Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026

Hon. Charles Muguta Kajege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mwibara

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026

MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika hoja hii ya Hotuba ya Waziri Mkuu. Kwanza nichukue fursa hii kumpongeza Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini vilevile nataka niwapongeze Waziri Mkuu Kassim Majaliwa na Naibu Waziri Mkuu, Mheshimiwa Dkt. Doto Biteko kwa kazi nzuri ambayo wameifanya. Hawa wamekuwa ni kiunganishi kizuri sana kati yetu na Serikali na hakika hakuna hata siku moja ambayo nimekwenda kuwaona, na wakashindwa kunisaidia katika kutatua changamoto yangu. Nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali yetu imefanya kazi kubwa sana katika kipindi cha hii miaka minne. Miradi mingi imetekelezwa. Sasa nitaigawa katika maeneo mawili, kwanza Kitaifa na lingine katika jimbo langu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa kwanza ni wa Bandari ya Dar es Salaam. Baada ya DP kupewa hii Bandari ya Dar es Salaam imekuwa na mafanikio makubwa. Katika kipindi cha kuanzia Julai mwaka 2024 mpaka Machi mwaka huu, jumla ya makasha 686,515 yameingia, ukilinganisha na makasha 670,724 katika kipindi hicho hicho katika mwaka uliopita.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile mapato yameongezeka kutoka shilingi bilioni 850 hadi kufikia shilingi trilioni moja. Vilevile muda wa meli kutia nanga kusubiri kuingia bandarini umepungua kutoka siku 30 hadi kufikia siku tatu. Hii ni improvement kubwa sana katika upande wa bandari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi mwingine ni Mradi wa Umeme wa Julius Nyerere ambao thamani yake ni shilingi trilioni 6.6. Mpaka kufikia Machi mwaka huu, jumla ya megawati 2,115 zimeingia katika Gridi ya Taifa na huu umeme umeweza kuingia katika vijiji vyote 12,318, lakini vilevile na vitongoji 33,657 ikiwa ni asilimia 52.3 ya vitongoji vyote nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika miradi jimboni kwangu nataka nikiri kwamba, kama kuna jimbo ambalo limepata miradi mingi, ni pamoja na Jimbo langu la Mwibara. Kwa upande wa elimu katika kipindi cha miaka minne, tumeweza kujenga shule nane mpya za sekondari ikiwa ni pamoja na shule moja ya wasichana ya special, Mara Girls, ambayo thamani yake ni shilingi bilioni 4.4.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tumepata VETA ambayo thamani yake ni shilingi bilioni 3.3. Pamoja na hiyo, tumeweza kupata madarasa mengine mapya 315, ambayo kama ingekuwa ni shule za msingi, ukigawa katika madarasa ambayo hayana mkondo, maana yake ni kwamba, tumepata shule nyingine mpya za msingi 45 na matundu 260 ya vyoo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa afya. Jimbo langu limeweza kupata vituo vingine viwili vipya vya afya; Kituo cha Isanju na Kituo cha Kisolya. Pamoja na hivyo, huduma zime-improve ikiwa ni pamoja na kupata x-ray na ultrasound.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna zahanati mpya zimejengwa, ambazo ni Zahanati ya Mranda, Nambaza, Lagata, Mwiseni na Sozia, lakini kuna zahanati nyingine ambazo zitakamilika hivi karibuni. Kwa hiyo, naishukuru sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa barabara. Mwaka 2021 wakati tunaingia madarakani, Jimbo la Mwibara lilikuwa halipitiki kabisa, barabara zote zilikuwa kama zimekufa, madaraja yalikuwa yamepasuka hayapitiki na baadhi yalikuwa yanabeba wanafunzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtangulizi wangu aliyekuwa ametangulia, aliwahi kusema kwenye mkutano wa hadhara kwamba, hizi barabara au haya madaraja hayataweza kujengwa labda mpaka Yesu atakapokuja, lakini kupitia Serikali ya Dkt. Mama Samia haya madaraja na barabara zimeweza kujengwa katika mwaka mmoja. Nampongeza sana mama Samia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia barabara tumeweza kujenga tena barabara nyingine kuunganisha maeneo mengine. Kwa mfano, barabara ya kutoka Bugala – Sikilo, Barabara ya kutoka Nambaza – Igundu na barabara nyingine ambayo itajengwa kutoka Kalukekere – Musoma Vijijini. Hizi ni jitihada za Mheshimiwa Rais kuhakikisha kwamba, maeneo yote yanafikika kwa uhakika, lakini vilevile barabara nyingine zote sasa hivi zinapitika kwa urahisi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jimbo langu hakuna sehemu ambayo barabara haipitiki, sasa hivi unaweza ukaenda hata na IST wakati kufikia mwaka 2020 ulikuwa hauwezi kwenda hata na Land Cruser. Kwa hiyo, hali ya barabara jimboni kwangu imekuwa nzuri sana na huduma zimekuwa nzuri zaidi. Naishukuru sana Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Mama Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa maji, vilevile tumepata miradi mikubwa ya maji ikiwa ni pamoja na mradi wa kutoka Buzimbwe – Lagata na Kabainja. Mradi huu unategemewa kukamilika hivi karibuni. Vilevile kuna mradi wa Isanju – Nyalugoma ambao umeshakamilika na vilevile kuna mradi mkubwa ambao umemaliziwa kusanifiwa, mradi ambao utapitia katika vijiji 33 ambao vilevile ukiwa katika kata sita ambazo ni Kata Kisolya, Nampindi, Igundu, Nansimo, Chitengule na Kibara. Mradi huu utakapokamilika utakuwa ni game changer kwa ajili ya kutatua changamoto ya maji katika Jimbo la Mwibara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mafanikio hayo, bado jimbo langu lina changamoto. Changamoto ya kwanza ni maji. Kama nilivyozungumza, kuna mradi wa maji ambao umekamilika kusanifiwa, lakini bado haujakamilika. Kwa hiyo, maeneo yote ambayo bado mradi haujaanza, maana yake ni kwamba yana matatizo ya maji. Naiomba sana Serikali ifanye kila iwezalo ili mradi huu uweze kujengwa na kukamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine ni kwenye kilimo. Kilimo ni sekta muhimu sana katika jimbo langu ambayo inasaidia wananchi wengi katika kupata kipato chao. Pamoja na kwamba jimbo langu kila kata imegusa kwenye maji, lakini bado tuna tatizo la maji sehemu nyingine nyingi. Hivyo, naomba Serikali itusaidie kujenga scheme za maji; na hii nimeshaongea na Mheshimiwa Waziri Bashe, tupate scheme za maji katika maeneo ya Kisorya, Mwitende, Kigaga, kuna Bulamba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukishapata hizi schemes nina imani kwamba hatutakuwa na haja tena ya kuomba vyakula Serikalini. Kwa hiyo, naomba Serikali itusaidie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni kuhusu umeme. Ni kweli kwamba vijiji vyote 12 vimepata umeme, lakini bado kuna vitongoji havijapata umeme. Kama ujuavyo umeme ni kila kitu sasa hivi katika maisha, tunaomba Serikali itusaidie umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile katika umeme, nataka nimkumbushe Mheshimiwa Waziri Mkuu, na hii ni Wizara yake. Aliahidi mwaka 2020 wakati akiwa anafanya ziara jimboni kwangu kwamba ataipatia Nafuba umeme wa sola. Kwa hiyo, kwa sababu Mheshimiwa Waziri Mkuu naye yupo hapa, nafikiri atasikia na nina imani kwamba tutapata umeme hivi karibuni katika hilo eneo la Nafuba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni mawasiliano. Jimbo langu vile vile lina visiwa vingi ikiwa ni pamoja na Nafuba, Buguma, Sozya na sehemu nyingine. Kutoka kwenye hivi visiwa kuja nchi kavu, kuna tatizo kubwa la usafiri. Serikali imeniahidi mara kadhaa kuhusu kunipatia vivuko. Naomba sasa Serikali itekeleze ahadi zake ili tupate vivuko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja tena katika upande wa elimu. Pamoja na kwamba tumepata shule mpya nyingine nane, lakini bado tunahitaji. Upande wa elimu, bado haijakaa vizuri. Kuna shule kongwe ambazo madarasa yake yamechakaa sana, naomba Serikali ianze kutusaidia kurekebisha madarasa hayo katika shule za Chitengule, Nansimo, Namibo A, Kinkombyo, Namhula Stoo, Kabainja, Ragata na Buzimbwe. Ukienda katika shule hizi, hali yake siyo nzuri, madarasa kabisa ni kama hayatakiwi...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Muda wako umeisha, malizia.

MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali itusaidie katika kuboresha haya madarasa kwenye hizi shule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile tunahitaji minara ya simu. Bado mawasiliano siyo mazuri katika jimbo langu. Kwa hiyo, tunahitaji minara mingine mingi ya simu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa afya, bado tuna upungufu wa madaktari, wauguzi na vifaatiba. Tunahitaji tena bado tupewe vituo vingine vya afya. Kuna ahadi za Serikali mwaka 2024 wakati wa ziara ya Mheshimiwa Waziri Mkuu katika jimbo langu...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kajege...

MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie dakika moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2024 wakati wa ziara ya Mheshimiwa Waziri Mkuu jimboni kwangu aliahidi kwamba kutajengwa kituo cha afya katika sehemu za Bulamba. Kituo hicho bado hakijajengwa. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri Mkuu atekeleze ahadi yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, na hivyo naunga mkono hii hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. (Makofi)