakuwa tu kuna lile dirisha la Emergency. Baadhi ya kliniki zinafungwa, ni mpaka pawe asubuhi. Kama tumeongeza majengo, kama tumeweza kuongeza vifaa, tuwaajiri na vijana wa Kitanzania ambao hawajaajiriwa na wamesoma na wengine wamesoma kwa kutumia kodi za Watanzania walipewa mkopo, waingie kwenye ajira rasmi hospitali zetu ziweze kufanya masaa 24, ili hata watu wengine ambao wanatoka huko nje waje watibiwe tuendelee kujiongezea kipato. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, Watanzania wakija kutibiwa wenyewe asubuhi, sawa, lakini mtu mwingine akija akifika labda na basi saa 12, whether ametoka, Kenya ametoka Malawi, apate huduma atibiwe ili asubuhi aweze kurudi kwao.
Mheshimiwa Spika, tusitegemee dirisha la Emergency peke yake katika kutoa huduma, kwa sababu kliniki zingine zinafungwa kwamba daktari mpaka siku fulani na wakati mwingine hata wagonjwa kupangiwa ratiba, kwamba kuna daktari bingwa aje aonwe baada ya wiki mbili. Kama Mungu alimpa siku sita za huyu mtu kuweza kuishi, kwa hiyo mtu huyu ataweza kwenda kuondoka japokuwa Mwenyezi Mungu hapangiwi katika hili. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, pamoja na mafanikio makubwa ambayo tunayataja, yako baadhi ya magonjwa hapa nchini kwetu ambayo kwa kweli yamekuwa tishio. Katika hili pia tunaomba Serikali iendelee kuweka msamaha kwa sababu magonjwa haya yameonekana kuendelea kuchukua watu sana.
Mheshimiwa Spika, mwezi ulioisha tu mwezi Mei Jimboni kwetu Momba watu ambao wamekufa kwa kukosa matibabu ya kufanya dialysis ya figo, ni zaidi ya watu nane, unapokea na ndiyo hizo simu zingine ambazo tumekuwa tunampigia Mheshimiwa Dkt. Mollel.
Mheshimiwa Spika, sasa tutapigia watu wangapi? Ni watu wangapi ambao hawawezi wakamfikia Mbunge? Ni watu wangapi ambao hawawezi kuwapigia Wabunge wengine waweze kusaidika?
Mheshimiwa Spika, tunaomba matibabu, kwenye kufanya dialysis kwenye figo, aidha yawekewe msamaha au yapunguzwe gharama, ni kubwa. Watanzania wengi hawawezi kumudu hayo matibabu halafu ni consecutively; wiki hii uweze kufanya, uweze kusafishwa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, mtu anatoka Momba anaambiwa akafanye dialysis rufaa. Kutoka Sanja tu kufika Mlowo nauli ni karibu shilingi 20,000; utoke Mlowo uende Mbeya, hakuna Watanzania ambao wanaweza.
Mheshimiwa Spika, kama ambavyo tumefanya msamaha kwenye baadhi ya magonjwa tukatafuta, whatever, wahisani sijui kwenye TB, kwenye HIV, watu wanapata matibabu bure, tunaomba na kwenye figo iwe hivyo hivyo. Watanzania wengi wanakufa, kwa ajili ya kukosa matibabu ya kusafisha figo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, katika hili tunaomba sana. Miongoni mwa vitu ambavyo Waziri avipe kipaumbele kwenye bajeti yake, Mheshimiwa Waziri, kipaumbele kiwe ni kusafisha figo. Iwe bure kabisa na elimu kuenea namna ambavyo watu tuendelee kutunza figo zetu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ugonjwa mwingine ambao tunaomba pia, tupate msamaha ni saratani. Kufanya hizo chemo, mionzi, kwa kweli, ni gharama sana. Watanzania wengi wanakufa, kwa ajili ya kwenda kufanya mionzi kwenye cancer. Licha ya kwamba, kuna Watanzania ambao hawana uwezo wa kufika huko India na maeneo mengineyo, lakini kufika tu hapo Ocean Road, mimi ninatolea mfano kwa sababu, ninatoka jimbo la kijijini na ni mbali sana; anafika hapo mtu hana ndugu Dar es Salaam, amechukua muuguzi akaendelee kumuuguza, wamepangiwa leo ufanye, baada ya wiki moja, baada ya wiki moja; matibabu yenyewe ni gharama. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, basi tuombe watu wajitafutie nauli ya kufika huko Ocean Road, wajitafutie gharama kidogo namna ya kula, kama watachangiwa na ndugu, lakini matibabu haya yapunguzwe, kwa ajili ya kuwasaidia Watanzania. Kama tumewekeza miundombinu yote hii, tumeweka vifaa tiba vyote hivi, tunamaanisha kwamba, Mheshimiwa Rais wetu nia yake ni kuokoa maisha ya Watanzania wengi. Wakati mwingine hata mtu akiambiwa tu ana kansa, labda kansa ya uzazi, ameambiwa tu pale Meta, anaishia hapo hapo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nauli tu ya kufika Dar es Salaam, vipimo hivyo atakavyoenda kutajiwa, namna ya kumwona daktari, mpaka amalize hiyo tiba miezi mitano, zote hizo ni pesa na ndiyo vifurushi hivyo vingine wamevitoa kwenye bima. Kwa kweli, tunaomba haya magojwa mawili, figo na saratani, waweke msamaha Watanzania watibiwe bure kwa sababu, ni magonjwa ambayo yanaua watu na watu hawana uwezo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ninaomba sana hili lichukuliwe kuwa ni kipaumbele. Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha hapa, tunaomba atoe matumaini, ili wale wagonjwa ambao wako Ocean Road saa hizi wasikie kabisa kwamba, Wizara ya Afya imekusudia kuwasaidia, kwa ajili ya jambo fulani. Pia, hawa ambao wanafanya dialysis wanasubiri, wamepangiwa tarehe, wasikate tamaa, yaani mtu akitajiwa pesa tu anakata tamaa anaenda kufa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kama ambavyo tulifanya jitihada kwenye TB, kwenye UKIMWI, watu wakaanza kuishi kwa matumaini na wanaishi na virusi. Watu wanasomesha watoto wanakufa uzee, tunaomba na kwenye haya magonjwa yasiyoambukiza tuweze kuyachukua kwa umuhimu wake, ili tusipange foleni kuendelea kuwapigia Mawaziri, kwa ajili ya kuomba msamaha. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, ninakushukuru sana. (Makofi)